Friday, March 21, 2014

HAUJAKATALIWA


                                                           

 

  1. Kut 17: 3-7
  1. Rum 5: 1-2.5-8
  1. Yn 4: 5-42

 

“Kuzomewa kunasikika sana kuliko kushangiliwa,” alisema Lance Armstrong.  Kama wewe umezomewa, umesemwa, umekataliwa na watu kumbuka Mungu wetu ni Mungu wa fursa nyingine, nafasi nyingine, Mungu hajakukataa.  “Nachukulia kukataliwa kama mtu anayepiga vuvuzera masikioni mwangu kuniamsha ili kuendelea na safari badala ya kurudi nyuma,” alisema Sylivester Stallone. Katika maisha tunkumbana na visa vya kukataliwa. Ombi la kazi kukataliwa. Ombi la kuongezewa mshahara kukataliwa. Ombi la uchumba kukataliwa. Hoja zako kwenye mkutano kukataliwa. Maoni yako kukataliwa. Lakini Mungu hajakukataa.

Katika Biblia tunasoma: “Mara hapo wafuasi wake walirudi na wakashangaa kumkuta anasema na mwanamke” (Yohane 4: 27). Mwanamke huyu alikuwa Msamaria. Alienda kuchota maji saa sita mchana kwenye Kisima cha Yakobo. Alijitahidi kukwepa wanawake wengine. Historia yake ilikuwa mbaya. Alikwepa majungu. Alikwepa kuyoshewa kidole. Alikwepa watu. Alikuwa na wanaume watano kabla na aliyekuwa naye wakati huo hakuwa mme wake. Wafuasi wa Yesu walishangaa kumkuta anaongea na mwanamke wa aina hii. Licha ya kukataliwa na wasamaria ni kama alikuwa amekataliwa na wafuasi wa Yesu. Kisa hiki kinatupa mafundisho yafuatayo.

Saa ambayo haumtafuti Yesu. Yeye anakutafuta. “Nilikubali wanikaribie watu wasioniuliza kitu, wanipate wale wasionitafuta” (Isaya 65:1). Yesu alimtafuta mwanamke huyu kumpa habari njema ya wakovu. Ni kama mchungaji mwema anayeacha kondoo tisini na tisa na kwenda kumtafuta kondoo aliyepotea. Yesu alimpata Zacchaeus na sio Zacchaeus aliyempata Yesu. Yesu alimtafuta Saulo (Paulo). Sio Paulo aliyemtafuta Yesu. Wakati tunapomtafuta Mungu naye anatutafuta.

Katika ubaya wako kuna uzuri. Mwanamke huyu Msamaria aliacha mtungi wake na kwenda kuwaita watu wamuone Yesu. Wamuone yule aliyemwambia aliyotenda. Wamuone Masiya. Mkwepaji watu anakuwa mtangazaji na habari njema. Kuna hadithi juu ya mitungi miwili ya kutekea maji. Muuza maji alikuwa anabeba mitungi hiyo miwili. Mmoja ulikuwa mtungi usio na ufa. Mtungi wa pili ulikuwa na nyufa tatu. Kila mara maji katika mtungi wenye nyufa yalimwagika. Mchota maji alilipwa pesa kidogo sababu hiyo. Mtungi wenye nyufa kila mara ulisononeka na kuwa na huzuni ukimwambia mteka maji kuwa unamfanya kupata kiasi kidogo cha fedha unamwaga maji njiani. Mteka maji aliuwaambia mtungi. Usijidharau. Sijakukataa. Tazama nyuma kila unapomwaga maji, unamwagilia maua ya bwana wangu na yanafanya sehemu hii ipendeze. Katika ubaya wa mtungi huu palikuwepo na uzuri. Yesu aligundua nyufa kwenye moyo, dhamira ya mwanamke Msamaria kisiwani.

Ukibadilika Mungu anakurudishia heshima ya kusikilizwa. Kadiri Bwana Yesu alivyongea na mwanamke mwanamke huyo alibadilika katika kumtabua Yesu ni nani. Kwanza alimuita wewe, baadaye Myahudi, baadaye Bwana au Sir, baadaye nabii na hatimaye Masiya. Kubadilika huku kunaakisi na kubadilika kimtazamo. Mwanamke huyo alipokimbia kutoa habari kwa watu aliowakwepa tunaambiwa: “Katika mji ule Wasamaria wengi walimsadiki kwa sababu ya neno la mwanamke yule aliyeshuhudia” (Yohane 4:39). Wasamaria walianza kuamini neno la mwanamke huyo. Kama unasimama kuongea watu wanasema wewe kaa chini au msimpe kipaza sauti. Heshima yako Mungu anaweza kuirudisha. Jambo la msingi ni kubadilika na kuacha ubaya.

Kukataliwa ni changamoto. “Watu wema wanapokufikiria kuwa wewe ni mtu mbaya, unakuwa na moyo wa kusaidia watu wabaya. Unawaelewa,” alisema Criss Jami. Usijidharau kwa vile watu wengine wamekudharau. Wewe sio bidhaa mbovu. Wewe si takataka. Wewe ni mpakwa mafuta kwa vile ulibatizwa. Inashangaza buibui anavyotengeneza utando wa kukamata wadudu lakini yeye hakamatwi. Inasemekana mwili wake unatoa mafuta ambayo hutiririka miguuni na kulainisha anapopita. Yeyote aliyebatizwa ana upako wa Roho Mtakatifu, ule uwezo wa kukwepa maovu. Lakini shida hatutumii uwezo huo. Ni kama stima au umeme. Watu wengi wanatumia stima au umeme kuona tu. Lakini unaweza kutumiwa kunyoshea nguo, kupikia, viwandani, kwenye runinga, simu, video kutaja matumizi machache.

Haujakataliwa. Mungu anakujua kwa jina. “Nitafanya na hilo neno uliloniomba, kwa maana umepata upendeleo wangu, na kwamba nakujua kwa jina lako” (Kutoka 33:17). Mungu anakupenda kama kwamba ni wewe peke yake duniani. Ukikataliwa kumbuka wewe si wa kwanza kukataliwa. Yesu alikataliwa na watu wa kijijini kwake. “Hakuna nabii mwenye kukubaliwa mjini mwake” (Luka 4:24).

ULICHOPATA KWA IMANI KITAPOTEA UKIKUFURU: Kutajwa kwa shamba na kisima cha Yakobo (Yn 4: 6) kunafunua ukweli huo. “Njiani alifika mji wa Samaria uitwao Sikari, karibu na Shamba ambalo Yakobo alimpa mwanawe Yozefu. Pale palikuwa na kisima cha Yakobo.” (Yn 4: 5-6). Kisima cha Yakobo kilikuwa karibu na Mlima Gerizimu. Yohana anataja mahali hapo penye Kisima, “kukumbusha mababu walichopata kwa imani kwa Mungu, wayahudi walikipoteza kwa kukufuru kwao,” alisema Baba wa Kanisa Theophyl. Ukiomba kupata kazi usikufuru. KAZI NI MBAYA UKIWA NAYO.

 

Saturday, March 15, 2014

USIJISAHAU, USIMSAHAU, USIWASAHAU




                                                 Jumapili ya 2 ya Kwaresima

1. Mwanzo 12: 1-4
2.  2 Timotheo 1: 8-10
3.  Mathayo 17: 1-9

 USIJISAHAU
Kama umemsahau Mungu umejisahau.” Ni methali ya Kiswahili. Wakati Yesu alipogeuka sura katika mlima Tabor Mtume Petro  alijisahahu katika masuala mawili. Kwanza alijisahau yeye na wenzake  katika suala la kusali. “Petro na wenzake walikuwa wameshikwa na usingizi, lakini walipoamka, waliona utukufu wake na wale watu wawili wakisimama naye” (Luka 9: 32).  Kuacha kusali ni kujisahau. Mtoto mmoja aliyeitwa John alikuwa anajiandaa  kusali sala za jioni alipomuuliza mama yake, “Ni lini unanishauri niache kusali kama baba alivyoacha kusali?”Mama alimweleza mtoto wake kuwa sala haina mambo ya likizo, haina kustaafu. Sala haina kuhairisha.
Pili alijisahau katika suala la kujenga vibanda. Petro alimwambia Yesu, “Mwalimu, ni vizuri kwetu kukaa hapa; tutajenga vibanda vitatu, kimoja chako, kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya.” (Mathayo 17: 4). Juu ya mtume Petro Caro Kardinali Maria Martini alikuwa na haya ya kusema. “Tilia maanani kutojipendelea kwake: vibanda ni kwa ajili ya Yesu, Musa na Eliya, wakati  mitume wanaweza kukaa nje ambako ni wazi.” Ingawa mtume Petro akujipendelea hakujipenda au alijisahau.  Marcus Tullius Cicero aliwahi kusema: “Sijawahi kusikia mtu ambaye ni mzee sana akisahau alipozika pesa yake! Wazee hukumbuka wanachokipenda: tarehe za kesi za madai, na majina ya wanaowadai na wadaiwa.” Kama tunakumbuka tunachopenda tusiwasahau watu wengine hatuna budi kuwapenda.
Mfanyabiashara anaweza kujisahau. Anatafuta pesa lakini hawezi kula vizuri au kulala mahali pazuri. Huko ni kujisahau. Mvuvi anaweza kujisahau. Wakati anauza samaki anakula chakula bila kitoweo. Fundi seremala wakati anatengeneza milango mizuri kwa ajili ya watu wengine unakuta mlango wake una matundu makubwa ya kupitisha kichwa. Mfinyanzi hulia kwenye kipande cha chungu. Ni methali ya Tanzania. Anayetengeneza vyungu vya kupikia yeye anatumia kipande cha chungu kilichovunjika. Fundi cherehani wakati anashonona mitindo mipya unakuta yeye anavaa nguo zilizochanika. Ni kujisahau. Daktari wakati anahimiza watu wengine wamalize dozi yeye akiugua anashindwa kumaliza dozi. Ni kujisahau. Unaweza kukuta mtu anauza baisikeli wakati yeye hana baisikeli. Ni kujisahau. Mwalimu anayefundisha somo la kuwekeza yeye hawekezi hata kidogo kuwekeza. Mwalimu anafundisha somo la Mipango Mikakati wakati yeye hana hata diari. Ni kujisahau. Mlinzi anaweza kujisahau. Unaweza ukagundua wizi umetokea mahali fulani lakini aliyesaidia kufanikisha zoezi hilo la kuhujumu ni mlinzi. Mwindaji anakuwa muwindwa. Kuna methali ya wahaya isemayo: Wanaolinda vibuyu vya pombe ndio wanaovivunja. Mwanampotevu alijisahau kuwa Baba yake ni Tajiri alikuwa tayari kujishibisha kwa r chakula cha nguruwe. Usijisahau wewe ni Mwana wa Mungu. Umeumbwa kwa mfano na sura ya Mwenyezi Mungu.


USIMSAHAU
Yesu usimsahau. Mto ambao usahau chanzo chake utakauka. Ni methali ya Yoruba. Yesu ni chanzo chako usimsahu. Kuna aliyesema: “Tukikutana na ukanisahau, haujapoteza chochote. Ukikutana na Yesu Kristo na ukamsahau, umepoteza kila kitu.” Mateso, shida, visitufanye tumsahau Yesu wa utukufu.  Mtume Yohane mmoja wa watatu aliandika: “Nasi tumeona utukufu wake” (Yohane 1: 14). Petro aliandika: “tulikuwa mashahidi wenyewe tulioona kwa macho yetu utukufu wake” (2 Petro 1: 16). Hii ni kumbukumbu ya kugeuka sura. Mitume kabla ya kuimarishwa na Roho Mtakatifu na kabla ya ufufuko walisahau Yesu wa utukufu, Yesu wa kugeuka sura. Petro alimfuata kwa mbali. Petro alimkana Yesu. Yohane akikumbuka vizuri Yesu wa utukufu alikuwa amesimama chini ya msalaba. Yakobo alikimbia. Usimsahau Yesu wa kugeuka sura. Katika Misale ya Waumini Chapa ya kumi ya mwaka 2008 katika kituo cha kumi na tano tunasali hivi: “Twakushukuru, ee Yesu, kwa mateso yako, lakini twakushukuru hasa kwa ufufuko wako, kwa kuwa huo ndio unaotupa hakika ya kuwa hatukuzaliwa kwa ajili ya mateso na maumivu, bali kwa ajili ya heri ya milele.” Katika maneno haya tunajifunza kuwa mateso hayana kauli ya mwisho. “Tuishi maisha yetu kama kwamba Kristo anakuja mchana huu,” alisema Jimmy Carter.
Mtakatifu Thomas Aquinas aliweka wazi lengo la Yesu kugeuka sura: “Wewe uligeuka sura mlimani, na kadiri walivyoweza, wafuasi wako walitafakari utukufu wako ee Kristo Mungu ili watakapokuona umesulubiwa waelewe kwamba mateso yako yalikuwa ya hiari, na watangaze duniani kwamba Wewe ni kweli mng’aro wa Baba.” Hapa tunajifunza kuwa Ijumaa Kuu inatangulia Jumapili ya Paska. Hapa tunajifunza kuwa mtaka cha uvunguni sharti ainame. “Imetupasa kuingia katika ufalme wa Mungu kwa njia ya dhiki nyingi” (Matendo ya Mitume 14:22).
Katika hadithi za Aesop kuna hadithi ya mbwa aliyeona sura yake ikiakisiwa kwenye dimbwi la maji chini ya miguu yake. Ingawa alikuwa ameshikilia mfupa, aliona wivu kuona mbwa kwenye dimbwi la maji akiwa na mfupa mdomoni. Alifungua kinywa chake ili kumbwekea mbwa mwingine na kuweza kumnyanganya mfupa. Utukufu kama wa Yesu wa kudumu ndio tunautafuta. Usiache utukufu huu na kukimbilia mambo yanayopita. Usiache mtego ambao umekamata ukaenda kuchungulia mtego uliotegwa.
USIWASAHAU
Watu wengine usiwasahau. Kusahau ni sawa na kutupa. Ni methali ya Kiafrika. Usiwatupe wenzako. Ukisikia mtu anasema amewatupa ndugu zake. Ina maana amewasahau. Petro alimwambia Yesu, “Mwalimu, ni vizuri kwetu kukaa hapa; tutajenga vibanda vitatu, kimoja chako, kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya.” (Mathayo 17: 4). Mt. Petro alisahau kuna watu wanawangoja chini ya Mlima.  Alisahau kuwa kuna mitume wenzake.  Yesu Kristu alitaka kuwaonesha kidogo utukufu ambao ni matokeo ya kubeba msalaba.  Ijumaa Kuu kwanza, Jumapili ya Paska baadaye.  Kula kutamu, kulima mavune.  "Mavune" maana yake " machofu".  Utukufu huu ilibidi Mt. Petro arudi chini ya mlima na wenzake waufanyie kazi.  Ukiona vyaelea vyaundwa. 
Petro hakulielewa bado neno hilo alipotamani kuishi na Kristo mlimani. Amekuwekea hayo, Petro, baada ya kifo chako lakini sasa yeye mwenyewe anakuambia: shuka kuangaika duniani, ukatumikie duniani, ukadharauliwe, ukasulubiwe duniani.Uzima umeshuka ili kuuawa:Njia imeshuka ili isikie uchovu wa duniani; chemichemi imeshuka ili kupata kiu;nawe wakataa kuteseka? (Mt. Augustino Sermo 78,6: PL38,492-493;Lk9:33). Cha bure hakipatikani. Mtaka cha uvunguni sharti ainame.
Kuwakumbuka watu wengine ni jambo muhimu. Mwizi msalabani alitaka kukumbukwa (Luka  23:42).  Wahaya wana msemo husemao, "Maji yakichemka hayasahau ubaridi."  Tusisahau makundi ya watu chini ya mlima, wenye shida, wenye matatizo.  Kuna mgonjwa wa kutembelea chini ya mlima, kuna wafu wa kuzika chini ya mlima, kuna mfungwa wa kutembelea chini ya mlima, kuna aliyeuchi ni wa kuvisha chini ya mlima.
Mtoa ahadi asiwasahau wale aliowapa ahadi. Nasi katika maisha tusiwasahau wengine.  Ahadi tunazofanya wakati wa matatizo na karaha, wakati wa matezo na masumbufu tunazisahau wakati wa raha, wakati wa utulivu.  Kukopa harusi, kulipa matanga.  Daktari alimwambia mgonjwa, “utapona lakini unaumwa sana”.  Mgonjwa alimjibu, “Tafadhali, Daktari fanya kila unaloweza kuakikisha ninapona.  Nikipona nitatoa milioni thelathini kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali mpya.”  Miezi michache baadaye mgonjwa huyo alipokuwa amepona kabisa daktari alimkumbusha ahadi yake: “Ulisema ukipona utatoa msaada wa milioni thelathini?”  Mgonjwa aliyepona alishangaa, “Kama nilisema hivyo, nilikuwa mgonjwa kweli.”   Mgonjwa aliyepona alimsahau daktari.
Mwalimu usiwasahau wanafunzi ni wateja wako wanakutegemea uwape elimu. Wanafunzi wanahitaji msaada toka kwa walimu kutokana na visa vifuatavyo: Mwalimu wakati wanaandikisha wanafunzi wa kujiunga na kidato cha kwanza. Mwalimu alimwambia mwanafunzi: “ Nitajie majina ya baba yako na mama yako. Mwanafunzi alijibu.” Majina yao ni Dadi na Mami.”  Katika kisa kingine mwalimu alimuuliza mwanafunzi: “Taja vitu viwili ambavyo havikuwepo miaka mia moja iliyopita.” Mwanafunzi alijibu: “Ni mimi na wewe.” Lakini binadamu si kitu. Mwalimu alimuuliza mwanafunzi: “Mama mdogo kwa Kiingereza anaitwaje?” Mtoto alijibu: “Anaitwa – minimum.” Na mama mkubwa anaitwaje?” mwalimu aliendelea kuuliza licha ya mwanafunzi kukosea. Mwanafunzi alijibu anaitwa maximu.” Mwanafunzi alikosea. Wanafunzi wanahitaji kusaidiwa.
Mwanasiasia usiwasahau wapiga kura wapo chini ya mlima wanakungoja.  Daktari, nesi, mganga, muuguzi usiwasahau wagonjwa. Wagonjwa wana hofu zao wengine hawaelewi. Kuna mtu mmoja alikuwa anatoka Hospitalini analia. Karibu na lango palikuwa na mgonjwa anaingia akauliza kwa nini unalia. Mgonjwa akasema wamekata kidole changu wakati wanatoa damu ili kuipima. Mgonjwa mwingine wa kiume akashtuka na kusema: “Mimi itakuwaje maana naenda wapime mkojo.” Mchungaji usiwasahau kondoo wako. Wakristu msiwasahau wachungaji.  Mtawala usiwasahau wale unaowatawala. Mzazi usiwasahau watoto wako. “Kuku mwenye vifaranga hamezi mnyoo.” Ni methali ya kisukuma. Watoto msiwasahau wazazi wenu. “Hujui kama unawapenda wazazi wako mpaka hapo wanapokufa.” Ni methali ya Namibia.
Mwanandoa usimsahau mwenzi wako wa ndoa. Kula umbakizie.  Mkumbuke. Usitake kwenda mbinguni peke yako. Ilikuwa ni wakati wa roho kuingia mbinguni. Watu waligawanywa kulingana na hali zao za maisha; hivyo, watu wa ndoa, watawa, mapadre, na watu wasio na miiito hiyo ya ndoa, utawa na upadre walikusanywa pamoja. Lango la mbinguni lilikuwa na mlango kwa kila hali ya maisha. Watu wa ndoa kwa mfano, walipaswa kuingia kupitia mlango wa kwanza. Hata hivyo mwanamume mmoja ambaye ndoa yake iliishatenguliwa kwenye mahakama ya serikali, zamu yake ya kuingia ilipowadia, alikuta kwamba mlango haufunguki tena.  “ Malaika”, alimwita mlinda mlango, “Nimejaribu kufungua huuu mlango kwa ufunguo wangu, lakini haufunguki”. “Mke wako yuko wapi ?” Malaika aliuliza. “Nilimpa talaka.” “Basi inabidi umtafute.” “Lakini sijui aliko!” alijibu mwanaume. “Heri ungelijua”, alisema malaika. “Lango la mbinguni kwa watu wa ndoa laweza kufunguliwa tu kwa funguo mbili’. “Lakini mke wangu ana nini la zaidi?” aliuliza kwa uchungu. “Bwana”, malaika akajibu, “ufunguo mwingine wa mlango anao yeye. Unahitaji ufunguo wake ili mpate kuingia pamoja”. (Angalisho Katika Kanisa Katoliki hakuna talaka. Panaweza kuwepo kutengana kwa muda. Au ndoa kubatilishwa kwa maana ya kutangazwa ndoa haikuwepo ni null and void)
Wakopaji msiwasahau waliowakopa. Isiwe kukopa arusi kulipa matanga. Tulio hai tuwakumbuke marehemu. Tuwaombee tusiwasahau.
HITIMISHO
Kumbuka kukumbuka. Kugeuka sura ni tukio linaloimarisha imani. “Tukio hili liliimarisha imani ya Mitume hao watatu kwa Bwana wetu Yesu. Bwana alijua kwamba imani yao itajaribiwa vikali sana baadaye watakapomwona bustanini katika mahangaiko makubwa, na hasa atakapokuwa anateswa na kuuawa msalabani. Kwetu sisi, hii ni nafasi ya kuiamsha upya imani yetu kwa Kristu Bwana wetu Msulubiwa na Mfufuka, ambaye heri yake tunatumaini kuishiriki baadaye. Kulitafakari fumbo hili kutujalie picha fulani ya heri hiyo ijayo.” (John Kabeya, Maisha ya Watakatifu, uk. 270). Yesu ni mfariji mateso tunayopitia. Unaweza kumweleza mtoto sababu za  kundugwa sindano nesi anapokuja kumdunga sindano anakimbia kumwendea mama yake. Kufarijiwa hakuhitaji sababu bali kujua kuna mfariji. 
Kuwa na utamaduni wa kupiga picha. Piga picha ya utukufu wa Kristo. Katika somo la kwanza tunaona utamaduni wa kupiga picha Mungu akamleta nje Abramu, akasema: “Utazame mbinguni, uhesabu nyota, kama waweza kuzihesabu. Akamwambia: Ndivyo uzao wako utakavyokuwa. Abramu akamwamini Bwana” (Mwanzo 15: 5-6).  Unapoomba kitu piga picha yake akilini.
Usimsahau Mungu katika kila kitu, hata kabla na baada ya kula. Kuna kijana alimwambia mwenzake mbona haukusali kabla ya kula. Mwenzake akamjibu hakuna haja mama anapika chakula kizuri sana. Kusahau kusali ni kujisahau na kumsahau Mungu. Toa huduma nzuri ulipo. Mhudumu katika hoteli moja alimwambia mteja. “Wewe na ni mara yako ya kwanza kuja hapa.” Mteja aliuliza: “Unajuaje?” Mhudumu alijibu: “Hapa mteja anayekula chakula harudi tena.” Huenda sababu mteja haudumiwi vizuri.

Saturday, March 8, 2014

PAMOJA NA YESU HAKUNA KUSHINDWA PAMOJA NA SHETANI HAKUNA KUSHINDA


                               JUMAPILI YA 1 YA KWARESIMA MWAKA A
 

1. Mwanzo 2: 7-9, 3: 1-7
2. Warumi 5: 12-19
3. Mt. 4: 1-11

 

 UTANGULIZI

Ukiwa pamoja na Yesu hakuna kushindwa. Ukiwa pamoja na shetani hakuna kushinda. Shetani hana meno ya kuuma.  Lakini Shetani ni mjanja. Ni mwerevu. Ni mdanganyifu. Ni mwenye kuahadaa. Ni mwenye ghiliba. Ni mwenye hila. Ni muongo. Ni mwasi. Ni mwovu. Ni adui. Ni Baba wa uongo. Lakini UKWELI ni ngao dhidi ya uongo wa shetani. Ni baba wa njia za mkato ambazo zinageuka na kuwa njia ndefu. Ni vizuri kujua ukweli huu, “Shetani ana uwezo wa kupendekeza jambo baya lakini hakupewa uwezo wa kukulazimisha kulitenda” (Mt. Cyril wa Yerusalemu.” Shetani alipendekeza mambo mbalimbali kwa Yesu lakini hakushinda.

 
Hadithi: Kuna mtoto aliyekuwa anawatupia watu Kanisani mawe madogo sana – changarawe padre alipomwagalia yeye alisema, padre endelea na mahubiri yako mimi nakusaidia watu wasisinzie. Shetani anaweza kupendekeza uje Kanisani lakini anaweza kukwambia sinzia kidogo.

 
SHETANI YUPO

Shetani wa mtu ni mtu. Methali hiyo inatumiwa na watu kuonyesha kuwa shetani hayupo. Mbaya wa binadamu ni binadamu mwenziwe. Je shetani yupo? Jorge Kardinali Medina alijibu swali hilo tarehe 26 Januari 1999, “Yeyote anayesema shetani hayupo sio muumini tena.” Shetani yupo ingawa hatumuoni. Kuna vitu maishani ambavyo vipo ingawa hatuvioni. Mfano, microwave (wimbi maikro), ultravioletrays (miali isiyoonekana kwa jicho), upepo upo lakini hatuoni. Ingawa shetani yupo lakini ni mfungwa. Mt. Augustini anamlinganisha shetani kama mbwa aliyefungwa kwenye myororo anaweza kukuhumiza ikiwa utamkaribia. Lakini kuna ambao wanamuona shetani kila mahali. Wakisikia paka anato sauti isiyo ya kawaida wanasema, huyo ni shetani maana sauti hiyo siyo ya kawaida.

 

 

SHETANI NI MJANJA

Shetani ni mjanja. Ni mwerevu. Ni mdanganyifu. Ni mwenye kuahadaa. Ni mwenye ghiliba. Ni mwenye hila. Ni muongo. Ni mwasi. Ni mwovu. Ni adui. Ni Baba wa uongo. Ni baba wa njia za mkato ambazo zinageuka na kuwa njia ndefu. “Shetani ana uwezo wa kupendekeza jambo baya lakini hakupewa uwezo wa kukulazimisha kulitenda.” (Mt. Cyril wa Yerusalemu.”

 

Shetani ni mpenda giza. Lakini, JIBU LA GIZA NI MWANGA. Ukiwa na dhambi moyoni mwako unakuwa na giza. Shetani anapenda hilo giza. Ukiileta dhambi hiyo kwenye mwanga katika sakramenti ya kitubio unamfukuza shetani. Dhambi ni mali ya shetani. Ananusa palipo na dhambi na kuelekea huko. Ni kama kwenye chumba chako ukiwa na uchafu, mende watafurika huko maana una mali zao yaani uchafu.

 

UJANJA WA SHETANI

 

1.                                                                                                                              PENDEKEZA SHUGHULI NYINGI

 Shetani anaweza kukushawishi ili uwe na shughuli nyingi ili usishughulikie jambo lilo muhimu. Eva alikuwa msaidizi wa Adamu na Adamu msaidizi wa Eva katika raha na shida katika magonjwa na afya. Lakini Eva alipokuwa anajaribiwa na Adamu, Adamu alikuwa na shughuli nyingi hakuwa pamoja na Eva. Pengine shughuli nyingi zinaweza kuwa namna ya uvivu. Nina shughuli nyingi sitaenda Kanisani. Hapo kuna uvivu wa kwenda Kanisani.

 

2.                                                                                                                              KUTIA MASHAKA

 

Shaka ni wasiwasi. Ni babahiko. Ni tuhuma. Ni hangaiko. KUTIA MASHAKA ni mbinu anayotumia shetani. Shetani kwa mbinu hii anakubabahisha. Anakuletea wasiwasi, tuhuma na mahangaiko. Anakuweka katika njia panda. Anakuweka katikati ya mambo mawili. Unaanza kujiuliza, “Niteme! Nikitema natema utamu. Nimeze! Nikimeza nameza moto.” Shetani anawaletea mashaka wanaojua ukweli wa mambo.  Shetani alimletea mashaka Eva si kwamba alikuwa hajui ukweli wa mambo: “Ati! Hivi ndivyo alivyosema Mungu, msile matunda ya miti yote ya bustani?” Neno “ati,” linadokeza mashaka.

 

Shetani alimletea Yesu  mashaka, “Ikiwa ndiwe Mwana wa Mungu, amuru kwamba mawe haya yawe nikate,” ikiwa ndiwe mwana wa Mungu jitupe chini.”  Neno “ikiwa,” linadokeza mashaka. Padre alijibu simu, “Leta Katoni sita za whisky, nyumbani kwangu.” Padre alielewa sauti hiyo kuwa ni ya Mkristu wake. Alimjibu, “Mimi ni paroko wako.” Alitegemea Mkristu huyo aombe msamaha, badala yake Mkristu huyo alijibu, “Unafanya nini kwenye stoo ya pombe.”  

 

Shetani anaweza kukuletea mashaka wakati wa msiba na matatizo. Kama Mungu anakupenda kweli, kwanini amemchukua mke wako? Kama Mungu anakupenda kweli kwanini amemchukua mme wako? Kama Mungu anakupenda kwa nini umepatwa na maradhi ambayo yanakufanya usitoke kitandani kutwa kucha?

 

3.                                                                                                                              KUONDOA HOFU

Kuondoa hofu ni mbinu ambayo shetani hutumia kuondoa mbegu iliyopandwa moyoni. Watu hukimbia kumkwepa nyoka na nyoka hukimbia kukwepa watu.” Hiyo ni methali ya Yoruba. Inatufunulia juu ya woga na hofu. Shetani alimuondolea hofu Eva. “Nyoka akamwambia mwanamke, ‘Hakika hamtakufa.” (Mwanzo 3:4)  Shetani alipomjaribu Yesu alitaka kumwondolea hofu, “Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu jitupe chini; kwa maana imeandikwa, ‘Atakuagiza malaika zake; Na mikononi mwao watakuchukua; usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe.” (Mathayo 4: 6) Shetani alimuondolea hofu kwa kutumia Biblia. Shetani anaweza kukuondolea hofu kwa kutumia Biblia vibaya. Kuna watu wanaofanya ulevi kuwa halali kwa kutumia maneno ya Paulo kwa Timotheo, “Usinywe maji tu, bali unywe divai kidogo kwa ajili ya tumbo lako, kwani unaugua mara kwa mara.” (1 Timotheo 5: 23) Mtume Paulo wa Tarsus hapingi kunywa divai bali anapendekeza kiasi katika neno kidogo. Anapinga ulevi. Lakini kifungu hiki kinaweza kutumiwa vibaya kuendekeza tabia ya ulevi.

 

Shetani anaweza kukuondolea hofu na ukasikia sauti kwenye moyo wako inakwambia, “Ukiiba hautakamatwa.” Lakini za mwizi ni arobaini. Unaweza kusikia sauti inakwambia moyoni, “Kumtazama mwanamke kwa kumtamani sio shida.” Lakini safari ndefu huanza kwa hatua moja. Yesu alisema, “...atakayemtazama mwanamke kwa kumtamani, amekwisha zini naye moyoni mwake.” (Mathayo 5: 28) Shida sio kutazama. Shida ni mawazo unayojenga baada ya kutazama. Maana makosa huanza kwanza na kuwaza baadaye ni kutekeleza. Kuna mtu aliyemwambia mwenzake, “Nilipomuona mwanamke huyo nilitenda dhambi za mawazo.” Rafiki yake akauliza, “Kwani uliyafurahia mawazo hayo.” Mtu huyo akajibu, “Sikuyafurahia bali yalinifurahisha.” Mawazo ya kutenda kinyume na matakwa ya Mungu kama yanakufurahisha ina maana unayafurahia na hapo ni mwanzo wa kupiga mbizi katika bahari ya ubaya na uovu.  Askofu Cyril (315-387) aliyekuwa Askofu wa Yerusalemu mwaka 349 alikuwa na haya ya kusema, “Shetani ana uwezo wa kupendekeza jambo baya lakini hakupewa uwezo wa kukulazimisha kulitenda.”  Shetani akipendekeza uue hakulazimishi kuua. Shetani akipendekeza uibe hakulazimishi uibe. Shetani akipendekeza useme uongo hakulazimishi kusema uongo. Lakini ujue kuwa ukiwa pamoja na Yesu hakuna kushindwa. Ukiwa pamoja na shetani hakuna kushinda.

 

 

4.                                                                                                                              TOA AHADI

Aliwapa ahadi Adamu na Eva, “Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” Shetani alimpa ahadi Yesu, “Kisha Ibilisi akamchukua mpaka mlima mrefu mno, akamwonyesha milki zote za ulimwengu, na fahari yake, akamwambia, “Haya yote nitakupa, ukianguka kunisujudia.”

 

Ahadi ni deni. Ni kweli lakini Shetani hutoa ahadi hewa. Aliwapa ahadi Adamu na Eva, “Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” Shetani alimpa ahadi Yesu, “Kisha Ibilisi akamchukua mpaka mlima mrefu mno, akamwonyesha milki zote za ulimwengu, na fahari yake, akamwambia, “Haya yote nitakupa, ukianguka kunisujudia.”

 

 “ Lakini nyinyi, watoto, ni wake Mungu na mmekwisha washinda hao manabii wa uongo; maana Roho aliye ndani yenu ana nguvu kuliko roho aliye ndani ya hao walio wa ulimwengu.” (1 Yohane 4:4)

 

 

Kutoa ahadi ya uongo ni kuhujumu ukweli. Ni kuhujumu sera ya Mungu sera ya ukweli. Tukumbuke kuwa DINI NI BIMA KATIKA DUNIA HII DHIDI YA MOTO WA MILELE AMBAPO SERA NZURI NI KUWA MKWELI.

 

 

5.                                                                                                                              VUTA KWINGINE

Shetani anaweza kukuvuta kwingine. Anakutoa kwenye barabara kuu. PITIA BARABARA KUU MCHEPUKO SI DILI. Yesu alianza kuwafundisha wanafunzi wake kwamba ni lazima Mwana wa Mtu apatwe na mateso mengi na kukataliwa na wazee na makuhani wakuu na waalimu wa sheria. Kwamba atauawa, na baada ya siku tatu atafufuka. Yesu aliwaambia jambo hilo waziwazi. Hapo, Petro akamchukua kando, akaanza kumkemea. Lakini Yesu akageuka, akawatatazama wanafunzi wake, akamkemea Petro akisema, ‘Ondoka mbele yangu Shetani! Mawazo yako si ya kimungu ila ni ya kibinadamu.” (Marko 8: 31 – 33) Hapana tuonaona nguvu ya HAPANA. Muite Yesu. “Naye Mungu aliye chanzo cha amani hatakawia kumponda Shetani chini ya miguu yenu.” (Warumi 16:20)

 

6.                                                                                                                              KUKATISHA TAMAA

Mtu aliyekata tamaa hamlii Mungu. Haombi. Yuda Iskarioti alikata tamaa. Hakuomba msamaha. Hakutoa machozi ya toba kama Petro. Shetani anapambana dhidi ya MATUMAINI.

 

7.                                                                                                                              KUNGOJA KESHO

Shetani anatumia mbinu ya kuhairisha mambo. Anaweza kukushawishi uende Kanisani lakini ikifikia suala la kutekeleza anakwambia ngoja kidogo.

 

 

8.                                                                                                                              FANYA BUBU

Mungu wetu sio kiziwi labda kama midomo yetu imekuwa bubu. Mbwa mwitu akitaka kumuua kondoo anamkaba koo kwenye shingo hasitoe sauti kumwita Bwana wake. Shetani akitaka kutumaliza anahakikisha hatutoi sauti. Anakuzuia kusali. Shetani aliwazuia Adamu na Eva wasimlilie Mungu na kuomba msaada wake. Wakati wa ubatizo Padre humgusa mtoto masikio na kinywa kwa kidole gumba, akisema: “Bwana Yesu aliyewafanya viziwi wasikie, na bubu waseme, akujalie uweze kusikia kwa masikio neno lake, na kuungama kwa mdomo imani ya kikristu, kwa sifa na utukufu wa Mungu Baba. Amina.” 

 

Adamu na Eva hawakuwa macho pia midomo yao ilifanywa bubu na shetani. Mtakatifu Petro anatuasa, “Mwe macho; kesheni! Maana adui yenu, Ibilisi, huzungukazunguka kama samba angurumaye akitafuta mawindo. Mwe imara katika imani na kumpinga.” (1 Petro 5:8-9) Kuwa imara katika imani kunahitaji kuinua mioyo juu na kumuomba Mungu atusaidie. Kwa kawaida mateso hutazama nyuma, wasiwasi huangalia pande zote, na imani hutazama juu. Katika taabu hatuna budi kufikiri kama Mtunga zaburi aliyesema, “Ee Bwana, nakuinulia nafsi yangu, ee Mungu wangu, nimetumaini wewe, nisiaibike, adui zangu wasifurahi kwa kunishinda.” (Zaburi 25:1). Mtunga zaburi anajua atazame upande upi-upande wa juu.

 

 

HITIMISHO

 Ushindi wa Yesu dhidi ya Shetani unatupa ukweli kuwa kushinda vishawishi kunawezekana. Yesu ni mwasisi wa ubinadamu mpya. Yesu ni mwasisi wa ushindi (Mwanzo 3:15).

Counter

You are visitor since April'08