Monday, November 11, 2013

TUONGEZEE IMANI


                                                       Jumatatu ya Juma la 32

 

                  “Mitume wakamwambia Bwana, ‘Tuongezee Imani” (Luka 17: 5)

 

Imani kidogo yaweza kufanya mambo makubwa. Ni ukweli unaoendana na ujumbe wa methali ya Kiswahili, Kidogo kidogo kamba ukatika. Nguvu ya mbegu haitegemei ukubwa au udogo wake inategemea uhai uliofichwa katika mbegu hiyo. Kuna nguvu ambayo imefichwa ndani mwako. Yesu aliwaambia mitume: “Mngekuwa na imani kiasi cha punje ya haradali, mngeuambia mforsadi huu, ‘Ng’oka, kapandikizwe baharini, nao ungewatii” (Luka 17:6). Kama ni hivyo unahitaji kujiamini kuwa utaweza kufanikiwa katika maisha. Kwa imani na kujiamini ndege imevumbuliwa. Kwa imani na kujiamini simu za mkononi zimegunduliwa. Kwa imani na kujiamini utalaamu wa kutengeneza runinga umefunuliwa.

 

Mitume walipoomba kuongezewa imani, Yesu hakusema nimewaongezea imani. Hakuahidi kuwaongezea imani. Ni kama aliwaambia anza na mlicho nacho, kidogo huvuta kikubwa, kidogo huzaa kikubwa, laini huzaa ngumu. Walikuwa kama mfanyabiashara asemaye nina pesa kidogo sana ngoja iwe nyingi ndipo nianze kufanya biashara. Je, itaongezekaje bila kuzalisha, kuuza na kununua? Walikuwa kama mkulima asemaye nina mbegu lakini hazitoshi nitalima nikiwa na mbegu za kutosha. Anza na ulicho nacho. Hawezi kusema sina pesa yote ya kujenga na kumalizia nyumba. Anza kujenga na pesa uliyo nayo. Ili kuwa na zaidi anza na ulicho nacho. Aliyenacho ataongezewa ndivyo  Bwana Yesu alivyofundisha.

 

Mitume walitaka imani yao ikomae na iwe thabiti. “ni kwa kuamini peke yake ndiko imani hukomaa na kuwa thabiti,” aliandika Baba Mtakatifu Benedikto XVI katika kitabu “Mlango wa Imani.”  Mitume wengi walikimbia Yesu alipokamatwa. Huu ni ushahidi wa imani ambayo si thabiti na ambayo haijakomaa. Imani ambayo si thabiti inakuwa na mashaka mengi wakati wa shida na matatizo.  Ni katika msingi huu mitume waliomba waongezewe imani. Baba anapomchukua mtoto wake mdogo wa kike na kumzungusha hewani, mtoto anacheka na kufurahi kwa vile anaamini na ana  imani katika baba yake. Ingawa anajikuta katika hali ambayo si ya kawaida kama miguu kuwa juu na kichwa chini umbali wa futi nne kutoka sakafuni. Haogopi kwa vile anamwamini baba yake. Hii ndiyo imani ambayo ni thabiti na iliyokamaa ambayo hatuna budi kuwa nayo kwa Baba wa mbinguni.  J. Hudson Taylor alimwandikia mke wake wakati mgumu akiwa anafanya kazi ya China Inlanda Mission, “Tuna centi ishirini na tano na ahadi zote za Mungu.”  Ni maneno ya mtu mwenye thabiti katika shida.

 

Counter

You are visitor since April'08