Saturday, May 6, 2017

UMENISHAWISHI NAMI NIMESHAWISHIKA

 
                                JUMAPILI YA 4 YA PASAKA
“Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kasha wawe nao tele” (Yohana 10:10).
 Yesu Mchungaji Mwema amekufia endelea kushawishika kumfuata. Yesu kama mchungaji mwema anakujua kwa jina endelea kushawishika kumfuata.  Katika tafakari ya leo tutatumia maneno ya nabii Yeremia: “Ee Bwana umenishawishi nami nimeshawishika” (Yeremia 20:7). Kuna mambo yanayowashawishi watu wamfuate Yesu mchungaji mwema. Katika wito wowote kuna ushawishi na kushawishika.  Katika wito uliomo muombe Bwana Yesu akusaidie kuendelea kushawishika kudumu isije ikasemwa, tulipiga ngoma haukucheza, tuliomboleza haukulia.
  1. UPENDO UPEO
    Upendo upeo ni upendo katika kiwango cha mwisho cha upendo. Ni upendo wa mtu kumfia mwingine. Upendo upeo unaelezwa hivi: “Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo” (Yohana 10:11). Katika Injili ya leo upendo upeo unaelewa hivi: “Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kasha wawe nao tele” (Yohana 10:10). Upendo upeo wa Yesu unashawishi na tunashawishika. Unatuvuta na tunavutiwa. Kuvuta ni kuleta mvuto. Msalaba unatuvuta kwa Yesu. Nakubaliana na John R.W.Stott aliyesema, “Msalaba ni moto uwakao ambapo moto wa upendo wetu unawashwa, na hatuna budi kukaribia sana ili cheche zake zitufikie.” Kama mchungaji mwema atoavyo uhai wake kwa ajili ya kondoo Yesu alitufia msalabani. Upendo wa namna hii unavuta. Yeye alisema: “Nami nikiinuliwa juu ya nchi, nitawavuta wote kwangu” (Yohana 12: 32). Pale pale msalabani kilimvuta askari Yule aliyemchoma Yesu mkuki akawa Mtakatifu Longinus. Longinus maana yake mkuki. “Basi Yule akida, na hao waliokuwa pamoja naye wakimlinda Yesu, walipoliona tetemeko la nchi na mambo yaliyofanyika, wakaogopa sana, wakisema, Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu” (Mathayo 27: 54). Kifo cha Yesu msalabani kiliwavuta akida na wale aliokuwa pamoja naye. Kifo cha Yesu msalabani kinatosha kwa wote kutukomboa lakini umuhimu wake ni kwa wale tu ambao wanakubali zawadi yake hii. Yaani wale wanaovutiwa au kushawishika. Wahaya wa Tanzania wana methali isemayo: Kitu kisichojitingisha ni jiwe. Kifo cha Yesu msalabani kina ushawishi.
    Upendo upeo unadai upendo kwa jirani. Diogenes alikuwa amesimama kwenye kona mtaani siku moja huku akicheka kama mwehu. “ Jambo gani linakufanya ucheke ?” Mpita njia alimuuliza. Unaona jiwe hilo katikati ya njia? Tangia nije hapa asubuhi watu wamekuwa wakijikwaa na kulaani jiwe. Lakini hakuna aliyejisumbua kulitoa ili wengine wasijikwae. Yesu kwa kuwa ni mchungaji ambaye si mtu wa mshahara ametuondolea vikwazo njiani, huu ni upendo upeo.    
  2. JINA KUBWA
    Jina la Yesu ni Jina Kubwa. Kwa kawaida jina huvuta watu. Watunzi mashuhuri wa vitabu huwa hawatangulizi jina la kitabu au kichwa cha kitabu bali jina lao linaandikwa kwa herufi kubwa kuzidi kichwa cha kitabu sababu jina tu linavuta ni “brand.” Watu huwa wanatafuta jina la mtunzi mashuhuri hata bila kujali ameandika nini. Jina la Yesu ni “brand.”  Petro anatwaambia “Jueni ninyi nyote na watu wote  wa Israeli ya kuwa  kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye  ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu…wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina lingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo!” (Mate 4:10-12). Petro alikua anajibu swali hili: “Kwa nguvu gani na kwa jina la nani ninyi mmefanya haya?” (Mate 4:7). Rais wa nchi akiingia hapa tulipo tutasimama kumpa heshima. Lakini Yesu Kristo akiingia hapa tulipo tutapiga magoti kumwabudu. YESU KRISTO ni JINA KUBWA.  Fanya urafiki naye. YESU TOSHA
  3. AHADI ZA KWELI
    Mungu akiahidi anatenda. Mungu akiahidi atafanya. Yesu alihaidi kuwa atafufuka na kweli alifufuka kama Petro anavyotwaambia katika somo la leo: “…ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu” (Mate 4: 10). Ahadi za kweli zinashawishi. Yesu ametushawishi nasi tumeshawishika. Yesu hatoi ahadi hewa. Watu wanavutwa na ahadi za kweli. Kuna aliyeshinda nishani huko Ulaya na kupewa hati ya kusafiri bure kwenye treni kwa kipindi cha miaka kumi. Alitembea amevaa hati ndogo ya kusafiri bure ikininginia shingoni hata siku moja hakusafiri kwa kutumia treni. Mungu ametupa ahadi nzuri. Ametupa kama hati za kusafiri bure. Je tunatumia ahadi za Mungu. Je tunachukua ahadi hizo. Mungu akiahidi anatenda. Yesu akiahidi anatenda. Yesu anashawishi kwa ahadi za kweli. 
    Sala: Ee Bwana wetu Yesu Kristo, nisaidie nishawishike kukufuata kila mara isije ikasemwa, tulipiga ngoma haukucheza, tuliomboleza haukulia. Amina.

Counter

You are visitor since April'08