Saturday, April 22, 2017

JE VIDONDA VYAKO NI VIDONDA VYA HURUMA?


  JUMAPILI YA HURUMA YA MUNGU (JUMAPILI YA 2 YA PASAKA)

“Tia kidole chako humu, tazama mikono yangu, lete mkono wako na kuutia katika ubavu wangu na usikose imani” (Yohane 20: 27)

“Bwana anatuonesha kupitia Injili, vidonda vyake. Ni vidonda vya huruma. Ni kweli; vidonda vya Yesu ni vidonda vya huruma,” alisema Papa Francis katika mahubiri yake Jumapili ya Huruma ya Mungu mwaka 2015. Yesu alipofuka vidonda vitano vilikuwa ni utambulisho wake. Yesu aliwaonesha mitume wake mikono yake na ubavu wake, walitambua kuwa ni yeye. “Yesu anatualika kutazama vidonda hivi, kuvigusa kama Thomasi alivyofanya, kuponya kutoamini kwetu. Licha ya hayo yote, anatualika kuingia kwenye fumbo la vidonda hivi, ambalo ni fumbo la upendo wake wa huruma,” alisema Papa Francis. Vidonda hivi vilibaki kama makovu si kumbukumbu ya ukatili kumbukumbu ya ukombozi. Yesu ametukomboa kwa huzuni na mateso. Utabiri wa nabii Isaya unasema ukweli wote, “Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, alichubuliwa kwa maovu yetu…na kwa kupigwa kwake sisi tumepona” (Isaya 53:5). Yesu alibaki na makovu yake kama alama ya ushindi na utukufu. “Nikaona Mwanakondoo amesimama kati ya kiti cha enzi na wenye uhai wanne waliozungukwa na wazee. Alionekana kama amechinjwa” (Ufunuo 5:6). Kuonekana kama amechinjwa kunabainisha makovu yake makubwa matano. Tukiyatazama kwa miwani chanya ni makovu ya kushinda vita dhidi ya uovu. Tukiyatazama kwa miwani hasi ni makovu ya ukatili.

Wachimba migodi wana vidonda vya kubeba mizigo wana “taji la miiba”  na makuli na wabebaji mizigo. Wawindaji wana vidonda miguuni, vidonda vya huruma, wakitafuta riziki ya familia. Fundi seremala wana vidonda vya kuchomwa na misumari. Wakati wa kuandikisha watu kwenye daftari la kudumu la wapiga kura iligundulika kuwa katika jamii za wakulima na wapiga kokoto alama za vidoleni zilishatoweka sababu ya matendo ya huruma kutafuta riziki kwa ajili ya wanafamilia. Kuna makovu ya huruma kwenye viganja.  Mafundi wa magari vidole vyao vina makovu ya huruma wakitafuta riziki za wanafamilia. Wakati wa kuandikisha wapiga kura kwenye daftari ya kudumu, iligundulika tulivyosikia kwenye vyombo vya habari kuwa watu wengine alama za vidoleni zilikwishafutika sababu ya shughuli za kilimo. Hayo ni makovu ya huruma kwa nafsi zao na huruma kwa wanafamilia wakiwatafutia lishe bora. Kuna watawa na mapadre ambao wana makovu kwenye magoti sababu ya tendo la huruma la kuwaombea wazima na wafu.

Mama aliyejifungua kwa njia ya operesheni ana makovu ya huruma. Ni huruma kwake na ni huruma kwa mtoto. Siku moja kuna mtoto wa miaka kumi na miwili aliyekuwa anaogelea mtoni. Mamba akashika miguu yake kwa meno. Mama yake aliyekuwa karibu akashikilia mikono kwa nguvu zake zote, hata kucha zikatoboa mikono ya mtoto. Bahati nzuri palikuwepo na mwindaji karibu. Alimpiga huyo mamba risasi, mamba alimwachia mtoto. Mtoto alipokuwa anauguza majeraha aliyasifia majeraha aliyokuwa nayo mikononi ni majeraha aliyopata sababu ya huruma ya mama, aliyemshikilia mpaka kucha za mama zikatoboa sehemu za mikono yake.

Kuna vidonda ambavyo si vya huruma: kuchubuka kwa sababu ya ulevi, kuchubuka kwa sababu ya hasira. Siku moja huko Afrika ya Kusini Gandhiji alikuwa anasafiri kwenye treini daraja la kwanza kinyume cha sheria. Polisi mzungu alitaka kumwondoa toka daraja la kwanza Gandhiji. Lakini Gandhiji aliona si haki alikataa. Mambo yalipofikia hatua hii polisi alikasirika na kumpiga kwa teke. Akijizuia kumtukana Gandhiji alijibu: “Ndugu, umehumiza mguu wako?” Polisi aliposikia swali hilo aliona aibu. Kama mguu wa polisi ulihumia kwa kumpiga teke Gandhiji, hicho hakikuwa kidonda cha huruma.

 

Bwana wetu Yesu Kristo alipofufuka alikuwa na makovu ya vidonda vya mwilini bila shaka alikuwa na makovu ya vidonda vya moyoni. Tunajifunza kwake mtazamo chanya. Alifufuka na makovu kama ishara ya ushindi na si ishara ya ukatili. Huo ni mtazamo chanya. Kuwa na mtazamo chanya ni tiba ya vidonda vya moyoni.                

MILANGO ILIYOFUNGWA NI BARAKA YA HURUMA KATIKA SURA YA BALAA

                JUMAPILI YA HURUMA YA MUNGU (JUMAPILI YA 2 YA PASAKA)

“(Yesu), akasimama katikati, ingawa milango ya chumba walimokaa wafuasi ilikuwa imefungwa kwa kuwaogopa wayahudi” (Yohane 20: 19). 

 “Mungu anapokupa mwanzo mpya, unaanza na mwisho. Mshukuru kwa milango iliyofungwa. Mara nyingi  inatuelekeza kwenye milango sahihi!” alisema mwanamke wa imani. Mlango wa ualimu wa Baba wa Taifa Julius Kambarage Nyerere ulipofungwa ukamwelekeza kwenye mlango wa urais. Naye Joyce Meyer alikuwa na haya ya kusema, “Usimwombe Mungu tu kufungua milango, lakini pia muombe Mungu kufunga milango ambayo inahitaji kufungwa.” Mlango wa ualimu kwa Baba wa Taifa ulihitaji kufungwa. “Leo funga baadhi ya milango. Si kwa sababu ya majivuno, kutokuwa na uwezo, au ubabe, lakini ni kwa sababu tu haikupeleki popote,” alisema Paul Coelho. 

Kwa mtu anayeomba kazi mlango uliofungwa ni ishara ya kukataliwa au kucheleweshwa lakini inaweza kuwa baraka katika sura ya balaa. Kwa milango iliyofungwa kwa sababu ya woga inaweza kuwa baraka katika sura ya balaa. Yesu alipouawa Ijumaa Kuu wafuasi wake baadaye waliingia chumbani na kufunga milango ya chumba. Milango iliyofungwa iliwawezesha mitume kufaidi tendo la huruma la kufundisha wajinga.

Tunasoma katika Injili ya Yohane. “(Yesu), akasimama katikati, ingawa milango ya chumba walimokaa wafuasi ilikuwa imefungwa kwa kuwaogopa wayahudi” (Yohane 20: 19).  “Yesu alingoja mpaka wote wamekusanyika: na milango imefungwa, ili kuonesha kuwa namna alivyoingia kwenye chumba ndivyo alivyoweza kufufuka jiwe likiwa juu ya kaburi,” alisema Baba wa Kanisa Theophilo. Milango iliyofungwa ilisaidia kama nyenzo za kufundishia somo la ufufuko. Yesu alifufuka wakati jiwe liko juu. Liliviringishwa na malaika sio kwa sababu Yesu apite bali mitume na wanawake wafuasi wa Yesu waweze kushuhudia kuwa amefufuka.

Milango iliyofungwa ilimtenga Thomasi, hakuwa na mitume. Aliporudi na kuambiwa kuwa Bwana Yesu amewatokea hakuamini. “Kutoamini kwa Thomasi (Yoh 11:6; 14:5; 20:24.26-29; 21:2) kumeleta faida zaidi kwenye imani yetu kuliko imani ya wafuasi wengine. Anavyomshika Kristo na kusadikishwa, kila mashaka yanaondolewa na imani yetu inaimarishwa. Hivyo mfuasi aliyekuwa akitia mashaka, aligusa madonda ya Yesu na kugeuka kuwa shahidi wa ukweli wa ufufuko” (Mt Gregori Mkuu). Tukumbuke kuwa kufundisha ni tendo la huruma, na ni baraka. Ni kweli milango iliyofungwa ni baraka ya huruma katika sura ya balaa.

Tendo la Yesu kuingia kwenye chumba wakati milango imefungwa ni somo juu ya ubikira wa Bikira Maria, baada ya kumzaa Yesu Kristo, alibaki bikira. “Milango iliyofungwa haikuzuia mwili ambapo umungu ulikaa. Aliweza kuingia bila milango kuwa wazi, ambaye alizaliwa bila kuharibu ubikira wa mama yake,” alisema Mt. Augustini. Tukumbuke kuwa kufundisha ni tendo la huruma, na ni baraka. Ni kweli milango iliyofungwa ni baraka ya huruma katika sura ya balaa.

 

“Mlango mmoja unapofungwa mwingine unafunguliwa; lakini mara nyingi tunatazama kwa kujutia mlango uliofungwa na hatuoni mlango ambao umefunguliwa kwa ajili yetu,” alisema Alexander Graham Bell. Mwanzoni mtume Thomasi aliutazama sana mlango uliofungwa wa Yesu wa Ijumaa Kuu na kuchelewa kuuona mlango uliokuwa wazi wa Yesu Kristo wa Pasaka.

Soichiro Honda wakati alipoomba kupewa kazi katika Kampuni ya Toyota Motors, baada ya kusailiwa hakupewa kazi. Mlango ulikuwa umefungwa. Lakini alitazama mlango uliofunguliwa. Tatizo la kukosa kazi katika kampuni hiyo lilikuwa ni alama ya mkato na si nukta. Alianzisha kampuni yake mwenyewe na kuanza kutengeneza baisikeli zenye injini ndogo. Leo hii Honda ni kampuni kubwa ya kutengeneza pikipiki na magari. Soichiro Honda alisema: “Mafanikio yanawakilisha asilimia moja ya kazi yako ambayo inatokana na asilimia tisini na tisa zinazoitwa kushindwa.” Kifaranga kwenye yai kinapopambana na ukuta wa yai uliokizunguka kitoke ukikionea huruma ukakisaidia kutoka unakinyima nafasi adimu ya kujiimarisha.

Mlango uliofungwa ni baraka ya huruma katika sura ya balaa.  Lakini Yesu hauzuiliwi na milango iliyofungwa. Kuna methali ya Tanzania isemayo, “Baraka ni baridi hata uwe umefunga mlango inaingia.” Yesu naye anaingia kwenye milango iliyofungwa. Mlango wa kupata kazi kama umefungwa Yesu anaweza kukusaidia kuingia. Mlango wa kupata mchumba kama umefungwa Yesu anaweza kukusaidia kuingia. “Naamini , ukiendelea kuamini, ukiendelea kutumaini, ukiendelea kuwa na mtazamo sahihi, na kama una shukrani, utamuona Mungu anafungua milango mipya,” alisema Mchungaji Joel Osteen.

 

Counter

You are visitor since April'08