Saturday, October 11, 2014

YESU ANAFUTA MACHOZI





                              Jumapili ya 28 ya Mwaka A

 “Atayafuta machozi katika nyuso za watu wote na kuwaondolea watu wake aibu duniani kote” (Isaya 25:8).

“Yesu ambaye hakutoa machozi kamwe asingeweza kufuta machozi yangu,” alisema Mchungaji Charles H. Spurgeon. Yesu anafuta machozi sababu naye alitoa machozi. Yesu alimlilia Lazaro. Yesu aliilia Yerusalemu. Yesu alitokwa machozi Gethsamane. Yesu Kristu tunayemfuata ni Bwana anayefuta machozi. Unabii wa Isaya unaweka hilo wazi, “Atayafuta machozi katika nyuso za watu wote na kuwaondolea watu wake aibu duniani kote” (Isaya 25:8). Yesu alifuta machozi ya Petro. Yesu alifuta machozi ya waombolezaji. Yesu alifuta machozi ya jamaa zake Lazaro.

Mtakatifu  Ambrose alisema, “Katika Kanisa kuna maji na machozi: maji ya Ubatizo na machozi ya Kitubio.” Lakini kuna aina mbalimbali za machozi. Kuna machozi ya kusingiziwa. Kuna machozi ya kurubuniwa. Kuna machozi ya kufiwa. Kuna machozi ya mpendwa kuwa mbali. Kuna machozi ya kukataliwa. Kuna machozi ya kutopata mchumba. Kuna machozi ya kutozaa. Kuna machozi ya kupoteza. Kuna machozi ya ahadi zilizovunjwa. Kuna machozi ya kusemwa. Kuna machozi kukata tamaa. Kuna machozi ya mateke ya shukrani ya Punda. Kuna methali isemayo; “Ninaotibu vidole ni ndio wanaoiba viazi vyangu.” Nyingine inasema: Nyuki anashukuriwa kwa kuchomwa moto. “Machozi ni maneno ambayo moyo huwezi kueleza,” alisema Loretta Lynn. Mtu akishindwa kueleza huzuni kwa maneno anaueleza kwa machozi. “Machozi ni lugha ya kimya ya huzuni,” alisema Voltaire. Lakini Yesu anafuta machozi.


Kuna hadithi juu ya Malaika aliyetumwa na Mungu kwenda duniani na kurudi na kitu cha thamani kubwa. Aliruka kwenda chini duniani na kutafuta toka ncha moja hadi ncha nyingine. Aliokota kipande cha dhahabu lakini aliona hakina uzuri wa kutosha kwa ajili ya Mfalme. Aliona lulu isiyo na doa bado aliona haina uzuri wa kutosha kwa ajili ya Mfalme. Malaika aliendelea kutafuta kila mahali. Hatimaye alisijia mtu aliyetoa mguno wa kulia. Alikuwa ni mtu ambaye alikuwa amepiga magoti anasali, akibwaga moyo wake kwa Mungu akiomba msaada na msamaha. Malaika alijiambia, “Ee, ndiyo kitu chenyewe.” Malaika alimshika mkono mtu huyo na kuweza kudaka chozi moja kati yam atone ya machozi yaliyokuwa yanabubujika. Alienda mbinguni kwa moyo wa ushindi na kumkabidhi Mungu chozi akimwambia: “Chozi ni jambo la thamani sana duniani.” Tumeona watu wengi wakibubujikwa machozi labda tunafikiri ni kitu cha kawaida. Machozi ni lugha Mungu anayoelewa. Machozi yako yamerokodiwa. Kumbukumbu ya machozi yako zimetunzwa.

Kuna watu ambao wamekuwa na mvua za machozi. Hasira inaweza kugeuka machozi. Huzuni unaweza kugeuka machozi. Kuna ambao wana machozi lakini wanayaficha. “Nilimdanganya kila mtu kwa tabasamu langu kubwa kwa miaka na miaka. Sikumwonesha mtu yeyote machozi yangu,” alisema Francine Chiar.

Namna gani atafuta machozi? Ataondoa kifuniko cha uchungu kwenye macho ya akili. “Ataliondoa wingu la huzuni lililowafunika watu wote, kifuniko cha uchungu juu ya mataifa yote” (Isaya 25: 7). Yesu ataondoa pazia kwenye macho ya akili. Ingawa tunasema macho hayana pazia, macho ya akili yanaweza kuwa na pazia. Kuna vitu ambavyo labda hauelewi. Tunasema, “La kuvunda halina ubani.” Yesu anaondoa kifuniko kwenye macho yetu ya akili. La kuvunda lina ubani. Alimfufua Lazaro. Unasema, “Kwa nini mimi Mungu?” Yesu anaondoa kifuniko kwenye macho yako ya akili. Katika maisha yake utagundua kuwa “Hakuna Jumapili ya Paska” bila “Ijumaa Kuu.”Namna hiyo anafuta machozi.

 Kama umepoteza jamaa yako Yesu atafuta machozi. Namna gani? Tajiri mmoja mwenye pesa kama serikali alikuwa na shamba kubwa na zuri la maua. Alilikabidhi kwa mtu mwingine alitunze aliyependa maua na alifahamu aina mbalimbali za maua. Ilikuwa ni furaha ya mtu huyu kumwagilia miche ya maua wakati wa ukame, kuweka fito za kutumika kama mihimili ya mashina laini, kukinga mimea dhidi ya upepo na baridi na dhidi ya wadudu na wanyama wahaaribifu. Asubuhi moja mtunza bustani aliamka na shauku isiyokuwa ya kawaida. Baadhi ya maua yake mazuri yalikuwa yamekaribia kutoa maua. Alitegemea kuwa yatakuwa katika hali nzuri yakiwa kamili. Kwa mshangao unaohumiza aligundua kuwa moja ya maua yake mazuri limechumwa kutoka kwenye shina lake. Akijaa hasira na masikitiko aliwaendea wafanyakazi wengine kwenye shamba, akitaka kujua aliyemwibia hazina yake. Aliwapitia mmoja baada ya mwingine kila mmoja akisema kuwa hana hatia, na aliwaamini. Hata hivyo moyo wake ulikuwa na masikitiko kwa kupoteza au lake zuri. Hatimaye mmoja wa wahudumu alimpa angalisho: “Nilimuona Bwana wa Shamba akitembea asubuhi hii katika bustani ya maua. Nilimuona  akichuma ua na kulibandika kwa pini kwenye koti lake. Mtunza bustani ya maua alipata liwazo kusikia kuwa Bwana wa Shamba ndiye amechuma ua. Alifurahi kusikia kuwa Bwana amependezwa na hilo ua. Alitabasamu kisirisiri kwa kulipoteza akijua kuwa limempendeza Bwana. Waliotutoka ni maua yaliyompendeza Bwana. Tunasoma katika kitabu cha ufunuo, “Andika! Heri watu ambao tangu sasa wanakufa wakiwa wameungana na Bwana. Naye Roho asema ‘Naam! Watapumzika kutoka taabu zao; maana matunda ya jasho lao yatawafuata” (Ufunuo 14: 13).

Kulia na kutoa machozi kunategemea unatazamaje mambo? Kuna mtoto ambaye alipoteza shilingi mia moja. Mzee mmoja alimkuta akilia barabarani. Alimuuliza, “Kwa nini unalia?” Mtoto huyo alisema, “Nimepoteza shilingi mia moja.” Mzee huyo akatoa shilingi mia moja na kumpa. Jambo la kushangaza mtoto aliendelea kulia sana na kupiga moyowe. Mzee akashangaa na kumuuliza, “Mbona baada ya kukupa shilingi mia moja umelia sana.” Mtoto akasema, “Sasa hivi ningekuwa nimefikisha shilingi mia mbili.” Mtoto huyu alikuwa na shida ya uchoyo. Penye kilio sababu ya uchoyo Yesu anafuta machozi akipendekeza kutupilia mbali uchoyo na kugawana. Alisema nilikuwa na kiu ukanipa maji ya kunywa, nilikuwa na njaa, ukanilisha. 

Machozi ya toba
Mtakatifu  Ambrose alisema, “Katika Kanisa kuna maji na machozi: maji ya Ubatizo na machozi ya Kitubio.” Kutubu ni kudondosha machozi ya toba. Mtakatifu Petro alipotubu alitokwa na mchozi ya toba (Luka 22: 61). Katika Injili ya Marko tunaambiwa, “Tubuni na kuiamini Habari Njema” (Marko 1: 15). Kutubu ni kubadili mwelekeo na uelekeo, njia na dira, msimamo na mtazamo. Kubadili mwelekeo kunaendana na maumivu kiasi cha kutoa machozi ya toba. Kutubu ni kuikimbia dhambi. Nilimuuliza Mkristu mmoja baada ya kuungama dhambi, “Sasa unajionaje?” Aliniambia, “Padre kabla ya kuungama dhambi nilikuwa mdhambi anayeikimbilia dhambi, sasa ninaikimbia dhambi.” Kutubu ni kuikimbia dhambi na kumkimbilia Yesu Kristo. Tunaambiwa, “Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia” (Marko 1: 15). Yesu ni ufalme wa Mungu wenyewe. Yuko karibu kama mdomo na pua.


 Tulie na Wanaolia
“Wale ambao hawajateseka hawajui mateso ya wengine,” ndivyo isemavyo methali ya Haiti. Kuna watu wanaoteseka wanahitaji kuwafariji. Wakimbizi wanateseka wanahitaji kuliliwa. Wasio na makazi wanateseka wanahitaji wa kuwalilia. Kwa kawaida jicho moja likiingiwa na mchanga linajililia lenyewe jicho la pili halilii. Binadamu hatuna budi  kuwa kinyume na jicho hili. Hatuwezi kusema kila jicho lijililie lenyewe. Ndio maana mtume Paulo anatuasa, “Lieni pamoja nao waliao.” (Warumi 12:15) Yesu mwenyewe alilia na waliomlilia Lazarus. “Basi Yesu alipomwona analia, na wale wayahudi waliofutana naye wanalia, aliugua rohoni, akafadhaika roho yake, akasema, “Mmemweka wapi? Wakamwambia, ‘Bwana, njoo utazame.’ Yesu akalia machozi.” (Yohane 11: 33-35) Yesu hakulia tu machozi alitoa msaada.

Kuna watu ambao wanabeba misalaba ya chuma ambayo siyo ya kujitakia yaani mateso makubwa maishani. Kuna ambao wanabeba misalaba ya kijitakia mfano kuna kijana wa miaka thelathini aliyemua baba yake na mama yake. Baada ya kutolewa hukumu aliulizwa kujitetea. Akasema naomba mnipunguzie miaka maana mimi ni mwana yatima sina baba sina mama. Huu ni msalaba wa kujitakia sio kwa sababu ya Yesu.

Kuna watu ambao wanapata mateso juu ya mateso tulie nao. Yaani tuwafariji na kuwasaidia. Kuna ambao wanakwepa mvua lakini wanaagukia mtoni. Tufarijianeni. Watu wengi wana matatizo. Watu wasio na matitizo ni wale waliozikwa makaburini. Kulia na wanaolia ina maana ya kujiweka katika nafasi ya wenye matatizo, kuingia katika viatu vyao  na kufikiria kama ingekuwa wewe. Licha ya hayo machozi yana nguvu. Kulia na wanaolia ni namna ya kuwafariji wanaolia. Kuna ambao wanabeba misalaba ya kutukanwa na kudharauliwa. “Vidonda vya maneno ni vibaya sana kuliko vidonda vya upanga.” Methali ya Kiarabu Tusiwadharau watu na kuwatukana kwa vile wanatoka kabila fulani au eneo fulani. Badala ya kuwatukana tuwasaidie.

Katika maisha ya kawaida ya kila siku mtoto wakati mwingine huwasiliana kwa kulia. Machozi yana nguvu. Mtoto anayelia huwafanya wazazi wajiulize kuna jambo gani? Penye shida mtoto husaidiwa. Hiyo ni nguvu ya machozi. Mzee Mwambarikutu aliulizwa, “Nguvu gani katika dunia hii ilikufanya umrudie mke wako wakati watu wote walijua mke wako alikuwa amekukosea,” Alijibu, “Nguvu ya machozi – sikuweza kuvumilia kulia kwake.” Machozi yana nguvu. Hata maji yakimwagika yanaweza kuzoeleka kama kuna wanaokulilia yaani wanaokuonea huruma na kutafuta suluhisho. Ili maji yazoeleke lazima pawepo na “Kulia na wanaolia.” Lazima watu wakulilie yaani wakuonee huruma na kukusaidia ambapo hauwezi kujisaidia mwenyewe.


Unahitaji washauri na wafariji wenye nguvu na sio duni. Ayubu aliwaambia marafiki zake wafariji duni “Mambo kama hayo nimeyasikia mengi: nyinyi ni wafariji duni kabisa!” (Ayubu: 16:2.) Mfalme Daudi katika Biblia alikumbana na washauri duni na wafariji duni: “Wanitembeleapo husema maneno matupu; wanakusanya mabaya juu yangu, na wafikapo nje huwatangazia wengine. Wote wanichukiao hunong’onezana juu yangu; wananiwazia mabaya ya kunidhuru. Husema: “Maradhi haya yatamuua; hatatoka tena kitandani mwake!” Hata rafiki yangu wa moyo niliyemwamini, rafiki ambaye alishiriki chakula changu, amegeuka kunishambulia!” (Zaburi 41: 6 -9)

Fariji kwa Kutumia Tiba ya Kuongea
Kuongea ni tiba. Kama una sononokeko na simanzi kuongea ni tiba. Kama una mfadhaiko kuongea ni tiba. Muulize mtu maswali ambayo hayambani mtu kutoa jibu la ndoa au hapana bali kuelezea. Kuna mitume wawili waliokuwa wanaenda Emmaus walikuwa wamekata tamaa. Yesu aliwauliza maswali mawili yanayohitaji majibu marefu ili waongee. Swali la Kwanza: “Mnazungumza nini huku mnatembea?” (Lk 24: 17). Swali la Pili: “Mambo gani?” (Lk 24: 19) Mitume hawa walikuwa wenye huzuni. Yesu aliwatia moyo waongee. Kuongea ni tiba na kutia mtu moyo aongee kunahitaji ufundi katika kuuliza maswali. Yesu alifuta machozi ya wafuasi wa Emmaus atafuta ya kwako.

Mfariji mwenye nguvu anayekulilia, atakukumbuka, akiwa na uwezo atakusaidia.  “Kristu alilia: binadamu ajililie mwenyewe. Kwa nini Kristu alilia, alitaka kuwafundisha watu kulia,” alisema Augustini wa Hippo aliyeishi karne ya tano huko Afrika ya Kaskazini.  Nasi hatuna budi kulia. Tulie kwa sababu ya makosa yetu. Hapa tutoe machozi ya toba kama Simon Petro.  “Bwana akageuka na kumtazama Petro, naye Petro akakumbuka yale aliyokuwa ameambiwa na Bwana: “Leo kabla jogoo hajawika, utanikana mara tatu.” Hapo akatoka nje, akalia sana.” (Luka 22: 61-62) Petro alijutia mabaya aliyomtendea Yesu kwa kumkana. Alitoa machozi ya toba. Tujutie mabaya tuliowatendea wengine kwa kutoa machozi ya toba. Toba ni majuto kwa kutenda maovu.


WASIFU WA MACHOZI
  1. Machozi ni kiona mbali: “Machozi mara nyingi ni kiona mbali ambacho kwacho watu huona mbali mbinguni,” alisema Henry Beecher.
  2. Machozi ni Lugha ya huzuni: “Machozi ni maneno ambayo moyo huwezi kueleza,” alisema Loretta Lynn.
  3. Ni sabuni ya maono: “Labda macho yetu yanahitaji kuoshwa na machozi mara moja moja ili tuyaone maisha kwa muono unaonekana vizuri zaidi,” alisema Alex Tan.
  4. Ni nyenzo ya makuzi na kusafisha: “Wakati mwingine lazima tuhumie ili tuweze kukua, lazima tushindwe ili kujua, wakati mwingine maono yetu yanaonekana baada tu ya macho yetu kusafishwa na machozi,” alisema Aaron Chan.

Counter

You are visitor since April'08