Monday, May 8, 2017

JIPROGRAMU NA MWACHE MUNGU AKUPROGRAMU



TAFAKARI 8/5/2017

“Nalikuwa katika mji wa Yafa nikiomba, roho yangu ikazimia, nikaona maono” (Matendo 11: 5)

Usipojipogramu watu wabaya watakuprogramu. Mungu asipokuprogramu watu wabaya wanaweza kukuprogramu. Mungu alimprogramu Simoni Petro kupitia ndoto au maono. “Jambo hili lilitendekea mara tatu” (Matendo 10:16). Mungu anatuprogramu mara nyingi. Mungu alitaka Petro abadili mtazamo wake: Kutoka Mungu wa Israeli kwenda Mungu wa mataifa yote. Kutoka kukumbatia waliotahiriwa kwenda kwenye kukumbatia wasiotahiriwa. Kutoka kula nyama ya wanyama walio safi hadi kula nyama ya wanyama najisi kama nguruwe.  Huenda Mungu atakuletea maono kama Petro lakini unaweza kupiga picha kichwani ya mambo mazuri. Unaweza kujiprogramu.

Kuna kitendawili kisemacho: “Nimelala usiku natazama filamu.” Jibu ni ndoto. Hatuna budi kuwa na filamu ya maisha tunayoyataka akilini mwetu.  “Ni muda muafaka wa kuishi maisha ambayo umeyafikiria,” alisema Henry James. Fikiria utakapokuwa kesho. “ Tuko tulivyo na tulipo kwa sababu kwanza tulipafikiria,” Donald Curtis. Kuna mambo kadhaa ya kuzingatia.

Kuwa na picha akilini. Unataka kununua gari, kuwa na picha ya gari hilo akilini. Unataka kuoa, kuwa na picha ya arusi akilini mwako. Unataka kujenga nyumba, kuwa na picha akilini mwako ya nyumba unayoipenda.  “Roho haiwezi kufikiri bila picha,” alisema Aristotle. Tunaweza kusema mtu hawezi kufikiri bila picha. Naye John Holland alisema, “Roho haiwezi kuzungumza bila picha.” Mtu hawezi kuzungumzia mipango yake bila picha. Ukizungumzia duka unalotaka kulianzisha kuwa na picha. Ukizungumzia taasisi unayotaka kujenga kuwa na picha akilini mwako.“ Badili sura za picha kwenye kichwa chako ziendane na maono kwenye moyo wako,” alisema mtu fulani. “Piga picha ya kitu unachokitaka akilini, kione, kihisi, kiamini. Fanya picha ya kitu hicho kichwani mwako, na anza kukijenga,” alisema Robert Collier. “Kupiga picha akilini ni kuona lile ambalo halipo, ambalo halionekani – ndoto.  Kupiga picha akilini kusema kweli na kutengeneza uongo unaonekana. Uongo unaonekana, hata hivyo una namna ya kuwa ukweli wa mambo,” alisema Peter McWilliams.

Fikiri kama kwamba unachokitaka kipo.  “Kuleta jambo katika maisha yako, fikiria kama kwamba tayari lipo,” alisema Richard Bach. Yapigie msitari maneno “kama kwamba” ni maneno muhimu. “Umba maono ya unayetaka kuwa na baadaye ishi katika picha hiyo kama kwamba ni kweli,” alisema Arnold Schwarzenegger.  Ishi kama kwamba lisilowezekana linawezekana. “Watu wa kawaida huamini tu katika linalowezekana. Watu wasio wa kawaida hupiga picha si ya lile ambalo linawezekana au linayamkinika bali lile ambalo haliwezekani. Na kwa kupiga picha ya lile lisilowezekana wanaanza kuliona kama linalowezekana,” alisema Cherie Carter-Scott.

Badili unachokiona. “Toa mawazo yako, maneno yako na macho kwenye mambo yalivyo, na yaweke tu kwenye namna ambavyo unataka mambo yawe,” alisema  Che Garman.  “Mtu anaweza kupokea lile ambalo anaona anapokea,” alisema Florence Scovel Shinn. “Lazima uone kitu vizuri akilini kabla ya kukifanya,” Alex Morrison.

Kuna faida nyingi za kuwa na picha ya unachokitaka akilini.  Kwanza, picha ya unachokitaka inakupa matumaini. “Ukiwa na maono kwa ajili ya maisha yako hilo linakuwezesha kuishi kwa matumaini badala ya hofu zako,” alisema Stedman Graham. Pili, ni kupiga hatua kimaendeleo.  Hatua ya kimaendeleo inategemea upeo wako ulivyo. Upeo wako ukiwa chini hutabaki chini. Upeo wako ukiwa juu utakuwa juu kweli. “Mtu anaweza kukua kiasi ambacho upeo wake unamruhusu,” alisema John Powell. Watu wenye upeo wa juu sana si wa kawaida. Tatu, kunasaidia kufanikiwa.  Ukweli huu unabainishiwa na methali ya kichina: “Dunia ni ya wale ambao wanavuka madaraja mengi katika kufikia kwao kabla ya wengine hawajaona hata daraja moja.” Nne, kupiga picha akilini kunasisimua, na kuleta ari mpya. “Kila dakika, kila saa, piga picha kichwani namna unavyotaka uwe. Sisimukia WEWE mpya,” alisema, Thomas D Willhite. Picha akilini ni kichocheo cha kutenda. "Picha inazaa shauku. Unakusudia lile ambalo umelipigia picha ya akilini,” alisema J. G. Gallimore. “Naota kwa hiyo nakuwa hivyo,” Cheryl Grossman.

Counter

You are visitor since April'08