Friday, December 26, 2014

GHARAMA YA KUMFUATA KRISTU




                                         SIKUKUU YA MT.STEFANO SHAHIDI
                                                         26 Desemba 2013

1.       Mate 6: 8-10, 7: 54 -59
2.        Mt 10: 17-22
 UTANGULIZI
 Jana ilikuwa “Birthday” ya Yesu Kristu. Leo ni Birthday ya Mtakatifu Stefano shahidi. Ni kuzaliwa kwa Mtakatifu Stefano. Lakini ni kuzaliwa kwake mbinguni. Sikukuu ya Mtakatifu Stefano inavumbua mbivu na mbichi katika kumfuata Yesu Kristu. Ili tuzaliwe mbinguni hatuna budi kulipa gharama. Jana Bwana alizaliwa duniani ili Stefano azaliwe mbinguni. Jana aliingia duniani ili Stefano aweze kuingia mbinguni.
  
GHARAMA YA KUMFUATA KRISTU
  
MSAMAHA
 Stefano aliwasamehe wauaji wake. Alisema, “Bwana, usiwalaumu kwa sababu ya dhambi hii” (Matendo 7:60). Msamaha ni gharama ya kumfuata Yesu Kristu. Watu hujiandaa kusamehe lakini walio wengi hawajiandai kusamehewa. Je kama unasemehewa unapokea msamaha? Bwana Yesu alipokuwa kufani msalabani alisema maneno saba msalabani: Neno la kwanza ni: “Baba, uwasamehe kwa maana hawajui wanalofanya,” (Luka 23: 34). “Kufanya makosa ni jambo la kibinadamu, kusamahe ni jambo la kimungu,” Alisema Alexander Pope (1688-1744) mshairi wa Uingereza. Lakini tujue kuwa kuendelea kutenda makosa bila kuacha ni jambo la kishetani. Yesu alivyowasamehe waliomkosea alifanya jambo la kimungu. Hakutaka kutwika uwezo wake wa kukumbuka mzigo mzito wa mambo yaliyopita. Kama yeye alifanya hivyo kwa nini sisi tunabeba mizigo mizito ya mambo mabaya tuliyotendewa.
 William Shakespeare aliandika hivi katika kazi yake iitwayo, “The Tempest,” “Prospero, alipopewa nafasi kuwaadhibu wale waliomwondoa katika nafasi yake kama mfalme, alisema, ‘Tusitwishe mzigo mzito kumbukumbu zetu kwa jambo zito ambalo limepita.” Kununa kwetu hakubadili historia. Kukasirika kwetu hakubadili historia. Kulaani hakubadili historia. Kutukana hakubadili historia. Kusamehe kunabadili historia maana hakuongezi idadi ya watu wabaya lakini kulipiza kisasi kunaongeza idadi ya watu wabaya.

Bwana Yesu ni kioo cha jamii na familia katika kutoa msamaha. Aliwatetea waliomfanyia mabaya kuwa hawakujua. Wanafamilia wajifunze toka kwa Yesu kusameheana. Maneno “nisamehe” yawe kama kiitikio katika familia. Familia ni shule ya kwanza ya kujifunza kusamehe na kupokea msamaha. Wazazi ni walimu wa kwanza wa somo la msamaha. Kama pametokea ugomvi, msamaha ufuate kama asubuhi inavyofuata usiku. Ugomvi huanza kwa kutokubali kosa na kuomba msamaha. Mfano, mtu mmoja alimwambia mwenzake, “ulitenda kosa.” Mwenzake alijibu, “sikutenda kosa.” Ugomvi ulianza na marafiki hao wawili walikasirikiana. Mmoja baadaye alisema, “Samahani naomba unisamehe.” “Na mimi naomba nisamehe pia,” alisema mwenzake. Ugomvi ulimalizika, kwa sababu ya maneno machache ya upendo.
 Kuomba msamaha na kukubali kupokea msamaha ni tiba. Karl Menninger, daktari bingwa wa magonjwa ya akili kama kichaa alisema kuwa kama angeweza kuwafanya wagonjwa kwenye hospitali ya wagonjwa wa akili kuamini kuwa dhambi zao zimesamehewa, asilimia 75 ya wao wangetoka wamepona siku inayofuata. Mzee Joe alikuwa kufani kwenye kitanda cha mahuti. Kwa muda wa miaka mingi alikuwa hapatani na Bill, ambaye zamani alikuwa mmoja wa marafiki zake. Akitaka kunyosha mambo yake kabla ya kuaga dunia alimtuma Bill waongee na kumaliza mambo. Bill alipofika, Joe alimwambia kuwa anaogopa kwenda mbinguni akiwa na kinyongo naye. Kwa kusita na kwa kujikaza Joe aliomba msamaha kwa mambo aliyoyasema na kuyatenda. Alimwaakikishia Bill kuwa amemsamehe kwa makosa yote aliyomtendea. Mambo yote yalionekana kwenda vizuri mpaka hapo Bill alipojiandaa kuondoka. Alipokuwa anatoka chumbani, Joe alimuita, “Lakini kumbuka, nikipona, haya yote niliyosema hayana maana wala uzito.”

KUSALI
Mtakatifu Stefano aliinua macho juu. Alisali. Mashaka yanatazama nyuma. Wasiwasi unatazama kila upande lakini imani inatazama juu. Tunasoma katika Biblia, “Waliendelea kumpiga Stefano kwa mawe huku akiwa anasali: “Bwana Yesu ipokee roho yangu!” (Matendo 7:59). Kusali ni gharama ya kumfuata Yesu Kristu.
Sala ni jiwe linalojenga msingi wa nyumba ya ndoa. Hoja ya msingi sio kusali tu bali kusali pamoja. Mtume Paulo anawaasa, “Mnapaswa kuwa na moyo mmoja, na fikra moja.” (1 Petro 3:8). Familia ambayo haisali ni familia iliyoasi. Mwanzo wa kuteleza kwa familia ni kudharau sala hasa sala za pamoja. Kusali hakuishii katika kusali pamoja nyumbani. Wanafamilia hawanabudi kwenda kusali pamoja Kanisani pia. Katika suala la kwenda Kanisani kusali Bwana hasimwachie Bibi yake. Hasiseme, “Sali kwa niaba yangu.” Huko mbinguni hatasema, “nenda kwa niaba yangu.”  Mbinguni ni pa wote wanaume na wanawake. Hakuna anayekunywa dawa kwa niaba ya mgonjwa. Kila mtu anawajibu wa kufanyia kazi wokovu wake.
 Mbinguni si pa jinsia moja tu. Sio kama mtoto Veronika alivyofikiri. Veronika mtoto wa miaka mitano alimuuliza mama yake, Jancita, “Mama, je wanaume huwa hawaendi mbunguni?” “Huwa wanaenda mbinguni.” Alijibiwa mtoto. Mama alitaka kujua kwa nini swali kama hilo linaulizwa. “Kwa nini Veronika unauliza kama wanaume wanaenda mbinguni.?” Alidadisi mama. “Ni kwa vile sijawahi kuona picha za malaika wenye ndevu.” “Wanaume huwa wananyolewa ndevu kabla ya kwenda mbinguni.” Alimjibu mama. Nguvu ya sala ya pamoja tunaiona katika maisha ya Tobia na Sara. “Tobia aliondoka kitandani, akamwambia mkewe, ‘Inuka,dada, tumwombe Bwana atuonee huruma na kutukinga salama.’ Sara akainuka. Tobia akaanza kusali: ‘Utukuzwe ee Mungu wa wazee wetu…Uwe na huruma kwake na kwangu utufikishe uzeeni pamoja!” (Tobiti 8:7) Tobia alifikia umri wa miaka mia moja ishirini na saba. Alifikia uzee pamoja na Sara.
 Tuwabebe wengine katika sala. Kubeba ni kuchukua mkononi, begani au kichwani. Ni kusaidia kwa kutoa mahitaji ya lazima. Tunaweza kusema anawabeba wazazi na kuwasimamia katika mahitaji yao yote. Yesu alipokuwa amefadhaika aliomba Mungu Baba ambebe. Tuwabebe wengine katika sala tuwalete kwa Yesu
 Tuwabebe katika sala watu wa makabila mengine na mataifa mengine. Filipo na Andrea wayahudi “waliwabeba” wagiriki kuwapeleka kwa Yesu (Yohane 12: 20-21). Tuwabebe watu wa makabilia mengine tuwapeleke kwa Yesu.  Hawa Wagiriki walikuwa wanatafuta na wanaangaika. Mtanzania ambebe Mkenya katika sala. Mkenya ambebe Mtanzania katika sala. Mkikuyu ambebe Mjaluo katika sala. Mjaluo ambebe Mkikuyu katika sala. Mkikuyu ambebe Mkalenjini katika sala. Mkalenjini ambebe Mkikuyu katika sala. Tuwabebe wenzetu katika sala. Mtakatifu Monica alimbeba mtoto wake Augustini katika sala. Augustini akabadilika. Ni huyu alisema, “Jinsi nilivyo ni zawadi ya Mungu kwangu. Jinsi nitakavyokuwa ni zawadi yangu kwa Mungu.”
 UNYENYEKEVU
Biblia yasema, “Akapiga magoti akalia kwa sauti kubwa” (Matendo 7:60). Kupiga magoti ni ishara ya unyenyekevu. Gharama ya kumfuata Yesu Kristu ni kunyenyekea. Kuna sababu nyingi za kunyenyekea. Kwanza sisi ni cha kupewa. “Nani amekupendelea wewe? Una kitu gani wewe ambacho hukupewa? Na ikiwa umepewa, ya nini kujivunia kana kwamba hukupewa?” 1 Kor.4:7. Mungu ametupa vipaji mbalimbali. Kuna kipaji cha lugha, kipaji cha mehesabu, kipaji cha uandishi, kipaji cha kuimba, kipaji cha kutibu na kipaji cha kucheza mpira. Lakini si busara kuwadharau wengine kwa vile unakipaji fulani. Wewe umepewa. Ya nini kujivunia kana kwamba hukupewa? Palikuwepo na Profesa aliyekuwa anavushwa na mvuvi kwenye mto. Wakiwa katikati ya mto, Profesa alimuuliza mvuvi, “Wewe mvuvi unajua kusoma?” Mvuvi alijibu, “Profesa sijui kusoma.” Profesa alisema, “Kama ni hivyo robo ya maisha yako imepotea.” Profesa aliuliza tena, “Wewe mvuvi unajua kuandika?” Mvuvi alijibu, “Profesa sijui kuandika.” Profesa alisema, “Kama ni hivyo nusu ya maisha yako imepotea.”Profesa aliuliza tena, “Wewe mvuvi unajua kuhesabu?” Mvuvi alijibu, “Profesa sijui kuhesabu.” Profesa alisema, “Kama ni hivyo umepoteza robo tatu ya maisha yako.” Wakati wanaendelea na safari upepo mkali ulianza kuvuma. Mvuvi alimuuliza Profesa, “Profesa unajua kuogelea.” Profesa alijibu, “Sijui kuogelea.” Mvuvi alisema, “Maisha yako yote yamepotea.”
 Kinyume cha unyenyekevu ni majivuno na kiburi. “Kijapo kiburi ndipo ijapo aibu.” (Mithali 11: 2)  Unyenyekevu sio kujidharau. Ni kukubali vipaji na uwezo ulio nao na kutambua kuwa hautoki kwako bali unapitia kwako unatoka kwa Mungu. USIJIVUNE SANA KINAKUDANGANYA KIOO. Dhambi ya kwanza kutendeka mbinguni ni majivuno. Lucifer aliangushwa toka mbinguni sababu ya majivuno. “Jinsi gani ulivyoporomoshwa toka mbinguni, wewe uliyekuwa nyota angavu ya alfajiri. Jinsi gani ulivyoangushwa chini, wewe uliyeyashinda mataifa!” (Isaya 14: 12) Chini ya kila kosa kuna majivuno.
 Kadili tumbili anavyopanda juu ndivyo makalio yanazidi kuonekana. Kadili tunavyopanda juu hatuna budi kunyenyekea. Hawezi kusema kama mtu fulani hayupo dunia itaacha kuzunguka kwenye mhimili wake. Itazunguka. Mlima uliaibisha kichuguu mpaka vyote viwili viliponyenyekeshwa na nyota. Mwembe ukiwa na miembe unakuwa umeinama. Ni unyenyekevu. Mwembe usio na maembe hauinami. Unyenyekevu ni mama wa wokovu “...alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe...” (Wafilipi  2: 8-10). 

Wednesday, December 24, 2014

JE UNAKUMBUKWA?



                                                  
  


                                                     NOELI USIKU
1. Isa 9: 1-6
2. Tit 2: 11-14
3. Lk 2: 1-14


“Zawadi kubwa sana maishani ni kukumbukwa,” alisema Ken Venturi. Siku ya Krismasi tunampa zawadi kubwa sana mtoto Yesu zawadi ya kumkumbuka. Siku ya Krismasi tunampa zawadi kubwa sana Bikira Maria zawadi ya kumkumbuka. Siku ya Krismasi tunampa zawadi kubwa sana Mtakatifu Yozefu  zawadi ya kumkumbuka. Siku ya Krismasi tunalipa hori zawadi kubwa sana alipozaliwa mtoto Yesu zawadi ya kulikumbuka. Hatumkumbuki meneja wa Nyumba ya Wageni aliyewanyima nafasi. Tunasoma hivi katika Biblia: “Walipokuwa huko, siku yake ya kujifungua ikawadia, akajifungua mtoto wake wa kwanza wa kiume, akamvika nguo za kitoto, akamlaza horini kwa sababu hawakupata nafasi katika nyumba ya wageni” (Luka 2: 6 -7). Kuna mambo saba ya kukumbukwa siku ya Krismasi.


Kwanza, Mtoto Yesu anapewa zawadi kubwa sana zawadi ya kukumbukwa. Kuna aliyemuuliza mtoto, “je umepata kile ulichohitaji katika Krismasi hii?” Mtoto alijibu sikupata kila nilichohitaji na kila nilichotegemea. Lakini hata hivyo siku ya leo siyo siku yangu ya kuzaliwa ni siku ya kuzaliwa Yesu Kristu.”  Ni vizuri watoto watambue kuwa Krismasi siyo siku yao ya kuzaliwa (labda kama mtoto alizaliwa tarehe 25/Desemba naye atakuwa anasherekea siku yake ya kuzaliwa) ni siku ya Kuzaliwa Yesu Kristu. Tatizo tunaweza kutekwa na kile kinachouzwa na kununuliwa tukamsahau yule aliyesababisha vitu vyenye maneno: “Heri ya Krismasi” viuzwe. Naye ni Yesu. Maneno ya kutakiana heri: Heri Krismasi; Baraka ya Krismasi; Furaha ya Krismasi yatukumbushe juu ya Yesu ambaye ni baraka kwa dunia. Kwa sababu yake kuna mabadiliko. Wafuasi wa Yesu wanafanya mengi ya maendeleo. Kuna Hospitali zimejengwa na madhehebu ya Kikristu. Vyuo vimejengwa kwa sababu Yesu alikuja. Inasikitisha kadi za Krismasi zinapokuwa hazina mchoro au “picha” ya Yesu. Krismasi bila Yesu ni bure.

Pili, Bikira Maria Mama wa Yesu anapewa zawadi kubwa sana ya kukumbukwa: Hakuna Krismasi bila Mama Maria Mama wa Yesu Kristo. “Hapa hakuwepo mkunga, hapakuwepo wasiwasi uliojaa huruma wa wanawake; alimvisha Yesu nguo za kitoto, yeye akiwa mama na mkunga,” alisema Mtakatifu Jerome. Ni kama “Mkunga” na “Nesi” katika Agano Jipya. Jambo kubwa na zuri sana ambalo baba anaweza kuwafanyia watoto ni kumpenda mama yao. Na jambo kubwa ambalo tunaweza kumfanyia Yesu mkombozi wetu ni kumpenda mama yake. Tuwaenzi wakina mama, tuwaheshimu wakina mama. Uchungu wa mwana aujuaye mzazi. Titi la mama li tamu, jingine halishi hamu. Mama ni mama ajapokuwa rikwama, hata akiwa na upungufu ni mama. Mama hamkani mwanawe japo awe kilema. Kuna watu ambao hutaka kulinganisha wakina mama. Mama wa Yesu hawezi kulinganishwa na mwanamke yeyote. Kuna Bwana mmoja aliyemwambia mke wake: “Chakula unachopika sio kitamu kama chakula mama yangu alikuwa anatupikia.” Mwanamke naye akamjibu: “Ni sawa, lakini hata mshahara wako ni mdogo ukilinganisha na mshahara baba yangu alikuwa anapata.”
Bikira Maria ni MAMA. Tafakari neno “MAMA.” Herufi ya Kwanza “M” inasimama badala ya Milioni ya vitu alivyokupa mama. “A” asante. Anastahili asante kwa mamilioni ya vitu alivyokupa. Waluhya wa Kenya wana methali isemayo: “Nyama choma haiwezi kuwa tamu sana ukasahau aliyeichoma.” Mama Maria anastahili asante kwa kukubali kumzaa mkombozi Yesu. “M” inasimama badala ya “Malezi” Mama analea mimba na analea mtoto. Mama Maria alilea mimba, mtoto Yesu akiwa tumboni. “A” inasimama badala ya “Adabu,” onyesha adabu kwa mama.

 Tatu, Mtakatifu Yozefu anapewa zawadi kubwa sana ya kukumbukwa: Jina Yozefu  linatokana na neno la kiebrania lenye maana: na aniongezee mwingine. Papa Leo XIII alikuwa na haya ya kusema juu ya Mtakatifu Yozefu, “Mtoto aliyekuwa anatishiwa na wivu wa mfalme alimkinga asiuawe na alimtafutia mahali pa kukimbilia; katika shida za safari na katika makali ya ukimbizi alikuwa daima mwenzi na msaada, mtetezi wa Bikira na Yesu.” Yozefu anakumbukwa kama baba mwema. Changamoto kwa wanaume ni kukumbukwa na watoto kama baba mwema. “Natumaini nakumbukwa na watoto wangu kama baba mwema,” alisema Orson scott Card.
Nne, Nguo za kitoto alizovikwa Yesu zinapewa zawadi kubwa ya kukumbukwa: Siku ya Krismasi tunazipa zawadi kubwa sana nguo za kitoto alizovikwa mtoto Yesu, tunazikumbuka. “Yeye aliyevisha dunia yenye uzuri wa aina mbalimbali alivikwa nguo za kawaida za kitani, ili tuweze kupokea vazi zuri sana; yeye ambaye vitu vyote vimafanyika, mikono yake na miguu  vinakunjwa ili mikono yetu iinuliwe kwa kila kazi tuifanyayo, na miguu yetu iongozwe katika njia ya amani,” alisema Baba wa Kanisa Bede. Tukumbuke vazi tulilovishwa tulipobatizwa.

Tano, Horini alipowekwa mtoto Yesu panapewa zawadi kubwa sana ya kukumbukwa: “Anafungiwa mahali padogo pa hori baya, ambaye kiti chake kilikuwa mbinguni, ili atupe chumba cha kutosha katika furaha za ufalme wa mbinguni. Yeye  ambaye ni mkate wa mbinguni analazwa horini, ili atushibishe kama wanyama walivyokuwa wanashibishwa,” alisema Baba wa Kanisa Bede. Kuingia horini ilibidi mtu kuinama, ishara ya unyenyekevu. Alitaka watakaoingia waingie kwa mtindo wa unyenyekevu. Horini alipozaliwa Yesu alizungukwa na wanyama. Kwa wayahudi wanyama kama ilivyo kwa Wamasai walikuwa ni ishara ya utajiri. Bwana Yesu alizungukwa na ishara ya utajiri kuonesha alikuja kututajirisha. Katika kupambana na umaskini ni vizuri hilo likasisitizwa vinginevyo tunaweza kuwaprogramu watu kuwa maskini (Umaskini wa kiroho ni muhimu lakini ulalahoi si muhimu). Ingawa watakatifu wengi wametokea “Slum” hatuwezi “kuendekeza” slums ili tuwapate watakatifu.

Sita, Bethlehemu alipozaliwa Yesu panapewa zawadi kubwa sana ya kukumbukwa. Hapo pamejengwa Kanisa. Bethlehemu maana yake ni nyumba ya mkate. Yeye aliyejitambulisha kama Mkate alizaliwa mahali penye maana ya Nyumba ya Mkate. “Ee Bethlehemu nchini Yudea, wewe si mdogo kamwe kati ya miji maarufu ya Yudea; maana kwako atatokea kiongozi atakayewaongoza watu wangu Israeli” (Mathayo 2: 6). Changamoto: “Kama Kristu anazaliwa mara elfu moja Bethlehemu na si katika moyo wako, umepotea milele yote,” alisema Angelus Silesius (1624-1677). Umuhimu wa mtu si mahali anapokaa na mahali anapotokea, au mahali alipozaliwa. Baraka Obama Rais wa Amerika ametokea Kijiji cha Kogelo huko Kisumu lakini sasa ni Rais wa Amerika. Hakutoka New York. Hakutokea Tel Aviv. Hakutokea London. Yesu hakutokea jiji la Yerusalemu. Alizaliwa Bethlehemu. Alitokea Nazareti, kijiji kilichodharauliwa sana kama tunavyosoma katika Biblia “Naye Nathanaeli akamwuliza Filipo, “Je kitu chema chaweza kutoka Nazareti?” Filipo akamwambia, “Njoo uone” (Yohane 1: 46).
Saba, usiku mtulivu na mtakatifu unapewa zawadi kubwa sana ya kukumbukwa. Kipindi cha Krismasi unaimbwa wimbo ambao umevuta nyoyo za watu “Silent Night” ambao umetafsiriwa kwa Kiswahili: Usiku mkuu! Usiku Mtakatifu! Uko utulivu; Bikira amezaa Mwana, Mtoto Mtakatifu ni Bwana; Alale amanini, Alale amanini.” Wimbo huu unazungumzia ukimya, utulivu, ukuu na utakatifu wa usiku alipozaliwa Yesu. Utulivu huu na ukimya huo ni wito wa kuwa na utamaduni wa kuwa kimya na kutulia. Wakati wa vita ya kwanza ya dunia Krismasi ya mwaka 1914 vikosi vyote vilivyokuwa vinapigana viliweka silaha chini na kuimba wimbo wa “Silent Night.” Kelele za bunduki zilisimamishwa. Lakini pongezi ingekuwa kama kelele hizo zingesimamishwa siku zote na sio usiku tu wa Krismasi. Utamaduni wa kutochafua hewa kwa kelele lisiwe suala la Krismasi tu. “Tunahitaji kumtafuta Mungu, na hapatikani katika kelele na kutotulia. Mungu ni rafiki wa ukimya. Tazama viumbe – miti, maua, nyasi vinakua katika ukimya; tazama nyota, mwezi na jua vinafanya mambo katika ukimya.. Tunahitaji ukimya kuweza kugusa nyoyo za watu,” alisema Mama Tereza wa Calcutta.
Kila mtu ajiulize anakumbukwa kwa lipi na atakumbukwa kwa lipi. Tenda wema huende zako wema hauozi. Tunasoma katika Biblia. “Habari kuhusu tukio hilo iliandikwa katika kitabu cha kumbukumbu mbele ya mfalme” (Esta 2:23). Matendo yako mazuri yataandikwa katika kitabu cha “Guiness” cha Mungu.
Kijana mwenye umri wa miaka kumi na nane alienda karibu na Ghala la Dawa na kutoa kreti ya soda aitumie kufikia kwenye sanduku la kupigia simu. Alisimama juu ya kreti ya soda na kubonyeza vitufe (buttons) za namba saba. Mmiliki wa Ghala ya Dawa alisikiliza mazungumzo: Kijana alisema, “Mama unaweza kunipa kazi ya kukata nyasi kwenye uwanja wako? Mama huyo alijibu, “Tayari nina mtu anayekata nyasi katika uwanja.” Kijana alisema, “Mama nitaka nyasi kwenye uwanja nusu ya gharama ya mtu anayekata nyasi katika uwanja wako.” Mama huyo alijibu, “Ninaridhika na kazi anayoifanya mfanyakazi wangu.” Kijana akionesha uvumilivu alisema, “Mama, nitafagia njia na vinjia katika eneo lako lote bure.”  Mama huyo alijibu kwa mkato, “Hapana, nashukuru.” Akiwa amevaa tabasamu, kijana huyo alimaliza mazungumzo. Mmiliki wa Ghala ya Dawa alisema, “Kijana nimependa mtazamo wako juu ya kazi nataka nikupe kazi.” Kijana alijibu kwa ufupi, “Hapana, nashukuru.” Mmiliki wa Ghala ya Dawa alimjibu, “Lakini ulikuwa unaomba sana upewe kazi.” Kijana alisema, “Nilikuwa nataka kujua kipimajoto cha kazi kikoje, kama mama ninayemfanyia kazi anaridhika na ananikumbuka kama mchapakazi.” Ndugu utakumbukwa kama Yozefu – Mfanyakazi? Ndugu utakumbukwa kama Bikira Maria – Mama mkimya aliyeweka yote moyoni? Ndugu utakumbukwa kama mtoto Yesu aliyekua katika umbo na hekima?


Saturday, December 13, 2014

JE UNA FURAHA?



                                               JUMAPILI YA 3 YA MAJILIO                                          

1. Isa 61: 1-2. 10-11
2.  1 Wath 5: 16 -24
3.  Yoh 1: 6-8. 19-28

Mungu wetu ni Mungu anayetaka uwe na furaha daima. Kufurahi ni wajibu. Una mawazo unayowawazia watu lakini Mungu anakuwazia mambo mazuri. Furahi kila wakati. Unafikiria watu Mungu anakufikiria. Furahi kila wakati. Tunapofanya tunaloweza, Mungu atafanya tusiloweza. Kwa namna hiyo tunaye Mungu anayeleta furaha. Furahi kila wakati. Jumapili hii katika Kanisa Katoliki inaitwa Jumapili ya Furaha. Furahi kwa kilatini “Gaudete.” Hatuna budi kufurahi sababu Yesu Kristo atazaliwa mioyoni mwetu siku ya Krismasi. Mtume Paulo anatushauri kwa msisitizo. ““Furahini kila wakati” (1 Wathesalonike 5:16). Pia mtume Paulo anasisitiza mahali pengine. “ Basi, furahini daima katika kuungana na Bwana! Nasema tena: furahini!” (Wafilipi 4:4).
 Wito ni furahi kila wakati. Katika insha moja iliandikwa kuwa mtoto anacheka mara 200 kwa siku. Mtu mzima anacheka mara 4 kwa siku. Kitabu cha mhubiri kinasema kuna wakati wa kucheka na wakati wa kulia. Kwa nini tofauti hii1. kubwa kati ya mtoto na mtu mzima? Furaha haitegemei mahali ulipo. Adamu na Eva walikuwa kwenye Bustani ya Eden, lakini baadaye hawakuwa na furaha baada ya kumkosea Mungu. Lucifer kadiri ya masimulizi ya maandiko matakatifu aliyekuwa mbinguni alimkosea Mungu na kukosa furaha. Alitumuliwa huko.  Alikuwa mbinguni hakuwa na furaha. Mtume Paulo anatualika, “Furahini kila wakati” (1 Wathesalonike 5:16). “Wanasema mtu anahitaji mambo matatu kuwa na furaha kweli katika dunia hii: nafsi  ya kupenda, kitu cha kufanya, na jambo la kutumainia,” alisema Tom Bodet.
Hakuna mtu anayependa Krismasi imkute kifungoni au jela. Taarifa ambazo huwa tunazipata toka zahanati na hospitalini ni kuwa wakati wa Krismasi wagonjwa wanapungua wadini. Hakuna ambaye anapenda Krismasi imkute wadini. Lakini ugonjwa haubishi hodi na hauna kalenda. Kipindi cha Krismasi ni kipindi cha kufurahi. Mtume Paulo anatukumbusha, “ Basi, furahini daima katika kuungana na Bwana! Nasema tena: furahini!” (Wafilipi 4:4). Krismasi inakaribia furahini. Mtume Paulo alipoandika barua kwa wafilipi mnamo mwaka 55 baada ya Kristo kuzaliwa alikuwa kifungoni. Licha ya kuwa katika matatizo alivaa vazi la furaha.
Daraja kati ya furaha na mateso sio ndefu. Wakati mwingine kuna furaha baada ya mateso. Kama tusemavyo, baada ya dhiki faraja. Kuna watu ambao wana furaha, wengine wana mateso. Baadhi ya watu wanakaa na kicheko na tabasamu utafikiri wana matangazo ya biashara ya dawa ya meno wanayotumia. Wengine wanakuwa na ndita za hasira usoni. Kuna ambao wanaambiwa usicheke uko kanisani. Kuna methali zinazobainisha ukweli huu: furaha ya mwenye meno, kibogoyo hashiriki, furaha ya kima mbwa hashiriki. Tofauti hizi zinatufanya tujiulize nini chemchemi ya furaha? Kwa wakatoliki Jumapili hii kabla ya Krismasi inaitwa Jumapili ya Furahi kwa kilatini “Gaudete.” Hatuna budi kufurahi sababu Yesu Kristo atazaliwa mioyoni mwetu siku ya Krismasi. Mtume Paulo anatushauri: “Furahini kila wakati. Salini bila kuchoka. Fanyeni shukrani katika yote” (1 Wathesalonike 5:16-18). Katika haya hii ya Biblia tunapata chemchemi ya furaha.
Kuthamini mtu na kushukuru kunaleta furaha. Unaposhukuru mtu ina maana unathamini zawadi yake naye unamthamini. Katika msingi huu unaweza kusema furaha yako ni furaha yangu. Furaha ya mwenzako iwe furaha yako. Katika msingi huu methali ya Kiswahili inasema, “Mzazi yeyote hufurahi amwonapo mtoto wake akicheka. Methali hii hutufunza kuwa mzazi yeyote humthamini mtoto. Kila mzazi hufurahi mwanawe anapoishi maisha ya furaha. Usipende pesa ukawatumia watu bali upende watu utumie pesa. Kwa maneno mengine thamini watu upate ya watu. Thamini watu upate furaha.

FURAHA IPO KATIKA KUPENDA NA KUPENDWA
Nafsi ya kwanza ya kupenda ni Mungu. Katika hili Mtakatifu Augustini alisema, “Hatutulii tutatulia katika Mungu.” Katika Mungu kuna furaha kamili. Kupendwa na Mungu ni furaha. Kumpenda Mungu ni furaha. Mungu huyu amejificha kati yetu. Yohane anasema, “katikati yenu amesimama yeye msiyemjua ninyi” (Yohane 1: 26). Katika Yesu Kristo Mungu amevaa ubinadamu wetu. Mungu wetu ni “Mungu aliyejificha.” Lakini anatufanyia makubwa nyuma ya pazia. Ni kama Mwandishi wa maisha ya mtu mwingine. Haonekani katika kitabu lakini anafanya mambo mengi. Kuna watoto ambao walikuwa wanacheza mchezo wa kujificha. Mtoto mmoja alipojificha hawakwenda kumfichua. Alipotoka kwenye maficho akakuta wanaendelea na mchezo mwingine. Mungu amajificha. Amejificha katika viumbe vyake mpaka watu tunachoka kumtafuta. Tunaambiwa “katikati yenu amesimama yeye msiyemjua ninyi” (Yohane 1: 26). Yupo kati ya wagonjwa. Yupo kati ya maskini. Yupo kati ya wageni.
Kutulia katika Mungu ni chemchemi ya furaha. Mtakatifu Augustini wa Hippo Afrika ya Kaskazini alisema, “Wewe umetufanya kwa ajili yako mwenyewe na mioyo yetu haitulii mpaka inapotulia ndani yako.” Tutakuwa na furaha kamili na ya kweli tutakapotulia katika Mungu, katika kutimiza mapenzi na amri za Mungu. Andika mipango yako kwa kalamu ya mtI Mungu mwenyewe ana mfutio. Msemo wetu uwe Bwana akipenda au msemo maarufu wa kiarabu Inshallah. Inatupasa kusema, “Bwana akipenda tutakuwa wazima bado na kufanya hiki na hiki” (Yakobo 4:15). Chemchemi ya furaha kamili haitokani na matukio yanatokea au mazingira tuliyomo. Inatoka katika Mungu anayekuwa ndani mwetu. Kutulia katika Mungu kunahitaji unyenyekevu. Kuna kijiji kimoja kilivamiwa na watu wakatili kuna mtoto wa miaka kama kumi na mawili ambaye alikuwa mlemavu wa miguu. Hivyo wazazi walipokimbia hakuwa na uwezo wa kukimbia walimwambia akae kama amekufa hivi. Hivyo aliachama. Maadui walipofika walishangaa usafi wa meno yake wakasema huyu amekufa lakini ana meno mazuri na masafi sijui anatumia dawa gani. Mtoto huyu akasema, “Natumia colgate.” Majivuno yalimuingiza hatarini wakajua hajafa. Nyenyekea ule vya Mungu na watu. Kukiri hali ya kumtegemea Mungu ni msingi wa furaha. Mungu ni nguvu yako. Mungu ni ngome yako.
Nafsi ya pili ya kupenda ni mtu mwingine au watu wengine. Kupendwa na watu ni furaha. Kupenda watu ni furaha. Ya mwisho ni nafsi yako. Kuwapenda wengine kama ambavyo unajipenda ni furaha.

FURAHA IPO KATIKA MATENDO MEMA
Furaha ipo katika kufanya kitu fulani hasa kutenda wema. “Furaha sio kitu ambacho kimetengenezwa tayari. Kinatoka katika matendo yako,” alisema Dalai Lama XIV. Matendo yanayozungumziwa ni matendo mema. Mtume Paulo anazidi kutuasa, “Kagueni yote: yaliyo mema yashikilieni. Mabaya ya kila namna yaepukeni” (1 Wathesalonike 5: 22). “Ukifanya mambo mazuri, watu watakushitaki kuwa una nia ya kujinufaisha iliyofichika, fanya mazuri vyovyote vile. Kama umefanikiwa,utajipatia marafiki ambao sio wa kweli na maadui kweli, fanikiwa vyovyote vile. Zuri utakalofanya leo litasahuliwa kesho, fanya jambo zuri vyovyote vile. Ukweli na uwazi vinaweza kukufanya udhuriwe. Kuwa mkweli na muwazi  vyovyote vile.  Watu wakubwa wa kike na kiume wenye mawazo makubwa wanaweza wanaweza kushushwa na watu wadogo wa kiume na kike wenye mawazo madogo. Fikiria makubwa vyovyote vile. Watu huwapenda watu wanaoonewa lakini huwaiga washindi tu. Pigania wanaoonewa vyovyote vile. Unachotumia  miaka mingi kujenga kinaweza kuharibiwa usiku mmoja. Jenga kwa vyovyote vile. Watu wanahitaji msaada kweli lakini wanaweza kukushambulia kama ukiwasaidia. Wasaidie vyovyote vile. Ipe dunia zuri ulilonalo utakabiliana na upinzani. Ipe dunia zuri kwa vyovyote vile,” aliandika Kent M. Keith. Katika kuwasaidia wengine kuna furaha. Kuna methali ya Kichina isemayo, “Ukitaka furaha kwa saa, lala. Ukitaka furaha kwa mchana wote, nenda kuvua. Ukitaka furaha kwa mwaka mmoja urithi mali. Ukitaka furaha kwa maisha yako yote, saidia mtu.”

FURAHA IPO KATIKA MATUMAINI
Kuwa na jambo la kutumainia kunaleta furaha. Mgonjwa akiwa kwenye chumba cha kungojea daktari wakimwambia kuwa daktari atakeyemtibu ni daktari bingwa, anakuwa na matumaini na matumaini hayo yanamletea furaha. Sasa hivi wakristu wanatumainia baraka na neema za Krismasi jambo kubwa zaidi Yesu azaliwe katika mioyo yao.  Lakini katika mateso na shida tunaweza kuwa na furaha. “Ni vigumu kusahau maumivu, lakini ni vigumu zaidi kukumbuka utamu. Hatuna makovu ya kuonesha furaha. Tunajifunza machache kutoka kwenye amani,” aliandika Chuck Palahniuk katika Diari yake.

FURAHA IPO KATIKA MAWAZO CHANYA
“Sio kile ulichonacho, au cheo ulichonacho au mahali ulipo panakufanya uwe na furaha. Ni kile unachofikiria juu yake,” aliandika Dale Carnegie. Furaha inakutwa katika kusema ndiyo ikawa ndiyo kweli na hapana ikawa hapana kweli. “Furaha ni pale unachofikiria, unachokisema na unachokitenda vinapatana kikamilifu,” alisema Mahatma Gandhi. Zaidi ya hayo furaha ni suala la mtazamo chanya.
GHARAMA YA FURAHA
Tukumbuke kuwa furaha inapatikana kwa gharama. Wanaoenda kupanda kwa machozi. Watavuna kwa kelele za shangwe. “Tunapotaka kuifikia furaha ya kweli kwa bei rahisi, tutaikuta imefungwa kama kitu cha bei rahisi,” aliandika  David Roberts katika kitabu chake, “The Grandeur and Misery of Man, 1955. Vya bei rahisi huenda visilete furaha. Ni katika msingi huu Yesu alisema anayetaka kunifuata ajitwike msalaba wake anifuate.
KUSHIRIKISHANA FURAHA
Furaha ni kamili unapowashirikisha wengine. “Furaha ndilo jambo pekee ambalo linaongezeka mara mbili unapowashirikisha wengine,” alisema Albert Schweitzer. Maneno hayo yalikwekwa namna nyingine na Ralph Ingersoll, “Njia ya kuwa na furaha ni kuwafanya wengine wawe na furaha.” “Furaha ni ya kweli tu wengine wanapoishiriki,” alisema Jon Krakauer
FURAHA IPO KATIKA FADHILA
Furaha ipo katika kuwa na fadhila. Unataka kuwa na furaha kuwa mpole. “Kwa kila dakika unayokasirika unapoteza sekunde sitini za furaha,” alisema Ralph Waldo Emerson. Unataka kuwa na furaha, kuwa na kiasi. Unataka kuwa na furaha kuwa na shukrani. Kiasi ni chemchemi ya furaha. Kiasi ni fadhila inayoratibu mvuto wa furaha. Fadhila inakuwa katikati. Furaha ni kituo cha njiani kati ya mengi sana na machache sana. Mfano unyenyekevu upo katikati ya majivuno na kujidhalilisha ambako ni kujinyenyekesha kupita kiasi. Ukarimu upo katikati ya uchoyo na kutapanya hovyo. Kutapanya hovyo ni ukarimu uliozidi mipaka. “Majonzi yanaweza yakajishughulikia yenyewe, lakini kupata thamani yote kabisa ya furaha lazima uwe na mtu wa kugawana naye,” alisema Mark Twain.

Counter

You are visitor since April'08