Saturday, July 15, 2017

MAMBO YOTE HAYAHUSU UDONGO, BALI YANAMHUSU MPANDAJI PIA


2017 Julai 16 Jumapili ya 15

“Mpanzi alikweda kupanda mbegu” (mathayo 13:3)
Alexander Maclaren aliandika: “Mfano wa mpanzi, ni wa kihistoria na wa kinabii. Unaeleza uzoefu halisi wa Kristo, na unabashiri juu ya watumishi wake.” Mafanikio au kushindwa, uzuri au ubaya, mpanzi Yesu Kristo au Mungu wetu, usikate tamaa. Yesu akiwa amejaa neema  anaonesha jitihada za kusonga mbele kila mara, bila kuwa na mawazo ya kukata tamaa. Changamoto kwetu, tunapaswa kuwa kama Baba yetu wa mbinguni Mpanzi Mkuu. Lazima tuungane nae tuanze kupanda mbengu za injili zaidi na pasipo kubagua. “Unaposikia maneno, mpanzi alitoka akaenda kupanda mbegu, usifikirie kwamba ni marudio.  Mpanzi anatoka  mara nyingi kwa malengo mbalimbali; kama  kulima, kung’oa magugu, kutoa miiba au kazi nyingine yoyote, lakini mtu huyo alienda moja kwa mojakupanda. Ni jambo lilitokea kwa mbegu? Robo tatu ziliharibika, na robo moja ilibakia; lakini siyo zote kwa namna ile, lakini kwa utofauti fulani, na alivyopanda nyingine zilianguka njiani” (Mt. Yohane Krisostomu)

Shetani anatumia mbinu ifuatazo kunyakua kilichopandwa moyoni yaani neno la Mungu.  Shetani anatumia mbinu ya kutoona. Mwenye macho haambiwi tazama. Yaani mtu akiwa na haja na kitu ni juu yake kukishughulikia. Hauwezi kungoja kuletewa mambo mazuri. “Penye miti hakuna wajenzi.” Ndivyo isemavyo methali ya Kiswahili. Ni kama watu hawaoni hiyo miti. Kuna vitu ambavyo vinaweza kumfanya mtu hasione. Mazoea huleta dharau, lakini mazoea huleta upofu. Tunaambiwa, “Kutazama mtatazama, lakini hamtaona.” (Mathayo 13: 14) Chuki bila sababu au maamuzi mbele yaweza kumfanya mtu hasione mfano Nathanaeli. “Naye Nathanaeli akamwuliza Filipo, “Je, kitu chema chaweza kutoka Nazareti?” (Yohane 1: 46) Ukabila unaweza kumfanya mtu asione zuri kutoka kabila fulani. Ubaguzi wa rangi unaweza kumfanya mtu hasione jambo zuri kutoka watu wa rangi tofauti na yake, ingawa damu yao wote ni nyekundu.

Mbinu  nyingene  ya shetani ya kuondoa mbegu iliyopandwa moyoni ni kuleta shaka au mashaka. Shetani aliwaletea Adamu na Eva mashaka katika sura ya nyoka kama tunavyosoma katika Biblia.  “Basi nyoka akamwambia huyo mwanamke, “Ati! Hivi ndivyo alivyosema Mungu, msile matunda ya miti yote ya bustani?” (Mwanzo 3: 1) Shetani alimletea Yesu  mashaka, “Ikiwa ndiwe Mwana wa Mungu, amuru kwamba mawe haya yawe nikate.” (Mathayo 4: 3)  Maneno ati, eti na ikiwa ni maneno ya kuonyesha au kueleza shaka au wasiwasi juu ya jambo.  Mashaka utengeneza milima ambayo imani inaweza kuhamisha. Sala ya mtu mwenye mashaka iko hivi, “Ee Mungu – kama yupo Mungu kweli okoa roho yangu kama nina roho kweli.Amina.”

 Kuondoa hofu ni mbinu ambayo shetani hutumia kuondoa mbegu iliyopandwa moyoni. Watu hukimbia kumkwepa nyoka na nyoka hukimbia kukwepa watu.” Hiyo ni methali ya Yoruba. Inatufunulia juu ya woga na hofu. Shetani alimuondolea hofu Eva. “Nyoka akamwambia mwanamke, ‘Hakika hamtakufa.” (Mwanzo 3:4)  Shetani alipomjaribu Yesu alitaka kumwondolea hofu, “Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu jitupe chini; kwa maana imeandikwa, ‘Atakuagiza malaika zake; Na mikononi mwao watakuchukua; usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe.” (Mathayo 4: 6) Shetani alimuondolea hofu kwa kutumia Biblia. Shetani anaweza kukuondolea hofu kwa kutumia Biblia vibaya. Kuna watu wanaofanya ulevi kuwa halali kwa kutumia maneno ya Paulo kwa Timotheo, “Usinywe maji tu, bali unywe divai kidogo kwa ajili ya tumbo lako, kwani unaugua mara kwa mara.” (1 Timotheo 5: 23) Mtume Paulo wa Tarsus hapingi kunywa divai bali anapendekeza kiasi katika neno kidogo. Anapinga ulevi. Lakini kifungu hiki kinaweza kutumiwa vibaya kuendekeza tabia ya ulevi.

 Sala: Mpendwa Yesu, ulipanda Neno la Mungu kwa mapendo, uvumilivu, juhudi na bila kuchoka, nisaidie kukuiga wewe uliye mpanzi wa Neno la Mungu. Amina.

Saturday, July 1, 2017

MSALABA UNABEBEKA




Jumapili ya 13

 “asiyepokea msalaba wake akanitafuta, hafai kwangu.”(Mathayo 10:38)
“Msalaba unamaanisha hakuna maangamizi ya meli baharini bila matumaini; hakuna giza bila mapambazuko; hakuna dhoruba bila bandari,” alisema Papa Mt.Yohane  Paulo II. “Kwa kuchukua msalaba, haimaanishi kitu kingine chochote zaidi ya kwamba tunapaswa kupokea na kuteseka kwa sababu ya  maumivu, mambo yanayopingana, mateso na kujikatalia tunavyopitia,” alisema Mtakatifu Francis wa Sales. Inabidi tubebe misalaba yetu badala ya kuiongelea tu. Tarehe 25 Oktoba 1970 Papa Paul VI aliwatangaza  watakatifu mashahidi40 wa Kiingereza. Alexander Briant alijitengenezea kimsalaba kidogo wakati wa kufungwa kwake jela na siku ya kuuwawa kwake alikishikilia mikononi mwake wakati wa hukumu ya kifo inatolewa.Walimyanganya kimsalaba chake, lakini alimwambia jaji: “Unaweza kukichukua toka mikononi mwangu na  si kutoka  moyoni mwangu.”  Msalaba juu ya Golgotha ​​hauwezi kukubadilisha wewe kama si haukusimikwa moyoni mwako. 

Msalaba ni mzigo lakini unabebeka kwa vile ni mzigo mwepesi. “Ukiubeba msalaba ipasvyo, msalaba utakubeba,” alisema Thomas à Kempis. Watoto ni misalaba lakini wanabebeka. Mzazi akiwabeba vyema nao baadaye watoto watambeba, akiisha zeeka hana nguvu watamtunza kama aliwaandalia vizuri maisha ya kesho. Kuna mtoto wa miaka kumi na miwili alikuwa amembeba mdogo wake wa mwaka mmoja. Alipoulizwa na jirani kama ni mzito. Mtoto alijibu, “Si mzito kwa vile ni ndugu yangu.” Siku moja rafiki wa baba aliyekuwa na watoto wanne alimuuliza, “Kwa nini unawapenda watoto wako?” Baba huyo alifikiria kwa dakika  na kupata jibu moja ambalo angelitumia, “Kwa sababu ni wangu.”  Watoto wanapendwa na wanapendeka. Wanabebeka kwa vile wanapendwa. Nao watoto wanawajibu kama isemavyo, ukibebwa bebeka.

Yesu alisema, “Mtu akitaka kuwa mfuasi wangu, ajikane mwenyewe, lazima ajitwike msalaba wake kila siku, anifuate” (Luka 9: 23). “Msalaba unabebwa kwa namna mbili: mwili kwa kujinyima na moyo unapoguswa na huruma” alisema Mtakatifu Gregori. Mzazi anajinyima mambo mazuri ya mwili kama kujipamba, mafuta, chakula kizuri, sehemu nzuri ya kukaa ili mtoto wake asome shule kwa namna hiyo anaubeba msalaba. Mzazi akifikiria maisha ya mbele anawaonea watoto wake huruma aubeba msalaba.  Mungu hakupi msalaba wa kubeba unaozidi uwezo wako. “Msalaba Mungu anaokutumia ameutathimini kwa macho yake yanayojua yote, ameuelewa kwa akili yake ya kimungu, ameujaribu na haki yake yenye hekima, umeupa joto kwa mikono yake ya upendo, ameupima kwa mikono yake kujua kuwa haupitilizi ukubwa hata kwa inchi moja na haupitilizi uzito hata kwa ratili moja, “ alisema Mtakatifu Francis de Sales. Wajibu ni msalaba lakini unabebeka: wajibu wako kwa umma, kwa familia, kwa Mungu na kwako wewe ni msalaba lakini unabebeka.

Msalaba unabebwa kila siku.  Lakini si kila siku ni kila saa. “Na sisi, kwa nini tumo hatarini kila saa? Siku kwa siku nipo taabani” (1 Wakorintho 15:30-31). Inavyoonekana ni jambo gumu kufa kila siku kuliko kufa mara moja. Ina maana kila mara unatoa sadaka ya kitu fulani iwe hata muda wako kwa ajili ya wengine. Mfanyakazi ofisini anabeba msalaba wake wa kazi kila saa. Anaporudi nyumbani kama ana wazazi wa kuwatimizia aja zao anafanya hivyo, kama ana mwenzi wa ndoa anamjali, kama ana watoto anasikiliza shida zao. Ni kila siku karibu ni kila saa kuubeba msalaba.

Sala: Ee Bwana wetu Yesu Kristo nisaidie ili hamasa na nguvu zangu vitoke kwenye kujikatalia na msalaba. Amina.

Counter

You are visitor since April'08