Tuesday, December 24, 2013

KRISMASI NI VIGELEGELE SIO KELELE


 

                                                     NOELI USIKU

1. Isa 9: 1-6
2. Tit 2: 11-14
3. Lk 2: 1-14

“Wanashangilia mbele yako, kama wanavyoshangilia wavunaji” (Isaya 9: 2)

“Mara jeshi kubwa la mbinguni wakawa pamoja na malaika wakimsifu Mungu, na kusema: Utukufu kwa Mungu juu, na amani duniani kwa watu aliopendezwa nao,” (Luka 2: 13-14)

UTANGULIZI

Kuna aliyemuuliza mtoto, “je umepata kile ulichohitaji katika Krismasi hii?” Mtoto alijibu sikupata kila nilichohitaji na kila nilichotegemea. Lakini hata hivyo siku ya leo siyo siku yangu ya kuzaliwa ni siku ya kuzaliwa Yesu Kristu.”  Ni vizuri watoto watambue kuwa Krismasi siyo siku yao ya kuzaliwa (labda kama mtoto alizaliwa tarehe 25/Desemba naye atakuwa anasherekea siku yake ya kuzaliwa lakini siyo Krismasi) ni siku ya Kuzaliwa Yesu Kristu. Tatizo tunaweza kutekwa na kile kinachouzwa tukamsahau yule aliyesababisha vitu vyenye heri ya Krismasi viuzwe. Naye ni Yesu. Maneno ya kutakiana heri: Heri Krismasi. Baraka ya Krismasi. Furaha ya Krismasi yatukumbushe juu ya Yesu ambaye ni baraka kwa dunia. Kwa sababu yake kuna mabadiliko. Wafuasi wa Yesu wanafanya mengi ya maendeleo. Kuna Hospitali zimejengwa na madhehebu ya Kikristu. Kuna mashule, mazahanati, vyuo na misaada mingi kwa watu walionamatatizo vinavyofanywa na wafuasi wa Yesu. Krismasi itukumbushe wema aliotenda Yesu na awe mfano wa kuigwa.

Kote duniani madhehebu mengi ya Kikristo yanasherehekea kuzaliwa kwa Yesu Kristu. Sherehe hii inajulikana kama Krismasi, Noeli, Sikukuu ya Kuzaliwa kwa Yesu Kristu, mhasisi wa dini ya Kikristu. Krismasi ni vigelegele sio kelele. “Mara jeshi kubwa la mbinguni wakawa pamoja na malaika wakimsifu Mungu, na kusema: Utukufu kwa Mungu juu, na amani duniani kwa watu aliopendezwa nao,” (Luka 2: 13-14. Hakuna mtu anayependa Krismasi imkute kifungoni au jela. Taarifa ambazo huwa tunazipata toka zahanati na hospitalini ni kuwa wakati wa Krismasi wagonjwa wanapungua wadini. Hakuna ambaye anapenda Krismasi imkute wadini. Lakini ugonjwa haubishi hodi na hauna kalenda. Kipindi cha Krismasi ni kipindi cha kufurahi. Mtume Paulo anatukumbusha, “ Basi, furahini daima katika kuungana na Bwana! Nasema tena: furahini!” (Wafilipi 4:4).

MAHUBIRI YENYEWE

“Kwa kawaida Krismasi huonekana kuwa ni likizo yenye kelele: litakuwa ni jambo zuri kwetu kuwa na ukimya kidogo…kuwa kimya ili uweze kusikia upole wa Mungu,” alisema Papa Fransisco Kiongozi wa Kanisa Katoliki. Methali ya Kiswahili inasema yote: kelele nyingi ni makeke (vishindo). Kelele nyingi haziwezi kutimiza chochote na huwa ni usumbufu tu kwani kelele nyingi ni sawa na vishindo. Methali hii hutuonya dhidi ya kupayuka. Kelele za muziki wa kusumbua jirani nyumbani, kelele za muziki kwenye matatu, kelele za bunduki, kelele za milio ya simu kwenye sehemu za ibada, kelele kwenye sehemu za starehe vinaharibu heshima ya Krismasi.

Kelele ni uchafu. Ni uchafuzi wa mazingira kupiga kelele. “Kelele zote ni uchafu. Kuza tabia ya utulivu katika katika maneno, katika mawazo yako na katika hisia zako. Kwa kawaida zungumza kwa sauti ya chini,”  alisema Elbert Hubbard  (1856-1915) mhariri na mwandishi wa Amerika.  Kelele ni kama maji taka. Vigelegele ni kama maji safi. Ukimya ni kama maji salama. Kelele zinakosa sifa moja kubwa sifa ya utulivu na ukimya. Vigelegele ni matokeo ya ukimya na kuwaza matendo makuu. Kelele si matokeo ya ukimya bali ukosefu wa ukimya. Nyota hazipigi kelele. Ni methali ya Ireland. Watu ambao ni nyota au mashuhuri hawapigi kelele. Mama wa Yesu Maria aliyatafakari katika ukimya matendo makuu ya Mungu Krismasi ya kwanza. “Naye Maria akatunza mambo hayo yote akiyawaza moyoni mwake” (Luka 2:19). Aliyatafakari kwa mwanga wa maandiko ya Agano la Kale.

Krismasi ni kipindi cha aina yake cha kumtafuta Mungu. “Tunahitaji kumtafuta Mungu, na hapatikani katika kelele na kutotulia. Mungu ni rafiki wa ukimya. Tazama viumbe – miti, maua, nyasi vinakua katika ukimya; tazama nyota, mwezi na jua vinafanya mambo katika ukimya.. Tunahitaji ukimya kuweza kugusa nyoyo za watu,” alisema Mama Tereza wa Calcutta. Kipindi cha Krismasi unaimbwa wimbo ambao umevuta nyoyo za watu “Silent Night” ambao umetafsiriwa kwa Kiswahili: Usiku mkuu! Usiku Mtakatifu! Uko utulivu; Bikira amezaa Mwana, Mtoto Mtakatifu ni Bwana; Alale amanini, Alale amanini.” Wimbo huu unazungumzia ukimya, utulivu, ukuu na utakatifu wa usiku alipozaliwa Yesu. Utulivu huu na ukimya huo ni wito wa kuwa na utamaduni wa kuwa kimya na kutulia. Wakati wa vita ya kwanza ya dunia Krismasi ya mwaka 1914 vikosi vyote vilivyokuwa vinapigana viliweka siraha chini na kuimba wimbo wa “Silent Night.” Kelele za bunduki zilisimamishwa. Lakini pongezi ingekuwa kama kelele hizo zingesimamishwa siku zote na sio usiku tu wa Krismasi. Utamaduni wa kutochafua hewa kwa kelele lisiwe suala la Krismasi tu.

Kadiri ya Kamusi ya Karne ya 21 kelele ni sauti kubwa sana. Kelele ni hali ya kutokuwa na utulivu; fujo, ghasia, rabsha, nyange, ngenga, chachawizo. Penye kelele kuna kutosikilizana. Penye kelele kuna kutoheshimiana. Penye kelele kuna kukasirikiana. Penye kelele hakuna mshikamano. Penye kelele hakuna utaratibu. Tukumbuke methali ya Kiswahili. Kelele za mpangaji hazimnyimi usingizi mwenye nyumba. Ni kama methali isemayo: Kelele za mwenye nyumba hazimkatazi mgeni kulala. Ni ushauri kuwa mtu mwenye nia ya kutimiza jambo fulani, hagutushwi na lawama, shutuma au malalamiko ya watu wengine wanaonuia kumkatisha tamaa.

 

Kelele za mlango hazininyimi usingizi. Ni methali ya Kiswahili. Mtu anapoamua kulala hajishughulishi na mlio au kelele za mlango kufungwa na kufunguliwa. Tunapoendelea na kazi zetu tusiwajali watu wenye kutuambia maneno ya upuuzi nay a kutuharibia wakati wetu. Tunapaswa kuwapuuza watu kama hao. Macho ya chura hayamnyimi ng’ombe kunywa maji.

 Krismasi ni kipindi cha kupiga vigelegele na si kelele. Kigelegele ni sauti ya kushangilia inayofanywa katika arusi kwa kuchezesha ulimi mdomoni. Lakini ulimi lazima uwekewe utaratibu usije ukachafua mazingira kwa kelele. Mbwa anapendwa na wengi sababu muda mwingi anatingisha mkia badala ya ulimi. Kupiga kelele na kusema kwa sauti ya juu ni ushahidi tosha kuwa mtu hana pointi au nguvu ya hoja. Nakubaliana na  mwanafalsafa wa Kifaransa na mwandishi Michel de Montaigne (1533-1592) aliyesema: “yeye anayejenga hoja yake kwa kelele na amri anaonyesha kuwa hoja yake ni dhaifu.” Kuna watoto wawili ambao walikuwa wanajidai juu ya uwezo wa mama zao. Mmoja akasema: mama yangu anaweza kutoa hotuba bila kusoma karatasi. Mwingine akasema: mama yangu anaweza kutoa hotuba bila kufikiria. Kutoa hotuba bila kufikiria ni kupiga kelele. Ukweli unabaki Krismasi ni vigelegele si kelele.

 

 KRISMASI NI KUTAJIRISHANA

 “Yeye amejitoa mwenyewe kwa ajili yetu” (Tito 2: 14)

Hakuna ambaye ni maskini kiasi cha kutokuwa na chochote cha kutoa na hakuna ambaye ni tajiri kiasi cha kutohitaji lolote. Krismasi imepambwa na ukarimu. “Krismasi, mwanangu, ni upendo kwa vitendo. Kila mara tunapopenda, kila mara tunapotoa, ni Krismasi,” alisema Dale Evans. Sura ya Krismasi ni sura ya ukarimu. Kutumiana zawadi. Kutumiana kadi za heri ya Krismasi. Watoto kununuliwa nguo. Watu wazima kununuliana nguo. Watoto wawili wadogo walikuwa wamemtembelea babu yao siku tatu kabla ya sikukuu ya Krismasi. Usiku walipiga magoti upandeni mwa kitanda kusali sala za usiku . Mdogo kiumri alipaza sauti kadiri ya mapafu yake yalivyomruhusu “Naomba nipate baisikeli mpya. Naomba nipate baisikeli mpya. Naomba nipate baisikeli mpya. Naomba nipate baisikeli mpya…” Kaka yake alimwambia mbona unaomba kwa sauti ya juu sana Mungu sio kiziwi anasikia. Mtoto mdogo alijibu. Mungu anasikia lakini babu yangu atakeyeninunulia baisikeli anajifanya kutosikia. Kipindi cha Krismasi ni kipindi cha kuwasikiliza watoto. Tutajirishane kwa kusikilizana. Kuna methali ya Nigeria isemayo: “Sikiliza na utasikia sauti ya hatua ya mchwa.” Sikiliza mwili wa mwenzako unaongea. Hasira, upendo, huruma vinaonekana kwenye mwili.

 Itakuwa makosa makubwa kuadhimisha Krismasi bila kumtaja Kristo, kuuza kadi za Krismasi bila kuandikwa jina Kristo. “Nilifunga zawadi zangu za Krismasi kwenye karatasi za kufungia zawadi lakini nilitumia karatasi ambazo si sahihi zilikuwa na meneno: Heri ya Kuzaliwa. Sikutaka kuzipoteza nikaongeza neno Yesu,” alisema Demetri Martin. 

Jina hilo Kristo wakati wa Krismasi linatajirisha wengi. Biblia yasema “Katika Kristo Yesu mmetajirika katika yote, katika kila neno na kila utambuzi” ( 1 Wakorintho 1:5). Yesu alikuja kututajirisha. Ikumbukwe vipimo vya utajiri si pesa tu. Yesu anaitwa mshauri wa ajabu. Ametutarisha kwa maneno ya ushauri katika Biblia. Nawe toa ushauri wa kutajirisha wengine. Tusitoe ushauri ambao hauwezekani. Hapo zamani kadiri ya hadithi za Aesop panya walikuwa na mkutano namna ya kumkwepa paka. Panya mmoja akatoa wazo kuwa tumfunge kengele shingoni paka akikaribia tutajua kuwa anakaribia. Panya huyo mdogo kwa umri alipigiwa makofi nakushangiliwa. Panya mkubwa akauliza. “Hilo ni wazo zuri lakini nani atamfunga paka kengele?”  “Inawezekana tatizo la paka kwa panya lingekwisha kama paka angefungwa kengele. Taabu ni kumpata panya wa kuifanya kazi hiyo. Na panya watakuwa wajinga sana kama watadhani kuwa paka watajifunga wenyewe kengele shingoni,” alisema Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliyekuwa rais wa kwanza wa Tanzania.

Ukarimu uonekane katika kurudisha wema. Ukitendewa wema rudisha wema hili kama au mnyororo wa wema usikatike. Mtu akiokota kitu chako akakuletea mpe zawadi. Mwanamke mmoja alipoteza begi lake wakati ananua vitu vya Krismasi. Mvulana mdogo mwaminifu aliokota begi hilo na kumrudishia mwanamke huyo. Alipotazama kwenye mfuko wake alisema: Kuna jambo la kushangaza katika begi langu palikuwepo noti moja ya shilingi elfu moja ya Kenya sasa nakuta noti 20 za shilingi hamsini hamsini.” Mtoto huyo alijibu haraka. Hiyo ni kweli. Niliwahi kuokota begi la mwanamke mwingine lakini hakuwa na pesa ndogo ndogo ya kunipa zawadi kama shukrani hivyo nimeamua kupata fedha ndogo ndogo wewe utaamua unanipa kiasi gani.  “Krismasi ni kufanya jambo la ziada kwa ajili ya mwingine,” alisema  Charles M. Schulz

Krismasi sio kipindi cha kuwaibia wengine ni kipindi cha kuwapatia wengine. Jaji aliyewatembelea wafungwa siku ya Krismasi alimuuliza mfungwa: wewe ulifanya kosa gani? Mfungwa alisema Nilifanya manunuzi ya vitu vya Krismasi mapema sana?” Jaji alisema hilo sio kosa. Lakini mapema ya saa ngapi ulifanya manunuzi hayo?” Mwizi huyo alisema: “Kabla duka alijafunguliwa. Huyu alidokoa. Huyu aliiba.

“Krismasi ni kipindi cha kuwasha moto wa ukarimu katika ukumbi, na miale ya joto la ukarimu moyoni,” alisema Washington Irving.  Wanafamilia wape muda wako. Muda ni mali. Kuwa nao. Siku hizi muda wa baba na mama kukaa na watoto wao ni mdogo. Wanakuwa shuleni. Wakienda likizo za Krismasi wanawekewa mwalimu wa kuwafundisha. Wape muda watoto wako. Krismasi sio kipindi cha kutapanya hovyo. Wengine wanatapanya hovyo mpaka wanatumia karo za watoto wao. Krismasi sio mwisho wa maisha kuna kesho.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Counter

You are visitor since April'08