Wednesday, May 10, 2017

KATIKA SHIDA NA RAHA, JARIBU KUSHUKURU



TAFAKARI 11/5/2017

(K)“ Watu na wakushukuru, Ee Mungu. Watu wote na wakushukuru” (Zab 67:5)

Wakati wa raha jaribu kushukuru. Zab 67 iliimbwa katika sikukuu ya shukrani baada ya mavuno (Kut23:24). Wakati wa shida jaribu kushukuru. Katika shida Ayubu alimsifu Mungu: “Bwana alitoa, na Bwana ametwaa; jina la Bwana litukuzwe” (Ayubu 1:21). Kusifu ni kushukuru. Maneno “watu wote” yanabainisha wenye raha na wenye shida, wenye nacho na wasio nacho, wagonjwa na wenye afya, walala hai na walalahoi, walalaheri na hohehahe, wanaoteseka na wanaofurahi.  Watu Wote wamshukuru Mungu. Hata unapokosewa unajifunza kitu fulani, shukuru. “Msamaha wa kweli ni pale unapoweza kusema, ‘Nashukuru kwa uzoefu huo,’” alisema Oprah Winfret. Biblia inatwaambia: “Shukuruni katika kila jambo; maana hayo ni mapenzi ya Mungu kwenu katika Kristo Yesu” (1 Wathesalonike 5: 18). Rick Warren katika kitabu chake Maisha Yanayoongozwa na Malengo alikuwa na haya ya kusema juu ya aya hiyo: “Mungu anakutaka umshukuru kwamba atatumia matatizo yako kutimiza malengo yake.”  Kutoshukuru ni kosa kubwa kuzidi kulipa kisasi. “Kutoshukuru ni kosa la kudharauliwa zaidi ya kulipa kisasi, ambacho ni kulipa baya kwa baya, wakati kutoshukuru ni kulipa baya kwa wema,” alisema William Jordan. Tujenge utamaduni wa kushukuru. Tanzania yenye utamaduni wa kushukuru inawezekana.

Mungu anapotoa hapimi kwa kijiko. Tusimbanie shukrani. Waluhya wana methali isemayo, “Nyama choma haiwezi kuwa tamu ukamsahau aliyeichoma.” Maisha yana baraka, usimsahau anayeleta baraka-Mwenyezi Mungu. Yesu alipoomba kulisha wanaume 5,000 wanaojua kula chakula Mungu Baba alimwongezea kuliko alivyokuwa ameomba wakakusanya mabaki vikapu kumi na viwili. Bikira Maria alipoomba na kusema: Hawana divai. Haikupatikana bora divai bali divai bora-grade one. Mfalme Solomoni aliomba hekima, Mungu akamwongezea na mali. Yosefu aliomba kukumbukwa. Alikumbukwa na zaidi alifanywa Waziri Mkuu. Huu ni mlipuko wa baraka. Kuna mzee fulani aliyekuwa hakosi kuhudhuria adhimisho la Misa. Jumapili moja alihamua kupanga matumizi yake. Aliweka shilingi elfu moja kwenye mfuko wa suruali kwa ajili ya kutoa sadaka na shilingi 10,000/= aliziweka kwenye mfuko wa shati kwa ajili ya matumizi madogo ya nyumbani. Wakati wa kutoa sadaka alitoa noti kwenye mfuko wa shati bila kuitazama. Baadaye alienda dukani kununua sukari na mchele. Baada ya kufunguwa bidhaa hiyo alipoingiza mkono wake kwenye mifuko alipata shilingi 1,000/=. Aimwomba samahani muuza dukani. Kwa kusononokea alienda nyumbani. Baada ya dakika tano akiwa nyumbani alikuja mtu aliyemletea pesa hili kumaliza deni lake la zamani laki tano. Mungu anapotoa hapimi kwa kilo. Kuna namna nyingi za kuwashukuru unaokaa nao.

Kushukuru ni kuomba tena. “Msijisumbue kwa neno lolote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu” (Filp 4:6).  Kushukuru ni kufanya haja zako zijulikane na Mungu. “Shukrani ni moyo wa kutegemea kupata misaada siku za baadaye” (Sir Robert Walpole). “Hakuna kazi ambayo inahitaji kufanyika haraka kama kutoa shukrani” (Mt. Ambrose). Tusishukuru kwa namna ya kuomba miujiza ya ajabu. Kuna mtoto aliyefanya mtihani wa darasa la saba. Usiku wakati wa sala za usiku alisikika akisema: “Mungu nakushukuru ulivyonisaidia kujibu maswali naomba Mwanza ugeuke kuwa Mji Mkuu wa Tanzania.” Kushukuru si kuomba kwa namna hiyo.

Kushukuru ni kuthamini. Mthamini mwenzako. Mungu wetu ni Mungu anayethamini. “Kwa kuwa ulikuwa wa thamani machoni pangu, na mwenye kuheshimiwa, nami nimekupenda” (Isaya 43:4). Wathamini watoto. Maua ya kesho yako kwenye mbegu za leo. Kuna mwalimu mmoja kila wanafunzi walipoingia darasani alisimama mlangoni akimwinamia kila mwanafunzi alipoulizwa kwa nini anafanya hivyo, alisema sijui hawa woto watakuwa wakina nani? Viongozi wangu wa kesho. Aliwathamini si jinsi walivyo tu bali watakavyokuwa. Mwanamke mmoja alimuuliza mke wake: “Mbona kila mara ninapoimba unatoa kichwa dirishani?” Mwanamke akasema: “Nataka majirani wajue kuwa anayeimba vibaya sio mimi.”

Sala: Ee Yesu nisaidie kushukuru katika shida na raha, katika magonjwa na afya, wakati wa vigelegele na wakati wa kelele. Amina.

Monday, May 8, 2017

WAKIWA NA MASHAKA NA UKRISTO WAKO, WEMA NA KAZI ZAKO VIKUSHUHUDIE


“Huko Antiokia, ndiko kwa mara ya kwanza, wafuasi waliitwa Wakristo” (Matendo 11:26)

“Kama tungetenda kama wakristo kweli, pansigekuwepo na watu ambao si wakristo,” alisema Mt. Papa Yohane XXII.  Ni katika mtazamo huo huo, Soame Jenyns alisema: “Kama nchi za kikristo zingekuwa nchi za kikristo, pasingekuwepo na vita.”  Kama ungekamatwa kwa kuwa mkristo, je pangekuwepo na ushahidi wa kutosha wa kukutia hatiani? Je, kuna ushahidi gani wa kuwa wewe ni mkristo. Mkristo kama mshumaa lazima atulie wakati huo huo anawaka mapendo. Mkristo anaonesha ukristo. Ukristo: “Ni wema nyumbani. Katika biashara ni ukweli. Katika jamii ni adabu. Kazini ni kutenda haki. Kwa wenye shida ni huruma. Ni msaada kwa wadhaifu. Upinzani dhidi ya waovu. Ni imani kwa wenye nguvu za kimaadili. Ni ‘msamaha’ kwa wakosefu. Ni furaha kwa waliofanikiwa. Ni uchaji na imani kwa Mungu,” alisema mtu fulani. Ukristo ni kuwa mkristo pale ulipo. Usipokuwa mkristo pale ulipo huwezi kuwa mkristo popote. Wanafunzi walioitwa wakristo walikuwa kwanza wakristo Antiokia.

Mtoto wa miaka minne alimuuliza mama yake: “Hivi mama Yesu unayenielezea habari zake kira mara ni mwema kama wewe? Mama alimjibu: “ Yesu ni mwema sana mimi najitahidi kumuiga.” Mtoto alijibu: “Kama ni hivyo nitampenda.” Wema ni sifa ya kuwa mkristo. Tunaambiwa juu ya mkristo Barnaba: “Barnaba alikuwa mtu mwema na mwenye kujaa Roho Mtakatifu na imani. Kundi kubwa la watu lilivutwa kwa Bwana” (Matendo 11:24).

Sifa nyingine ya mkristo ni kuwatia wengine moyo. Barnaba maana yake mwana wa kutia moyo. Alimtia moyo Paulo. Mtu akinunua pikipiki mtie moyo. Usiseme, “Inafanana na yangu.” Ukaishia hapo. Mtu akinunua nguo nzuri mpongeze. Usiseme, “Nilinunua kama hii mwaka 1970.” Mwanafunzi anayepata maksi za chini, mtie moyo. Dante Gabriel Rossetti mshairi na mchoraji maarufu wa karne ya 19 alitembelewa na mzee fulani. Mzee huyo alikuwa amebeba picha na michoro mbali mbali ambazo alitaka zihakikiwe ili kujua kama ni mizuri. Rossetti alizitazama kwa makini sana. Baada ya kuziangalia chache alisema ukweli kuwa michoro si mizuri. Mgeni huyo alisikitika sana. Alitoa michoro mingine na kumwambia kuwa imechorwa na kijana mwanafunzi. Rosseti alizitazama na kuchangamka na kuwa na furaha na kusema, “Michoro hii ni mizuri. Kijana huyo aliyezichora ana kipaji kikubwa. Apewe kila msaada na kutiwa moyo katika wito wake wa kuwa mchoraji. Kijana huyo ni nani? Ni mtoto wako?” Mzee alijibu. “Siyo mtoto wangu ila ni mimi miaka arobaini iliyopita. Kama miaka hiyo ningesikia maneno mazuri kama haya ningekuwa mchoraji mzuri sana. Hata kama watu hawakutii moyo jitie moyo. Kuna mwanafunzi ambaye alikuwa hapendwi na wenzake. Aliitwa Siima. Hata walimtania kuwa hata kivuli chake hakimpendeki hakiko tayari kumfuata. Siku moja alikuwa anaadhimisha Siku yake ya Kuzaliwa. Alijua kuwa hakuna atakayemwandikia kadi ya pongezi. Alifanya kitu fulani. Wenzake walipokuja kumtembelea na kumkejeli walikuta kadi kumi na mbili. Walishangaa. Walipozisoma zikuwa zote zinatoka kwa mtu mmoja. Kutoka kwa Siima kwenda kwa Siima.

Kazi zako zikushuhudie. “Kazi ninazofanya mimi kwa jina la Baba yangu zinanishuhudia” (Yohane 10:25). Watu walikuwa wamemuuliza Yesu kama ndiye Kristo. Kazi zake za huruma zilimshuhudia. Wewe kama ni mkristo kazi zako zikushuhudie. Matendo ya huruma yakushuhudie. Wewe kama ni daktari wa binadamu, kazi zako zikushuhudie. Wewe kama ni mwalimu kazi zako zikushuhudie. Wewe kama ni mwanasiasa kazi zako zikushuhudie. Pilato alipoambiwa kuwa kuna watu wanasema anaimba vibaya. Alijibu, “Nitafanya mazoezi na kuimba vizuri hakuna atakayewaamini.” Kazi zako zifanye watu wasiamini mabaya yanayosemwa juu yako. Kuna watu waliosema  vibaya juu ya Bwana Yesu alipokuja anakula na kunywa tofauti na Yohane Mbatizaji lakini kazi zake nzuri zilimshuhudia.

Sala: Ee Bwana Yesu nisaidie niwe mkristo kweli, niwe sauti ambayo kwayo utazungumza,niwe moyo ambao kwao utapenda, niwe mikono ambayo kwayo utasaidia. Amina.

 

JIPROGRAMU NA MWACHE MUNGU AKUPROGRAMU



TAFAKARI 8/5/2017

“Nalikuwa katika mji wa Yafa nikiomba, roho yangu ikazimia, nikaona maono” (Matendo 11: 5)

Usipojipogramu watu wabaya watakuprogramu. Mungu asipokuprogramu watu wabaya wanaweza kukuprogramu. Mungu alimprogramu Simoni Petro kupitia ndoto au maono. “Jambo hili lilitendekea mara tatu” (Matendo 10:16). Mungu anatuprogramu mara nyingi. Mungu alitaka Petro abadili mtazamo wake: Kutoka Mungu wa Israeli kwenda Mungu wa mataifa yote. Kutoka kukumbatia waliotahiriwa kwenda kwenye kukumbatia wasiotahiriwa. Kutoka kula nyama ya wanyama walio safi hadi kula nyama ya wanyama najisi kama nguruwe.  Huenda Mungu atakuletea maono kama Petro lakini unaweza kupiga picha kichwani ya mambo mazuri. Unaweza kujiprogramu.

Kuna kitendawili kisemacho: “Nimelala usiku natazama filamu.” Jibu ni ndoto. Hatuna budi kuwa na filamu ya maisha tunayoyataka akilini mwetu.  “Ni muda muafaka wa kuishi maisha ambayo umeyafikiria,” alisema Henry James. Fikiria utakapokuwa kesho. “ Tuko tulivyo na tulipo kwa sababu kwanza tulipafikiria,” Donald Curtis. Kuna mambo kadhaa ya kuzingatia.

Kuwa na picha akilini. Unataka kununua gari, kuwa na picha ya gari hilo akilini. Unataka kuoa, kuwa na picha ya arusi akilini mwako. Unataka kujenga nyumba, kuwa na picha akilini mwako ya nyumba unayoipenda.  “Roho haiwezi kufikiri bila picha,” alisema Aristotle. Tunaweza kusema mtu hawezi kufikiri bila picha. Naye John Holland alisema, “Roho haiwezi kuzungumza bila picha.” Mtu hawezi kuzungumzia mipango yake bila picha. Ukizungumzia duka unalotaka kulianzisha kuwa na picha. Ukizungumzia taasisi unayotaka kujenga kuwa na picha akilini mwako.“ Badili sura za picha kwenye kichwa chako ziendane na maono kwenye moyo wako,” alisema mtu fulani. “Piga picha ya kitu unachokitaka akilini, kione, kihisi, kiamini. Fanya picha ya kitu hicho kichwani mwako, na anza kukijenga,” alisema Robert Collier. “Kupiga picha akilini ni kuona lile ambalo halipo, ambalo halionekani – ndoto.  Kupiga picha akilini kusema kweli na kutengeneza uongo unaonekana. Uongo unaonekana, hata hivyo una namna ya kuwa ukweli wa mambo,” alisema Peter McWilliams.

Fikiri kama kwamba unachokitaka kipo.  “Kuleta jambo katika maisha yako, fikiria kama kwamba tayari lipo,” alisema Richard Bach. Yapigie msitari maneno “kama kwamba” ni maneno muhimu. “Umba maono ya unayetaka kuwa na baadaye ishi katika picha hiyo kama kwamba ni kweli,” alisema Arnold Schwarzenegger.  Ishi kama kwamba lisilowezekana linawezekana. “Watu wa kawaida huamini tu katika linalowezekana. Watu wasio wa kawaida hupiga picha si ya lile ambalo linawezekana au linayamkinika bali lile ambalo haliwezekani. Na kwa kupiga picha ya lile lisilowezekana wanaanza kuliona kama linalowezekana,” alisema Cherie Carter-Scott.

Badili unachokiona. “Toa mawazo yako, maneno yako na macho kwenye mambo yalivyo, na yaweke tu kwenye namna ambavyo unataka mambo yawe,” alisema  Che Garman.  “Mtu anaweza kupokea lile ambalo anaona anapokea,” alisema Florence Scovel Shinn. “Lazima uone kitu vizuri akilini kabla ya kukifanya,” Alex Morrison.

Kuna faida nyingi za kuwa na picha ya unachokitaka akilini.  Kwanza, picha ya unachokitaka inakupa matumaini. “Ukiwa na maono kwa ajili ya maisha yako hilo linakuwezesha kuishi kwa matumaini badala ya hofu zako,” alisema Stedman Graham. Pili, ni kupiga hatua kimaendeleo.  Hatua ya kimaendeleo inategemea upeo wako ulivyo. Upeo wako ukiwa chini hutabaki chini. Upeo wako ukiwa juu utakuwa juu kweli. “Mtu anaweza kukua kiasi ambacho upeo wake unamruhusu,” alisema John Powell. Watu wenye upeo wa juu sana si wa kawaida. Tatu, kunasaidia kufanikiwa.  Ukweli huu unabainishiwa na methali ya kichina: “Dunia ni ya wale ambao wanavuka madaraja mengi katika kufikia kwao kabla ya wengine hawajaona hata daraja moja.” Nne, kupiga picha akilini kunasisimua, na kuleta ari mpya. “Kila dakika, kila saa, piga picha kichwani namna unavyotaka uwe. Sisimukia WEWE mpya,” alisema, Thomas D Willhite. Picha akilini ni kichocheo cha kutenda. "Picha inazaa shauku. Unakusudia lile ambalo umelipigia picha ya akilini,” alisema J. G. Gallimore. “Naota kwa hiyo nakuwa hivyo,” Cheryl Grossman.

Saturday, May 6, 2017

UMENISHAWISHI NAMI NIMESHAWISHIKA

 
                                JUMAPILI YA 4 YA PASAKA
“Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kasha wawe nao tele” (Yohana 10:10).
 Yesu Mchungaji Mwema amekufia endelea kushawishika kumfuata. Yesu kama mchungaji mwema anakujua kwa jina endelea kushawishika kumfuata.  Katika tafakari ya leo tutatumia maneno ya nabii Yeremia: “Ee Bwana umenishawishi nami nimeshawishika” (Yeremia 20:7). Kuna mambo yanayowashawishi watu wamfuate Yesu mchungaji mwema. Katika wito wowote kuna ushawishi na kushawishika.  Katika wito uliomo muombe Bwana Yesu akusaidie kuendelea kushawishika kudumu isije ikasemwa, tulipiga ngoma haukucheza, tuliomboleza haukulia.
  1. UPENDO UPEO
    Upendo upeo ni upendo katika kiwango cha mwisho cha upendo. Ni upendo wa mtu kumfia mwingine. Upendo upeo unaelezwa hivi: “Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo” (Yohana 10:11). Katika Injili ya leo upendo upeo unaelewa hivi: “Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kasha wawe nao tele” (Yohana 10:10). Upendo upeo wa Yesu unashawishi na tunashawishika. Unatuvuta na tunavutiwa. Kuvuta ni kuleta mvuto. Msalaba unatuvuta kwa Yesu. Nakubaliana na John R.W.Stott aliyesema, “Msalaba ni moto uwakao ambapo moto wa upendo wetu unawashwa, na hatuna budi kukaribia sana ili cheche zake zitufikie.” Kama mchungaji mwema atoavyo uhai wake kwa ajili ya kondoo Yesu alitufia msalabani. Upendo wa namna hii unavuta. Yeye alisema: “Nami nikiinuliwa juu ya nchi, nitawavuta wote kwangu” (Yohana 12: 32). Pale pale msalabani kilimvuta askari Yule aliyemchoma Yesu mkuki akawa Mtakatifu Longinus. Longinus maana yake mkuki. “Basi Yule akida, na hao waliokuwa pamoja naye wakimlinda Yesu, walipoliona tetemeko la nchi na mambo yaliyofanyika, wakaogopa sana, wakisema, Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu” (Mathayo 27: 54). Kifo cha Yesu msalabani kiliwavuta akida na wale aliokuwa pamoja naye. Kifo cha Yesu msalabani kinatosha kwa wote kutukomboa lakini umuhimu wake ni kwa wale tu ambao wanakubali zawadi yake hii. Yaani wale wanaovutiwa au kushawishika. Wahaya wa Tanzania wana methali isemayo: Kitu kisichojitingisha ni jiwe. Kifo cha Yesu msalabani kina ushawishi.
    Upendo upeo unadai upendo kwa jirani. Diogenes alikuwa amesimama kwenye kona mtaani siku moja huku akicheka kama mwehu. “ Jambo gani linakufanya ucheke ?” Mpita njia alimuuliza. Unaona jiwe hilo katikati ya njia? Tangia nije hapa asubuhi watu wamekuwa wakijikwaa na kulaani jiwe. Lakini hakuna aliyejisumbua kulitoa ili wengine wasijikwae. Yesu kwa kuwa ni mchungaji ambaye si mtu wa mshahara ametuondolea vikwazo njiani, huu ni upendo upeo.    
  2. JINA KUBWA
    Jina la Yesu ni Jina Kubwa. Kwa kawaida jina huvuta watu. Watunzi mashuhuri wa vitabu huwa hawatangulizi jina la kitabu au kichwa cha kitabu bali jina lao linaandikwa kwa herufi kubwa kuzidi kichwa cha kitabu sababu jina tu linavuta ni “brand.” Watu huwa wanatafuta jina la mtunzi mashuhuri hata bila kujali ameandika nini. Jina la Yesu ni “brand.”  Petro anatwaambia “Jueni ninyi nyote na watu wote  wa Israeli ya kuwa  kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye  ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu…wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina lingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo!” (Mate 4:10-12). Petro alikua anajibu swali hili: “Kwa nguvu gani na kwa jina la nani ninyi mmefanya haya?” (Mate 4:7). Rais wa nchi akiingia hapa tulipo tutasimama kumpa heshima. Lakini Yesu Kristo akiingia hapa tulipo tutapiga magoti kumwabudu. YESU KRISTO ni JINA KUBWA.  Fanya urafiki naye. YESU TOSHA
  3. AHADI ZA KWELI
    Mungu akiahidi anatenda. Mungu akiahidi atafanya. Yesu alihaidi kuwa atafufuka na kweli alifufuka kama Petro anavyotwaambia katika somo la leo: “…ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu” (Mate 4: 10). Ahadi za kweli zinashawishi. Yesu ametushawishi nasi tumeshawishika. Yesu hatoi ahadi hewa. Watu wanavutwa na ahadi za kweli. Kuna aliyeshinda nishani huko Ulaya na kupewa hati ya kusafiri bure kwenye treni kwa kipindi cha miaka kumi. Alitembea amevaa hati ndogo ya kusafiri bure ikininginia shingoni hata siku moja hakusafiri kwa kutumia treni. Mungu ametupa ahadi nzuri. Ametupa kama hati za kusafiri bure. Je tunatumia ahadi za Mungu. Je tunachukua ahadi hizo. Mungu akiahidi anatenda. Yesu akiahidi anatenda. Yesu anashawishi kwa ahadi za kweli. 
    Sala: Ee Bwana wetu Yesu Kristo, nisaidie nishawishike kukufuata kila mara isije ikasemwa, tulipiga ngoma haukucheza, tuliomboleza haukulia. Amina.

Counter

You are visitor since April'08