Monday, May 8, 2017

WAKIWA NA MASHAKA NA UKRISTO WAKO, WEMA NA KAZI ZAKO VIKUSHUHUDIE


“Huko Antiokia, ndiko kwa mara ya kwanza, wafuasi waliitwa Wakristo” (Matendo 11:26)

“Kama tungetenda kama wakristo kweli, pansigekuwepo na watu ambao si wakristo,” alisema Mt. Papa Yohane XXII.  Ni katika mtazamo huo huo, Soame Jenyns alisema: “Kama nchi za kikristo zingekuwa nchi za kikristo, pasingekuwepo na vita.”  Kama ungekamatwa kwa kuwa mkristo, je pangekuwepo na ushahidi wa kutosha wa kukutia hatiani? Je, kuna ushahidi gani wa kuwa wewe ni mkristo. Mkristo kama mshumaa lazima atulie wakati huo huo anawaka mapendo. Mkristo anaonesha ukristo. Ukristo: “Ni wema nyumbani. Katika biashara ni ukweli. Katika jamii ni adabu. Kazini ni kutenda haki. Kwa wenye shida ni huruma. Ni msaada kwa wadhaifu. Upinzani dhidi ya waovu. Ni imani kwa wenye nguvu za kimaadili. Ni ‘msamaha’ kwa wakosefu. Ni furaha kwa waliofanikiwa. Ni uchaji na imani kwa Mungu,” alisema mtu fulani. Ukristo ni kuwa mkristo pale ulipo. Usipokuwa mkristo pale ulipo huwezi kuwa mkristo popote. Wanafunzi walioitwa wakristo walikuwa kwanza wakristo Antiokia.

Mtoto wa miaka minne alimuuliza mama yake: “Hivi mama Yesu unayenielezea habari zake kira mara ni mwema kama wewe? Mama alimjibu: “ Yesu ni mwema sana mimi najitahidi kumuiga.” Mtoto alijibu: “Kama ni hivyo nitampenda.” Wema ni sifa ya kuwa mkristo. Tunaambiwa juu ya mkristo Barnaba: “Barnaba alikuwa mtu mwema na mwenye kujaa Roho Mtakatifu na imani. Kundi kubwa la watu lilivutwa kwa Bwana” (Matendo 11:24).

Sifa nyingine ya mkristo ni kuwatia wengine moyo. Barnaba maana yake mwana wa kutia moyo. Alimtia moyo Paulo. Mtu akinunua pikipiki mtie moyo. Usiseme, “Inafanana na yangu.” Ukaishia hapo. Mtu akinunua nguo nzuri mpongeze. Usiseme, “Nilinunua kama hii mwaka 1970.” Mwanafunzi anayepata maksi za chini, mtie moyo. Dante Gabriel Rossetti mshairi na mchoraji maarufu wa karne ya 19 alitembelewa na mzee fulani. Mzee huyo alikuwa amebeba picha na michoro mbali mbali ambazo alitaka zihakikiwe ili kujua kama ni mizuri. Rossetti alizitazama kwa makini sana. Baada ya kuziangalia chache alisema ukweli kuwa michoro si mizuri. Mgeni huyo alisikitika sana. Alitoa michoro mingine na kumwambia kuwa imechorwa na kijana mwanafunzi. Rosseti alizitazama na kuchangamka na kuwa na furaha na kusema, “Michoro hii ni mizuri. Kijana huyo aliyezichora ana kipaji kikubwa. Apewe kila msaada na kutiwa moyo katika wito wake wa kuwa mchoraji. Kijana huyo ni nani? Ni mtoto wako?” Mzee alijibu. “Siyo mtoto wangu ila ni mimi miaka arobaini iliyopita. Kama miaka hiyo ningesikia maneno mazuri kama haya ningekuwa mchoraji mzuri sana. Hata kama watu hawakutii moyo jitie moyo. Kuna mwanafunzi ambaye alikuwa hapendwi na wenzake. Aliitwa Siima. Hata walimtania kuwa hata kivuli chake hakimpendeki hakiko tayari kumfuata. Siku moja alikuwa anaadhimisha Siku yake ya Kuzaliwa. Alijua kuwa hakuna atakayemwandikia kadi ya pongezi. Alifanya kitu fulani. Wenzake walipokuja kumtembelea na kumkejeli walikuta kadi kumi na mbili. Walishangaa. Walipozisoma zikuwa zote zinatoka kwa mtu mmoja. Kutoka kwa Siima kwenda kwa Siima.

Kazi zako zikushuhudie. “Kazi ninazofanya mimi kwa jina la Baba yangu zinanishuhudia” (Yohane 10:25). Watu walikuwa wamemuuliza Yesu kama ndiye Kristo. Kazi zake za huruma zilimshuhudia. Wewe kama ni mkristo kazi zako zikushuhudie. Matendo ya huruma yakushuhudie. Wewe kama ni daktari wa binadamu, kazi zako zikushuhudie. Wewe kama ni mwalimu kazi zako zikushuhudie. Wewe kama ni mwanasiasa kazi zako zikushuhudie. Pilato alipoambiwa kuwa kuna watu wanasema anaimba vibaya. Alijibu, “Nitafanya mazoezi na kuimba vizuri hakuna atakayewaamini.” Kazi zako zifanye watu wasiamini mabaya yanayosemwa juu yako. Kuna watu waliosema  vibaya juu ya Bwana Yesu alipokuja anakula na kunywa tofauti na Yohane Mbatizaji lakini kazi zake nzuri zilimshuhudia.

Sala: Ee Bwana Yesu nisaidie niwe mkristo kweli, niwe sauti ambayo kwayo utazungumza,niwe moyo ambao kwao utapenda, niwe mikono ambayo kwayo utasaidia. Amina.

 

Counter

You are visitor since April'08