Saturday, May 24, 2014

MWISHO WA MATUMAINI NA MATUMAINI YASIYO NA MWISHO



                
                                                             JUMAPILI YA 6 YA PASKA
1. Mdo 8: 5-8, 14 -17
2. 1 Pet 3: 15-18
3. Yn 14: 15-21

“Mwe tayari sikuzote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu” (1 Pet 3: 15).
Kuna aliyekuwa anagonga jiwe kwa nyundo ili alivunje vipande vipande. Aligonga mara mia moja jiwe halikunjika akakata tamaa. Mwenzake waliyekuwa wanafanya kazi hiyo pamoja alikuja na kugonga jiwe mara moja liwe lilivunjika. Iliitajika mara ya mia na moja jiwe livunjike lakini mgongaji wa kwanza alikata tamaa. Kukata tamaa ni mwisho wa matumaini. Mtume Petro anatutaka tuikie wito huu: “Mwe tayari sikuzote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu” (1 Pet 3: 15). Tumaini lililo ndani yetu ni hili: Maisha pamoja na Yesu ni matumaini yasiyo na mwisho, bila yeye, ni mwisho usio na matumaini. Tumaini letu ni hili:  “Sitawaacha ninyi yatima” (Yn 14: 15-21). Matumaini hayamuui yeyote.” Hii ni methali ya Kongo. Ingawa matumaini hayaliwi kama chakula hatuwezi kuishi bila matumaini. “Matumaini ni nguzo ya dunia.” Ndivyo isemavyo methali ya Kiafrika. Matumaini ni kumpokea Roho Mtakatifu. “nao wakampokea Roho Mtakatifu” (Mdo 8: 17). Kukata tamaa ni kumkataa Roho Mtakatifu.

MATUMAINI NI MTAZAMO CHANYA
Watu wanapokwambia, “Kata tamaa,”  matumaini yanasema, “jaribu tena.” Watu wanapokwambia, “nusu glasi haikujaa,”  matumaini yanasema, “nusu glasi imejaa.” Watu wanapokwambia, “matatizo ni mengi,”  matumaini yanasema, “yana mwisho” Watu wanapokwambia, “mlango wa kazi umefungwa,”  matumaini yanasema, “Mungu anafungua mlango mwingine.” Siku moja nilikutana na msichana niliyesoma naye Chuo Kikuu. Alikuwa na mimba. Aliniambia Mungu amemfungulia mlango, dirisha na madirisha madogo. Niliuliza namna gani aliniambia kuwa baada ya kumaliza masomo chuo kikuu alipata kazi. Pili alimpata mme bora. Tatu alikuwa na mimba. Mungu wetu si kuwa anaweza kukufungulia mlango tu bali anaweza kukufungulia milango na madirisha. Endelea kuvumilia na endelea kuamini ukitafuta suluhisho la shida. Endelea kutumaini.
MATUMAINI NI SILAHA
Shetani alitumia mateso, misiba, balaa, na mikosi kumkatisha Ayubu tamaa. Lakini ayubu hakukata tamaa. “Hapo Shetani akaondoka mbele ya Mwenyezi Mungu, akamtesa Ayubu...Mkewe akamwambia, ‘Bado tu ungali ukishikilia unyofu wako? Mtukane Mungu, ufe? Ayubu akamjibu mkewe, “...Tukipokea mema kutoka kwa Mungu, kwa nini tukatae kutoka pia mabaya kutoka kwake?” (Ayubu 2: 7-10). Ayubu alitumia silaha ya matumaini kwa Mungu katika mapambano yake na shetani. Matumaini yamebeba uvumilivu. Mvumilivu hula mbivu. Kupata pancha sio mwisho wa safari.  Matumaini yamebeba subira. Subira yavuta heri.
YESU NI SHUJAA WA MATUMAINI
Maisha pamoja na Yesu ni matumaini yasiyo na mwisho, bila yeye, ni mwisho usio na matumaini. Yesu alipokuwa msalabani alivumilia sababu alikuwa na matumaini katika ufufuko na katika ushindi. Makuhani wakuu, waandishi, na wazee walimcheka wakisema, “Aliwaokoa wengine, kujiokoa mwenyewe hawezi. Kama ni mfalme wa Israeli, basi ashuke sasa msalabani, nasi tutamsadiki” (Mathayo 27: 42). Yesu hakushuka toka msalabani. Ni kama unamwambia askari atoke uwanja wa vita ili umwamini kuwa ni askari. Ni kama unamwambia mwanandoa atoke kwenye ndoa ili umwamini kuwa ameolewa. Ni kama unamwambia mwanafunzi aache shule ili umwamini kuwa yeye ni mwanafunzi. Yesu hakushuka toka msalabani alivumilia. Matunda yake ni kwamba kwa uvumilivu wake alituonyesha njia.Hakuna Jumapili ya Paska bila Ijumaa Kuu. Alitukumboa. Fikiria stampu kwenye barua. Manufaa yake yapo katika uwezo wake wa kubaki kwenye bahasha mpaka bahasha imfikie mlengwa. Huo ni mfano wa nguvu ya uvumilivu wa kulishughulia jambo kwa muda mrefu bila kuliacha.
MATUMAINI NI HITAJI LA BINADAMU
Matumaini yetu yawe kama nywele na kucha. Haijalishi unazikata mara ngapi haziachi kuota. Hata ukiwa kwenye matatizo kuwa na matumaini. Matatizo ni giza la kukusaidia kuona nyota.   Katika giza la matatizo uwe na matumaini. Ukitembea  usiku wenye giza unaona nyota. Katika mtazamo huo Stephanie Meyer  alisema: “Napenda usiku. Bila giza tusingeona nyota.”  Katika matatizo unahitaji kuwa na matumaini. Usikatishwe tamaa na giza la maneno ya kukukatisha tamaa. Baba wa Uchimbaji mafuta Edwin L. Drake aliambiwa mwaka 1859: “Unataka kuchimba mafuta? Unamaanisha kuchimba ardhi ukitafuta mafuta utakuwa umerukwa na akili!” Kilichofuata ni historia bwana huyo hakusikiliza maneno ya kukatisha tamaa. Katika yote unahitaji matumaini. Ni kweli alivyosema Louise Phillipe: “Giza linapokuwa giza nene, nyota inaangaza sana.”
Biblia yasema: “Kabila lililotembea gizani limeona nuru kuu” (Isaya 9:2). Katika kutembea gizani unaweza kuona nyota. Wana wa Israel waliogandamizwa na kuteswa katika giza la mateso waliona nuru kuu. “Nyakati za balaa mbaya sana na machafuko zimekuwa nyakati za uzalishaji kwa watu wanaofikiri sana. Chuma kisichokuwa na uchafu kinatolewa penye joto jingi sana. Radi inayoangaza sana inatokana na wingu na dhoruba jeusi sana,” alisema Charles Caleb Colton.  Kumbe matatizo ni giza la kusaidia kuona nyota. Vitu vingi vimevumbuliwa kutokana na matatizo. Waisraeli katika matatizo makubwa ya ukame wamegundua kilimo cha umwagiaji kwenye shina la mche tu. Wanazalisha matunda na kuuza nchi za nje nchi yenye ukame. Katika matatizo ya giza umeme umevumbuliwa. Tulizoea kusema barua nu nusu ya kuonana. Katika matatizo ya kutoonana sasa kumevumbuliwa namna ya kuonana kupitia Skype. Sio vizuri kuwa na matatizo ukabweteka. Pengine si vizuri sana kuongejea giza ili uone mwanga. Methali ya Kifaransa inasema: “Yeye anayengojea kuvaa viatu vya marehemu anaweza kutembea pekupeku kwa muda mrefu.
Katika matatizo makubwa tunaweza kutambua uwepo wa Mwenyezi Mungu. Tunaweza kumwona Mungu. Biblia yasema: “Usifurahi juu yangu, ewe adui yangu, maana nikianguka, nitasimama tena, nikikaa katika giza, Bwana ni mwangaza wangu” (Mika 7:8). Katika giza utamwona Bwana mwangaza wako. Matatizo uliyonayo ni mwaliko wa kuwa na matumaini. Geuza hasi iwe chanya. Badili sumu iwe dawa. Badili jangwa liwe msitu. Badili mlima uwe tambarare. Penye giza washa mshumaa. Penye chuki panda upendo. Katika mto usiopitika jenga daraja.
Matumaini yawe mtaji wako na raslimali yako kwamba inawezekana.  Matumaini yatakuletea furaha katika giza la matatizo. “Kwa tumaini,mkifurahi katika dhiki, mkisubiri” (Warumi 12:12). Matumaini yetu yaendane na hali halisi yasionekane kama kichekesho. Kuna mpagaji aliyeulizwa: “Lini utalipa malimbikizo ya kodi ya chumba?” Alijibu: “Muda mfupi baada ya kupokea cheki  ambayo mchapishaji wa kitabu changu atanipa nitakulipa. Hii itategemea kama atakubali  kuchapisha kitabu hicho ambacho napanga kuandika nitakapapata jambo la kuandika juu yake na wazo fulani.” Ndoto zifanyiwe kazi. Kama una ndoto ya kujenga ghorofa angani anza kujenga msingi kuanzia chini. “Si kwamba mambo ni magumu ndio maana hatuthubutu, ni kwa sababu hatuthubutu ndiyo maana mambo ni magumu,” alisema mwanafalsafa Seneca.
“Namna tunavyoona tatizo ni tatizo,” alisema Stephen R. Covey. Unaweza kuona tatizo ni giza tu. Namna hiyo ya kuona ni tatizo. Lakini unaweza kuona tatizo kama giza la kukusaidia kuona nyota. Kumbe tatizo si tatizo. Tatizo ni namna tunavyoliona tatizo. Nchi zilizoendelea zimekabiliana na matatizo makubwa kwa mtazamo ambao si tatizo. Tunaweza kusema matatizo makubwa maendeleo “makubwa”. Mateso mengi na neema nyingi. Kumbuka kuwa penye matatizo kuna neema. Penye hasi kuna chanya. Penye kivuli kuna mwanga. Painapo ndipo painukapo.
USIKATE TAMAA PANCHA SIO MWISHO WA SAFARI
La kuvunda halina ubani. Maji yakimwagika hayazoeleki. Ni methali za kukatisha tamaa. Methali hizi zina maana  kuwa jambo likiharibika haliwezi kurekebishwa. Harufu mbaya ya uozo wa tabia haizuiwi. Kwa shetani la kuvunda halina ubani. Kwa Mungu la kuvunda lina ubani. Kwa shetani maji yakimwagika hayazoeleki, kwa Mungu maji yakimwagika yanazoeleka. “Hakuna jambo lisilowezekana kwa Mungu.” (Luka 1: 37) Mbinu ya nne ambayo shetani huitumia kuwafanya watu washindwe kutenda mazuri wengine wajiue ni kukata tamaa.
Shetani alitumia mbinu hii ya kukata tamaa kwa Yuda Iskarioti ambaye alimuuza Yesu baadaye Yuda Iskarioti alijiua. Tunasoma hivi katika Biblia, “Shetani akamwingia Yuda aitwaye Iskarioti...akaenda, akajadiliana na makuhani wakuu na walinzi wa hekalu kuhusu atakavyomsaliti Yesu kwao.” (Luka 22: 2-4) Maandiko haya yanasema Shetani alimuingia Yuda. Shetani alitumia mbinu yake ya kukata tamaa. “Yuda...alipoona kwamba wamekwisha mhukumu Yesu...akazitupa zile pesa hekaluni, akatoka nje, akaenda akajinyonga.” (Mathayo 27: 3-5) Yuda Iskarioti aliona kuwa mipango yake imeharibika alikata tamaa. Tatizo la dhambi ni kuwa mtu anaweza kuchukia hata zile pesa ambazo hakupata kwa njia ya halali. Yuda alichukia zile pesa. Kama Yuda Iskarioti angeomba msamaha tungekuwa na historia nyingine labda ya Mtakatifu Yuda Iskarioti Msimamizi wa Benki, Msimamizi wa watunza pesa  na Msimamizi wa Taasisi za Pesa. Alikata tamaa na kukosa matumaini ya kusamehewa.
Kuna methali ya wamaasai isemayo, “matumaini sio sawa na kukuta tamaa.” Mtu ambaye amekata tamaa hamlilii Mungu. Yuda hakumlilia Mungu. Mtu aliyekata tamaa hatafuti na haombi msamaha. Maisha yakikosa malengo yanakosa na maana. Namna hiyo sababu ya kuishi inaweza kuponyoka toka mikononi mwa mtu. Matumaini ni kinyume cha kukata tamaa.

Saturday, May 17, 2014

KUULIZA SI UJINGA



                                                
                                                  JUMAPILI YA TANO YA PASKA
Mtume wa Yesu Thomasi alimuuliza Yesu: “Bwana, hata uendako hatujui; basi, twaijuaje njia?” (Yohane 14: 5).
Anayeuliza njia hatakosa njia. Ni methali ya Kiswahili. Kuuliza ni msingi wa kujua. Kuuliza ni msingi wa hekima. “Ufunguo wa kwanza wa hekima ni kuuliza kwa uangalifu na mara nyingi …kwa kuwa na mashaka unauliza na kwa kuuliza unafikia ukweli,” alisema Peter Abelard mwanafalsafa wa Kifaransa (1079 – 1142). Kuna mtoto aliyemuuliza maswali mengi baba yake kama: Baba lami inatengenezwa na nini? Baba kwa nini Mungu ameficha madini mbali sana? Baba kiberiti kinatengenezwaje? Baba mimi nilitoka wapi na namna gani? Baba yake akamwambia mtoto mimi ningewasumbua wazazi wangu kwa maswali mengi kama haya ingekuwaje? Mtoto akamjibu: “Ungepata majibu ya kunijibu.”  “Mtoto anaweza kuuliza maswali elfu moja ambayo mtu mwenye busara sana hawezi kujibu,” alisema Jacob Abbott. Nakubaliana na Charles Proteus Steinmetz aliyesema: “Hakuna mtu yeyote anageuka mpumbavu isipokuwa akiacha kuuliza maswali.” Huyu alikuwa mwamerika mwenye asili ya Kijerumani (1865 – 1923).
Mtume wa Yesu Thomasi alimuuliza Yesu: “Bwana, hata uendako hatujui; basi, twaijuaje njia?” (Yohane 14: 5). “Kuuliza si upumbavu ni tamaa ya kusikiliza yote vizuri kabisa.” Ni methali ya Kilozi. Mtume Thomasi Msimamizi wa Watafiti alikuwa na tamaa ya kusikiliza vizuri. Yesu alimjibu: Mimi ni Njia Ukweli na Uzima.  Wahaya wa Tanzania wana methali isemayo: Kuulizia njia wakati umekanyaga kwenye njia hiyo. Thomasi alipoulizia njia alikuwa kwenye njia ya Yesu. Wanafunzi wa Yesu walijulikana kama Wanafunzi wa Njia. Yesu alisema kuwa yeye ni Njia. Swali la Mtume Thomasi lilikuwa swali la msingi. Methali ya Kiswahili inasema yote: Usiende bila kuuliza. Mtume Thomasi alijua kama isemavyo methali ya Uganda: Kuuliza ni kujua. “Ukitaka jibu lenye hekima, lazima kuuliza swali lenye maana,” alisema Johann von Goethe. Thomasi aliuliza swali lenye maana na alipata jibu lenye hekima.
Wayahudi ni watu waliongolea sana njia. Katika Biblia tunasoma maneno kama haya: Njia za Mungu si njia zetu. “Patakuwepo na barabara kuu, nayo itaitwa njia takatifu: wasio safi hawataruhusiwa pale” (Isaya 35:8). Njia inaweza kumaniisha falsafa au mtazamo mfano Njia za Mungu si njia zetu. Falsafa ya Yesu ni Ijumaa Kuu kwanza Jumapili ya Paska baadaye au dhiki kwanza faraja baadaye. Yesu yeye ni njia kwa maana hii. Fikiria huko nchi ya ugenini. Unaulizia njia. Mtu anakwambia. Chukua barabara ndogo upande wa kulia utakayokutana nayo. Ukifika kwenye makutano ya barabara panda kushoto. Nenda moja kwa moja. Utaona Kanisa upande wa kulia. Pita hapo. Usitoke barabara hiyo. Hesabu barabara ndogo nne upande wa kushoto. Barabara ya tano ndipo penyewe upande wa kulia kwake. Lakini fikiria huyo mtu uliyemuuliza anakwambia nitakupeleka mimi mwenyewe. Yesu hakutoa ushauri na maelekezo. Anatuongoza yeye mwenyewe. Hatumwambii tu juu ya njia yeye mwenyewe ni njia.
“Jambo muhimu ni kutoacha kuuliza,” alisema Albert Einstein. Mitume hawakuacha kumuuliza Yesu. Baada ya Thomasi kuuliza swali hilo Philipo naye aliuuliza: “Bwana, utuoneshe Baba, yatutosha.” Philipo alitaka kumuona Mungu kwa macho ya akili yaani kumwelewa. Mazoea ambayo huleta dharau labda yalimfanya kuuliza swali la namna hiyo. Matendo ya Yesu yalikuwa ya kimungu kama: kutembea juu ya maji, kufufua wafu, kukemea upepo na ukamtii, kuponya wagonjwa kwa neno tu, na kusamehe dhambi. Kama tunataka kumjua Mungu hatuhitaji kuifikiria njia yetu kwa mzunguko au kutumia muda mwingi katika utafiti wa pekee. Tunachohitaji kufanya ni kumwangalia Kristo, kuona alichokifanya, kusikiliza kile alichofundisha, kuangalia alivyotenda, kuangalia jinsi alivyopenda, kuangalia ni nani aliyempendelea, nani alishirikiana naye na kwa sababu gani, nani na pamoja na nani alikula chakula chake, ni nani aliyemkaripia au kumtetea, kwa sababu yeye ni sura ya kibinadamu ya Mungu. Kuna aliyesema hivi: “Mungu atajibu maswali yetu yote kwa njia moja na njia moja tu – kwa kuitaja, kutuonesha zaidi kuhusu Mwana Wake.” Mwana wake ni Yesu.
Ni katika kuuliza mambo mengi yamevumbuliwa. “Katika mambo yote, biashara na shughuli binafsi, ni jambo lenye tija kwa sasa na baadaye kutundika alama kubwa ya kuuliza kwenye mambo ambayo umeyachukulia kuwa ni ya kweli,” alisema Bertrand Russell. Kuuliza si ujinga ni kutaka kujua. “Lugha ilivumbuliwa ili kuuliza maswali. Majibu yanaweza kuwa minongono au ishara, lakini maswali lazima yaulizwe kwa sauti. Ubinadamu ulikomaa pale ambapo mtu aliuliza swali la kwanza. Kudumaa kijamii hakutokani na kukosekana kwa majibu bali kutukuwepo na msukumo wa kuuliza maswali,” alisema Eric Hoffer.Ukweli unabaki. Kuuliza si ujinga.
MASWALI NI NUSU YA MAJIBU
 “Anayeuliza mengi, atajifunza mengi, na kubaki na mengi,” alisema Francis Bacon (1561 – 1626) mwanafalsafa wa Uingereza. Methali ya Kiswahili inayapa uzito maneno ya mwanafalsafa huyo: Kuuliza si ujinga. Kuuliza swali hakumaanishi mwulizaji ni mjinga bali huonyesha kuwa angetaka kujielimisha au kujifahamisha. Ukiuliza maswali unajua mengi. Baba alimwambia mtoto wake wa miaka mitano. Wewe ni mtoto wa ajabu katika kuuliza maswali mengi. Sijui ingekuwaje kama mimi ningeuuliza maswali mengi nikiwa mtoto. Mtoto akamjibu: ungepata majibu ya kujibu baadhi ya maswali yangu. Maswali yanaweza kukusaidia kumpima mtu anayeuliza. Ni katika msingi huu Voltaire (1694 – 1778) mwandishi wa Kifaransa na mwanahistoria alisema: “Wahukumu watu kwa maswali yao, badala ya majibu yao.” Kadiri ya mwandishi huyu unaweza kugundua mjinga. “Atakuwa ni mjinga sana kwa vile anajibu kila swali analoulizwa,” alisema Voltaire.
Yesu akiwa na umri wa miaka kumi na miwili alikuwa na ufahamu wa kushangaza. Ufahamu huo ulionekana katika kuwauliza walimu wa sheria maswali. Tunasoma hivi: “Ikawa baada ya siku tatu, walimkuta hekaluni, ameketi kati ya walimu akiwasikiliza na kuwauliza maswali; nao wote waliomsikia walistaajabia ufahamu wake na majibu yake” (Luka 2:46).  Bila shaka Bwana Yesu aliuliza maswali sahihi kupata majibu sahihi. Ni kweli “ufundi na sayansi ya kuuliza maswali ni chanzo cha ujuzi  wote,” kama alivyosemaThomas Berger. Lazima katika maisha hujioji maswali mbalimbali juu ya maendeleo yako kama: Je una mtazamo chanya au hasi? Je unashindwa kupanga au unapanga kushindwa? Je umetoka wapi? Uko wapi? Unakwenda wapi? Pilipili usiyokula kwa nini inakuwasha? Je unatembea barabara kuu ya wito wako au uko kwenye mchepuko au vichochoroni? Kwa nini uliumbwa? Yaliyopita si ndwele kwa nini unaishi katika wakati uliopita? Je ya wengine sebuleni ya kwako moyoni?
Zig Ziglar aliyekuwa na ufundi mkubwa wa kutia watu moyo aliweka katika maandishi maswali kama haya: “Je unajiandalia ya kesho au unaingoja kesho? Je unajua zaidi kuhusu kazi yako, familia yako, na kuhusu wewe leo kuliko ilivyokuwa jana? Ni habari gani mpya au ufundi gani mpya umejifunza? Je unaiacha kesho itokee tu, au unachukua hatua kesho iwe unavyotaka iwe? Je unaacha jana ikufundishe au ikushinde? Je unajua kuwa mtu mwingine ana maoni mengine na yanaweza kuwa sahihi?” Alihitimisha kwa kusema: “Maswali ni majibu kweli, na ukiuliza ya kutosha nay a kweli, utaishia kwa mtu wa furaha zaidi, mwenye afya zaidi..” Ingawa anayaona maswali ni majibu, mimi nayaona maswali ni nusu ya majibu. Ni kama barua ilivyo nusu ya kuonana. Kuelewa swali ni kama nusu ya jibu. Kuuliza swali sahihi unaweza kupata jibu sahihi. Uwe kama  Anne Rice aliyesema: “Kila mara ninatazama kila mara ninauliza maswali.”  Kuuliza swali sahihi ni jambo la msingi. “Mwanasayansi sio mtu anayetoa majibu sahihi, bali ni yule anauliza maswali sahihi,” alisema Claude Lévi-Strauss. Alikazia umuhimu wa kuuliza maswali sahihi.
Sio kila swali linakuwa na matokeo mazuri. Inategemea ni swali la namna gani.  Mwanamke fulani alimwambia mme wake: haunipendi tena, maana unapoona ninalia hauniulizi kwa nini ninalia. Samahani sana maswali haya yamenifanya nitoe pesa nyingi katika kuyajibu.




Saturday, May 10, 2014

UNAVYOFIKIRIA NDIVYO UTAKAVYOKUWA




                                  JUMAPILI YA 4 YA PASKA
                JUMAPILI YA MCHUNGAJI MWEMA NA KUOMBEA MIITO
                     “Vijana wenu wataona njozi” (Matendo ya Mitume 2:17

Mdo 2: 14a. 36-41
1 Pet 2: 20b-25
Yn 10: 1-10

Picha ina thamani zaidi ya maneno 1000. Bwana wetu Yesu Kristu alikuwa fundi wa kupiga picha akilini, wa kufundisha kwa kuleta picha. Picha ya mchungaji: Yesu ni mchungaji. Si mchungaji tu ni mchungaji mwema. Anatoa uhai wake kwa ajili ya kondoo. Yesu ni mlango. (Yohane 10:7). Wachungaji huko Uyahudi walilala mlangoni mwa pango walimo wanyama ili kuzuia wanyama kama kondoo wasitoke pangoni na kuzuia wanyama wakali wasiingie pangoni. Yesu ni lango kuelekea kwa Baba.
Mtume Petro naye alikuwa bingwa wa kupiga picha akilini na kutumia lugha ya picha. “Maana mlikuwa kama kondoo waliopotea, lakini sasa mmemrudia mchungaji na msimamizi wa roho zenu” (1 Petro 2:25). Tunaona picha ya mchungaji na msimamizi. Tumuuige Bwana Yesu Kristu na mtume Petro tuwe mafundi wa kupiga picha ya wito tunaoutamani.
Piga picha akilini unataka kuwa nani. Kupiga picha akilini ni namna ya kufikiria. “Namna yetu ya kufikiri inatengeneza matokeo mazuri au mabaya,” alisema  Stephen Richards.  Wito wowote unaoutamani lazima uupigie picha. Unatamani kuwa padre au mchungaji piga picha unahubiri, piga picha unaendesha ibada. Unataka kufunga ndoa, piga picha unavikwa pete, piga picha ya arusi. Unataka kuwa daktari, piga picha unatibu mgonjwa, piga picha umevalia kama daktari. Tunasoma hivi katika Biblia: “Vijana wenu wataona njozi” (Matendo ya Mitume 2:17). Ni vizuri vijana kuwa na njozi, kuwa na ndoto. Kuna kitendawili kisemacho: usiku mzima nimetazama filamu. Jibu ni ndoto. Vijana hawana budi kuota ndoto za mchana. Ni kupiga picha ya kile unachokitaka, na unachokitamani. Alfred A. Montapert alikuwa na haya ya kusema:  “Kufanya mambo makubwa lazima kwanza kuota ndoto, halafu piga picha, halafu panga…amini…tenda!” 
 Suala la kuota ndoto na kupiga picha si la vijana tu hata wazee. Tunasoma hivi katika Biblia: “Na Wazee wenu wataota ndoto” (Matendo ya Mitume 2:17). Nakubaliana na Jack Youngblood  aliyesema: “Napiga picha akilini ya mambo kabla ya kuyafanya. Ni kama kuwa na karakarana akilini.”  Kupiga picha akilini ni kuangalia ambavyo havipo na havionekani. Tunaaswa hivi: ““Tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana” (2 Wakorintho 4:18). Kardinali Polycarp Pengo wa Tanzania alipokuwa bado kijana mdogo alienda Kanisani kusali. Siku hiyo ilikuwa ni kumbukumbu ya Mtakatifu Polycarp Askofu na Shahidi. Baada ya kutoka Kanisani alimwambia mama yake kuwa anapenda naye kuwa Askofu na shahidi. Mama yake alimwambia kuwa hawezi kuwa Askofu kabla ya kuwa padre. Yeye alizidi kusisitiza kuwa Kanisani walisema Polycarp alikuwa Askofu hawajazungumzia suala la padre. Kilichotokea ni historia. Kijana huyo amekuwa Askofu na sasa ni Kardinali Polycarp Pengo. Huu ni ushahidi wa hoja ninayoijenga: unavyofikiria ndivyo utakavyokuwa. Nakubaliana na Robert Collier  aliyesema: “Tazama mambo kwa namna ambayo ungependa kuwa nayo badala ya jinsi yalivyo,” alisema.
  Ukiwa unaelekea mahali fulani ingawa haujafika unapiga picha kukoje. Ukiomba piga picha Mungu atakupatia. Ili kupiga picha unahitaji macho ya imani. Biblia ina mifano mingi kuhusu jambo hili. Walau tuuone mfano mmoja: Mungu akamleta nje Abramu, akasema: “Utazame mbinguni, uhesabu nyota, kama waweza kuzihesabu. Akamwambia: Ndivyo uzao wako utakavyokuwa. Abramu akamwamini Bwana” (Mwanzo 15: 5-6). Mungu alimtaka Abramu apige picha. Kuamini maana yake ni mtu kuweka matumaini kwa Mungu hata kama hakuna ushahidi kwamba Mungu atafanya kitu. Kwa macho Abramu hakuwa na mtoto. Kwa macho Abramu alikuwa amezeeka. Kwa macho Sarah alikuwa amezeeka. Kwa imani uzao wao utakuwa kama nyota.
Juu ya kisa cha Abramu Joel Osteen alikuwa na haya ya kusema: “ Mungu alijua kuwa Abrahamu alihitaji picha ya ahadi katika akili yake. Abarahamu na Sarah walikuwa wamezeeka na bila mtoto, katika maumbile, ilikuwa hali ambayo haiwezekani. Lakini kila mara Abrahamu alipotozama nyota, alikumbushwa ahadi ya Mungu. Alianza kuona ahadi kupitia macho ya imani. Huwezi kuzaa ndoto ambayo  kwanza hujaiwazia. Lazima huiwazie ndani mwako kupitia macho ya imani kabla ya kuitoa nje. Badili kile unachokiona, utabadili kile unachozalisha.”
Omba “kama” kwamba” Umepata
Yesu  akawaambia, Waketisheni  Watu” (Yohane 6: 10).  Yesu aliwataka watu wakae mkao wa kula chakula “kama kwamba” chakula kimeishapatikana. Muujiza wa kuongeza mikate ulikuwa haujafanyika lakini Yesu alitenda kama kwamba. Kuna wakristu katika parokia moja hapa Tanzania walimuomba padre Jumapili iliyokuwa inafuatia iwe siku ya kuomba kupata mvua. Wakristu hao walishangazwa na padre aliposema hayuko tayari kufanya maombi ya kuomba mvua kwa vile wakristu hawakwenda na miavuli ya kujikinga na mvua. Suala la kuwa na miavuli linadokeza maana ya “kama kwamba.” Yesu aliwambia wakoma kumi waende wajioneshe kwa makuhani kama kwamba wamepona. Bikira Maria aliwaambia watumishi: lolote atakalowambieni fanyeni “kama kwamba” Yesu amekubali.
Piga picha ya kile unachokitaka. Bila shaka Bwana Yesu Kristu alipiga picha ya muujiza, picha ya ongezeko la samali wawili na mikate mitatu.  Suala la kupiga picha ni muhimu ili ufanikiwe. “Akamleta (Abramu) nje akasema:Utazame mbinguni, uhesabu nyota, kama waweza kuzihesabu.Akamwambia: Ndivyo uzao wako utakavyokuwa” (Mwanzo 15:5). Mungu alisisitiza umuhimu wa kupiga picha.
 Linda vizuri mawazo yako, mawazo yako yanasikika Mbinguni. Ukifikiria kuwa tajiri, na mwaminifu, mawazo hayo yanasikika mbinguni. Ukifikiria kuwa maskini na myonge, mawazo hayo yanasikika mbinguni. Ukifikiria kuwa mtakatifu au kutenda dhambi, mawazo hayo yanasikika mbinguni. Mtu anayefanikiwa maishani ni mshindi. Mtu ambaye anashindwa maishani ni mshinde. Mshindi anasema ni jambo gumu lakini linawezekana. Mshinde anasema, linawezekana lakini ni jambo gumu sana . Mshindi anaona jibu kwa kila swali. Mshinde anaona swali katika kila jibu. Mshindi ni sehemu ya jibu. Mshinde ni sehemu ya tatizo. Mshindi anaona jambo zuri katika kila shida. Mshinde anaona shida katika kila jambo zuri. Marehemu Edward Cole alipokuwa meneja wa Kampuni General Motors aliulizwa swali, “Jambo gani linakufanya uwe tofauti na watu wengine – kwa nini umefanikiwa kuliko maelfu ya watu na kupata kazi ya juu sana katika General Motors?”  Bwana Edward Cole alifikiri kwa muda na kujibu, “Napenda matatizo!” Katika matatizo aliona jibu. Uwe na ndoto kubwa hata kama kuna matatizo kama Yozefu wa Agano la Kale. “Usiku mmoja, Yozefu aliota ndoto, lakini alipowasimulia ndugu zake, wao wakazidi kumchukia” (Mwanzo 37: 5). Ukiwa na ndoto kubwa utachukiwa lakini usikate tamaa. Yozefu alifanikiwa. Kwa Mungu hakuna lisilowezekana. Ulivyo sasa ni matokeo ya mawazo na fikira zako. Juhudi ukijumlisha na ndoto kubwa ukajumlisha na Mungu ni sawasawa na mafanikio.  Mafanikio yako ya kesho yanategemea jambo unalolifikiria leo. Nakubaliana na James Allen aliyesema, “Leo upo pale ambapo mawazo yako yamekuleta; kesho utakuwa pale ambapo mawazo yako yatakupeleka.”
Usitazame pale tu ulipo tazama na pale unapoweza kuwa. Usitazame chini ulipo tazama na juu unapoweza kuwa. Usifikirie jinsi ulivyo, fikiria unavyoweza kuwa. Yesu alimwambia Simoni mwana wa Yohane, “Wewe ni Simoni mwana wa Yohane. Sasa utaitwa Kefa” (Yohane 1: 42). Kefa ni Petro, yaani Mwamba.  Yesu alimtia moyo Simoni awe na picha ya mwamba. Alimtia moyo afikirie kuwa yeye ni mwamba. “Watu wana namna ya kuweza kubadilika wakawa unavyowatia moyo wawe na sivyo unavyowasumbua wawe,” alisema  Scudder N. Parker.
Mtu anavyofikiria katika akili yake anakuwa hivyo, na anavyochagua anakuwa hivyo” (Methali 23: 7). Zig ziglar alisema, “picha unayochora katika akili yako, akili yako itaifanyia kazi ili kuifanikisha. Unapobadili picha zako unabadili na utendaji.”  Kila kitu ambacho unaongeza na kufungia kwa maneno haya “mimi ni ....” Utageuka kuwa hivyo. Jibariki kwa maneno haya: Mimi ni mwema. Mimi ni mwaminifu. Mimi ni tajiri. Mimi ni mvumilivu. Mimi ni mchapakazi. Mimi ni mcha mungu. Mimi ni mwamba. Mimi ni mzuri. Mimi ni mwenye busara. Mimi ni mwenye heshima. Mimi ni mpole. Mimi ni mtoto wa Muungu.Mimi ni kisura, Mungu haumbi takataka. Mungu haumbi mtumba.
Mtu ni watu. Watu wanatujenga au wanatubomoa. Picha tuliyonayo, tunavyojiona uenda imetoka kwa watu wengine, imetoka kwako, imetoka kwa neno la Mungu, imetoka kwa wazazi, imetoka kwa shetani. Lakini Yesu ana picha yake, Yesu anaona uwezekano, yanayowezakana, unayoweza kufanya. Mwanamke alikuwa anamuuliza mme wake, “Sijui huko mbinguni patakuwepo na nguo za gharama sana za wanawake?” Mme wake akajibu, “ Unataka kuniambia tukiwa mbinguni nitaangaika kutafuta pesa za kukununulia nguo.” Mwanamke akamjibu, “Usiwe na wasiwasi, usiogope, wewe hautakuwa huko.” Maneno kama hayo hayamuinui mwanaume.

Afadhali adui mzuri kuliko rafiki mbaya. Niambie rafiki yako nitakwambia tabia yako. Simoni Petro alikuwa na ndugu yake Andrea. Hawa hawakuwa tu ndugu bali walikuwa marafiki. Andrea alimleta Simoni Petro kwa Yesu. Andrea alimpa Simoni Petro picha nzuri. Kuna picha inayotoka kwa marafiki zetu. Wanavyotuona na sisi inatujengea picha tunavyojiona. Andrea alimuona Simon Petro kama mtu anayeweza kuwa mfuasi mzuri wa Yesu akamleta kwa Yesu. Katika maisha ungekuwa juu lakini marafiki zako wanapicha ya kukuweka chini. Ungekuwa mbali lakini picha kutoka kwa marafiki zako ni ya puani.  Picha ya Andrea ilikuwa ya juu.

Marafiki ambao hawakusaidii kuwa kama Yesu anavyotaka uwe, marafiki ambao hawakuinui wakiamua kukuacha waache waende: “WATU HAO WAMETOKEA KATI YETU LAKINI HAWAKUWA WA KWETU NA NDIYO MAANA WALITUACHA; KAMA WANGALIKUWA WA KWETU, WANGALIBAKI NASI. LAKINI WALIONDOKA, WAKAENDA ZAO, KUSUDI IONEKANE WAZI KWAMBA HAWAKUWA KAMWE WA KWETU” (I Yohane 2: 19).


Counter

You are visitor since April'08