Wednesday, May 10, 2017

KATIKA SHIDA NA RAHA, JARIBU KUSHUKURU



TAFAKARI 11/5/2017

(K)“ Watu na wakushukuru, Ee Mungu. Watu wote na wakushukuru” (Zab 67:5)

Wakati wa raha jaribu kushukuru. Zab 67 iliimbwa katika sikukuu ya shukrani baada ya mavuno (Kut23:24). Wakati wa shida jaribu kushukuru. Katika shida Ayubu alimsifu Mungu: “Bwana alitoa, na Bwana ametwaa; jina la Bwana litukuzwe” (Ayubu 1:21). Kusifu ni kushukuru. Maneno “watu wote” yanabainisha wenye raha na wenye shida, wenye nacho na wasio nacho, wagonjwa na wenye afya, walala hai na walalahoi, walalaheri na hohehahe, wanaoteseka na wanaofurahi.  Watu Wote wamshukuru Mungu. Hata unapokosewa unajifunza kitu fulani, shukuru. “Msamaha wa kweli ni pale unapoweza kusema, ‘Nashukuru kwa uzoefu huo,’” alisema Oprah Winfret. Biblia inatwaambia: “Shukuruni katika kila jambo; maana hayo ni mapenzi ya Mungu kwenu katika Kristo Yesu” (1 Wathesalonike 5: 18). Rick Warren katika kitabu chake Maisha Yanayoongozwa na Malengo alikuwa na haya ya kusema juu ya aya hiyo: “Mungu anakutaka umshukuru kwamba atatumia matatizo yako kutimiza malengo yake.”  Kutoshukuru ni kosa kubwa kuzidi kulipa kisasi. “Kutoshukuru ni kosa la kudharauliwa zaidi ya kulipa kisasi, ambacho ni kulipa baya kwa baya, wakati kutoshukuru ni kulipa baya kwa wema,” alisema William Jordan. Tujenge utamaduni wa kushukuru. Tanzania yenye utamaduni wa kushukuru inawezekana.

Mungu anapotoa hapimi kwa kijiko. Tusimbanie shukrani. Waluhya wana methali isemayo, “Nyama choma haiwezi kuwa tamu ukamsahau aliyeichoma.” Maisha yana baraka, usimsahau anayeleta baraka-Mwenyezi Mungu. Yesu alipoomba kulisha wanaume 5,000 wanaojua kula chakula Mungu Baba alimwongezea kuliko alivyokuwa ameomba wakakusanya mabaki vikapu kumi na viwili. Bikira Maria alipoomba na kusema: Hawana divai. Haikupatikana bora divai bali divai bora-grade one. Mfalme Solomoni aliomba hekima, Mungu akamwongezea na mali. Yosefu aliomba kukumbukwa. Alikumbukwa na zaidi alifanywa Waziri Mkuu. Huu ni mlipuko wa baraka. Kuna mzee fulani aliyekuwa hakosi kuhudhuria adhimisho la Misa. Jumapili moja alihamua kupanga matumizi yake. Aliweka shilingi elfu moja kwenye mfuko wa suruali kwa ajili ya kutoa sadaka na shilingi 10,000/= aliziweka kwenye mfuko wa shati kwa ajili ya matumizi madogo ya nyumbani. Wakati wa kutoa sadaka alitoa noti kwenye mfuko wa shati bila kuitazama. Baadaye alienda dukani kununua sukari na mchele. Baada ya kufunguwa bidhaa hiyo alipoingiza mkono wake kwenye mifuko alipata shilingi 1,000/=. Aimwomba samahani muuza dukani. Kwa kusononokea alienda nyumbani. Baada ya dakika tano akiwa nyumbani alikuja mtu aliyemletea pesa hili kumaliza deni lake la zamani laki tano. Mungu anapotoa hapimi kwa kilo. Kuna namna nyingi za kuwashukuru unaokaa nao.

Kushukuru ni kuomba tena. “Msijisumbue kwa neno lolote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu” (Filp 4:6).  Kushukuru ni kufanya haja zako zijulikane na Mungu. “Shukrani ni moyo wa kutegemea kupata misaada siku za baadaye” (Sir Robert Walpole). “Hakuna kazi ambayo inahitaji kufanyika haraka kama kutoa shukrani” (Mt. Ambrose). Tusishukuru kwa namna ya kuomba miujiza ya ajabu. Kuna mtoto aliyefanya mtihani wa darasa la saba. Usiku wakati wa sala za usiku alisikika akisema: “Mungu nakushukuru ulivyonisaidia kujibu maswali naomba Mwanza ugeuke kuwa Mji Mkuu wa Tanzania.” Kushukuru si kuomba kwa namna hiyo.

Kushukuru ni kuthamini. Mthamini mwenzako. Mungu wetu ni Mungu anayethamini. “Kwa kuwa ulikuwa wa thamani machoni pangu, na mwenye kuheshimiwa, nami nimekupenda” (Isaya 43:4). Wathamini watoto. Maua ya kesho yako kwenye mbegu za leo. Kuna mwalimu mmoja kila wanafunzi walipoingia darasani alisimama mlangoni akimwinamia kila mwanafunzi alipoulizwa kwa nini anafanya hivyo, alisema sijui hawa woto watakuwa wakina nani? Viongozi wangu wa kesho. Aliwathamini si jinsi walivyo tu bali watakavyokuwa. Mwanamke mmoja alimuuliza mke wake: “Mbona kila mara ninapoimba unatoa kichwa dirishani?” Mwanamke akasema: “Nataka majirani wajue kuwa anayeimba vibaya sio mimi.”

Sala: Ee Yesu nisaidie kushukuru katika shida na raha, katika magonjwa na afya, wakati wa vigelegele na wakati wa kelele. Amina.

Counter

You are visitor since April'08