Friday, July 29, 2016

HATUTULII TUTATULIA KATIKA MUNGU



            HATUTULII TUTATULIA KATIKA MUNGU
                
                                Jumapili ya 18 ya Mwaka C
                
1. Mhubiri  1:2; 2:21-23
Wokolosai 3:1-5, 9-11
Luka 12:13-21

UTANGULIZI
“Ee Bwana umetuumba kwa ajili yako hatutulii mpaka tutakapotulia katika wewe,” alisema Mtakatifu Augustini wa Hippo Afrika ya Kaskazini. Katika mali hatutulii tutatulia katika Mungu. Katika mapenzi hatutulii tutatulia katika Mungu.Katika mamlaka hatutulii tutatulia katika Mungu. Kuna anayesema nikipata gari nitakuwa nafuraha. Je ni kutokuwa na gari kunakuzuia usiwe na furaha.Kuna anayesema nikipanda cheo nitakuwa na furaha. Je, nikutopanda cheo kunakuzuia kutokuwa na furaha? Ni katika msingi huo Mhubiri anasema Ubatili. Mali bila Mungu ni ubatili. Mamlaka bila Mungu ni ubatili. Mapenzi bila Mungu ni ubatili. Furaha kamili tutaipata katika Mungu.


KATIKA MALI HATUTULII
Kuna mtoto wa miaka saba alikuwa akitafuta michango ya kusaidia watoto wenye shida. Alipofika benki moja huko Tanzania. Meneja wa benki alimwambia kuwa ana sarafu ya shilingi mia mbili na noti ya shilingi mia tano. Achague kati ya sarafu ya mia mbili na noti ya shilingi mia tano. Mtoto huyo alimwambia meneja. “Nitachukua sarafu ya mia mbili lakini hili isipotee, nitaikunja kwenye noti hiyo ya shilingi mia tano.” Mtoto huyo alitaka kuchukua pesa yote. Hatutulii katika pesa. Katika Injili ya Luka 12: 16-20 tunapewa mfano wa mtu aliyemiliki mali lakini mali ilimmiliki. Alikuwa tajiri. Tumpe jina la Dives jina la kilatini maana yake  tajiri. Dives hakufikiria katika msingi wa methali isemayo, “Hakuna mifuko katika sanda.” Hakufikiria katika msingi wa msemo husemao, “sisi ni marehemu watarajiwa.” Mungu alimuita “mpumbavu.” Mpumbavu ni mtu mjinga, jua na zuzu. Biblia ina picha nyingi za mtu mpumbavu: “haifai kwa mpumbavu kuishi kwa anasa” (Methali 19: 10). Tajiri Dives aliishi kwa anasa. “Mpumbavu hudharau mafundisho ya baba yake” (Methali 15: 5). Tajiri Dives alidharau mafundisho ya Mungu Baba yake-Mpende Mungu kwa moyo wako wote, kwa akili zako zote na kwa nguvu zako zote. Hakumpa Mungu kipaumbele. “Mtoto mpumbavu ni huzuni kwa baba yake” (Methali 17: 25). Tajiri Dives alikuwa huzuni kwa Mungu –Baba yake.


Masimulizi hayo ni kama ifuatavyo, “Kulikuwa na tajiri mmoja ambaye shamba lake lilizaa mavuno mengi. Tajiri huyo akafikiri moyoni mwake: ‘Nitafanyaje nami sina mahali pa kuhifadhia mavuno yangu? Nitafanya hivi: nitabomoa ghala zangu na kujenga kubwa zaidi, nami nitahifadhi humo mavuno yangu yote na mali yangu. Hapo nitaweza kuiambia roho yangu: sasa unayo akiba ya matumizi kwa miaka na miaka. Ponda mali, kula, kunywa na kufurahi.” Lakini Mungu akamwambia: ‘Mpumbavu wewe; leo usiku roho yako itachukuliwa. Na vitu vile vyote ulivyojirundikia vitakuwa vya nani?” (Luka 12: 16-20).

Dives alipopata mavuno mengi alikuwa tayari tajiri kama serikali au mwenye pesa kama njugu. Hakuangalia uwezekano mwingine wa kutumia mali yake kama kuendeleza kazi ya Mungu, kusaidia maskini, kuacha zawadi ya watunzi, wateteaji amani. Alifikiria tumbo lake, usingizi wake, anasa zake. Hakumpa Mungu nafasi. Hakumpa jirani nafasi.


Tajiri Dives hakutulia katika mali. Hakumkaribisha Mungu katika maisha yake. Ni katika msingi huo Mhubiri anasema Ubatili. Mali bila Mungu ni ubatili. Mamlaka bila Mungu ni ubatili. Tayari alikuwa tajiri mkubwa sana alipopata mavuno yakutosha. Ebu tuchambue binadamu hasivyotulia katika mali. Mtu akijenga nyumba anajenga na ukuta lakini hatulii. Anaweka vipande vya chupa juu ya ukuta, lakini hatulii. Anaweka nyaya za umeme, lakini hatulii. Anajenga nyumba ndogo ya mlinzi, lakini hatulii. Anaweka kibao chenye maneno yasemayo, “Kuna Mbwa Mkali,” lakini hatulii hata kama mbwa huyo hana meno. Anaweka kibao chenye maneno, “Nyumba hii Inalindwa na Mitambo Maalum.” Lakini hatulii. Anaweka Kamera za kupiga picha lakini hatulii. Mtu mwingine ambaye ana imani katika uchawi anaweka mkia wa mjusi kama kusema, “Nyumba hii inalindwa na mkia wa mjusi.” Ni vizuri kuwa na ulinzi imara bila kuamini katika uchawi, lakini usimsahau Mungu. Mtunga Zaburi anatwaambia, “Mwenyezi-Mungu asipoijenga nyumba,waijengao wanajisumbua bure. Mwenyezi-Mungu asipoulinda mji, waulindao wanakesha bure” (Zaburi 127: 1). 


Tajiri Dives angefikiria kukiachia kizazi kijacho urithi. Lakini hakufanya hivyo. Kilikuwa ni kipindi cha masika yatokanayo na pepo za Monsuni katika Bahari ya Hindi, na mzee aliyekuwa amekula chumvi alikuwa akilima mashimo katika bustani yake. “ Unafanya nini ?” Jirani yake alimuuliza. “Ninapanda miti ya miembe” lilikuwa jibu. “ Unategemea utakula maembe toka katika miembe hiyo ?”“Hapana, sitaishi muda mrefu kwa ajili ya hilo. Lakini wengine watakula. Lakini maisha yangu yote nimekula maembe ambayo yamepandwa na watu wengine. Hii ndiyo njia ya kuonesha shukrani”.


Katika pesa hatutulii. Kuna mtu alienda kwa padre kumwomba padre afanye ibada ya kuzimzika mbwa wake. Padre akasema huwa tunafanya ibada kuzika binadamu na wala sio mbwa. Yule mtu akaondoka akiwa amehuzunika. Baada ya kutembea hatua kadhaa mbele aligeuka nyuma akamwambia huyo padre kama ungefanya ibada ya kumzika mbwa wangu ningekupa $ 1000. Padre huyo akasema, “Kwa nini ukuniambia kuwa mbwa wako ni mkatoliki ningemzika haraka.” Pesa ilimpofusha macho huyo padre hasijue mambo ya kiroho yanayohusu binadamu na wala sio mbwa.



KATIKA MAMLAKA HATUTULII
Napoleoni aliwahi kusema, “Nimejaribu kuvuta watu kwangu kwa kutumia mabavu lakini Yesu amewavuta kwake kwa kutumia upendo.” Watu walikuwa wakimshangilia Kaisari na kusema, “muungu, muungu, muungu.” Upandeni alikaa mtu aliyekuwa akimwambia, “Kumbuka wewe ni binadamu.” Tunapotafuta mamlaka tukumbuke sisi ni binadamu. Hatutulii katika mamlaka tutatulia katika Mungu.

Kuna hadithi juu ya mahali ilipofichwa furaha. Mungu alitaka kuficha furaha. Alijiambia, nikiificha nchi za kigeni watu watafika huko. Nikiificha kenye mamlaka watu watafuta mamlaka wayapate, nikiificha kwenye uzuri watu watajipodoa, nikiificha kwenye biashara watu watafanya biashara waipate, nikiificha kwenye mapenzi watu watafanya mapenzi waipate. Mungu akaificha ndani mwetu. Nenda katika moyo wako. Tunasafiri kwenda Ulaya lakini kuna mabao hawataki kusafiri kwenda katika mioyo kuona kuna nini? Kuna sauti ya Mungu katika moyo wako inayokwaambia kutenda mazuri na kuacha mabaya isikilize nawe utakuwa na furaha. Furaka kamili ni katika Mungu.



HATUTULII KATIKA MAISHA SISI NI MAREHEMU WATARAJIWA
“Utufundishe ufupi wa maisha yetu ili tuweze kuwa na hekima” (Zaburi 90:12). Tajiri anayezungumziwa katika Injili ya leo hakufikiria ufupi wa maisha yake. Vinginevyo angekuwa na hekima akumuacha Mungu aitwe Mungu na kumpa nafasi ya kwanza katika maisha yake. Hadithi inapokuwa tamu au nzuri katika gazeti hukatizwa na chini yake maneno “Itaendelea Toleo Lijalo” huandikwa. “Toleo Lijalo” kwa marehemu ni mbinguni au toharani au motoni. Tajiri aliyekuwa anapanga kufurahia mavuno yake aliambiwa ‘Mpumbavu wewe; leo usiku roho yako itachukuliwa.” Tajiri huyo hakujua kuwa alikuwa marehemu mtarajiwa. Tunasoma hivi katika kitabu cha Ayubu, “Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu. Yeye huchanua kama vile ua, kisha hukatwa” (Ayubu 14: 1-2). Kuna kijana aliulizwa, “Baada ya kidato cha nne, nini kitafuata?” Alijibu, “Nitaendelea na masomo kidato cha tano na sita.” “Halafu?” “Nitajiunga na Chuo Kikuu.” Alijibu. “Halafu?” “Nitatafuta ajira?” Alijibu. “Halafu?” “Nitaanza kufanya kazi kwa juhudi na maarifa.” Alijibu. “Halafu?” “Nitachumbia.” Alijibu. “Halafu?” “Nitafunga ndoa.” Alijibu. “Halafu?””Nitapata watoto.” Alijibu. “Halafu?” “Nitawapa elimu nzuri.” Alijibu. “Halafu?” “Nitastaafu.” Alijibu. “Halafu?” “Nitaanza kula pensheni.” Alijibu. “Halafu?” “Nitazeeka.” Alijibu. “Halafu?” “Halafu halafu…Mungu ataniita.” Alijibu kwa huzuni na kusitasita. “Ni mwanaume gani atakayeishi asione mauti?” (Zaburi 89:48). Niliwahi kuona maneno kwenye kaburi yameandikwa “Jinsi ulivyo ndivyo nilivyokuwa. Jinsi nilivyo ndivyo utakavyokuwa.” Kama ni hivyo tujitahidi kutulia katika Bwana.

Counter

You are visitor since April'08