Saturday, July 1, 2017

MSALABA UNABEBEKA




Jumapili ya 13

 “asiyepokea msalaba wake akanitafuta, hafai kwangu.”(Mathayo 10:38)
“Msalaba unamaanisha hakuna maangamizi ya meli baharini bila matumaini; hakuna giza bila mapambazuko; hakuna dhoruba bila bandari,” alisema Papa Mt.Yohane  Paulo II. “Kwa kuchukua msalaba, haimaanishi kitu kingine chochote zaidi ya kwamba tunapaswa kupokea na kuteseka kwa sababu ya  maumivu, mambo yanayopingana, mateso na kujikatalia tunavyopitia,” alisema Mtakatifu Francis wa Sales. Inabidi tubebe misalaba yetu badala ya kuiongelea tu. Tarehe 25 Oktoba 1970 Papa Paul VI aliwatangaza  watakatifu mashahidi40 wa Kiingereza. Alexander Briant alijitengenezea kimsalaba kidogo wakati wa kufungwa kwake jela na siku ya kuuwawa kwake alikishikilia mikononi mwake wakati wa hukumu ya kifo inatolewa.Walimyanganya kimsalaba chake, lakini alimwambia jaji: “Unaweza kukichukua toka mikononi mwangu na  si kutoka  moyoni mwangu.”  Msalaba juu ya Golgotha ​​hauwezi kukubadilisha wewe kama si haukusimikwa moyoni mwako. 

Msalaba ni mzigo lakini unabebeka kwa vile ni mzigo mwepesi. “Ukiubeba msalaba ipasvyo, msalaba utakubeba,” alisema Thomas à Kempis. Watoto ni misalaba lakini wanabebeka. Mzazi akiwabeba vyema nao baadaye watoto watambeba, akiisha zeeka hana nguvu watamtunza kama aliwaandalia vizuri maisha ya kesho. Kuna mtoto wa miaka kumi na miwili alikuwa amembeba mdogo wake wa mwaka mmoja. Alipoulizwa na jirani kama ni mzito. Mtoto alijibu, “Si mzito kwa vile ni ndugu yangu.” Siku moja rafiki wa baba aliyekuwa na watoto wanne alimuuliza, “Kwa nini unawapenda watoto wako?” Baba huyo alifikiria kwa dakika  na kupata jibu moja ambalo angelitumia, “Kwa sababu ni wangu.”  Watoto wanapendwa na wanapendeka. Wanabebeka kwa vile wanapendwa. Nao watoto wanawajibu kama isemavyo, ukibebwa bebeka.

Yesu alisema, “Mtu akitaka kuwa mfuasi wangu, ajikane mwenyewe, lazima ajitwike msalaba wake kila siku, anifuate” (Luka 9: 23). “Msalaba unabebwa kwa namna mbili: mwili kwa kujinyima na moyo unapoguswa na huruma” alisema Mtakatifu Gregori. Mzazi anajinyima mambo mazuri ya mwili kama kujipamba, mafuta, chakula kizuri, sehemu nzuri ya kukaa ili mtoto wake asome shule kwa namna hiyo anaubeba msalaba. Mzazi akifikiria maisha ya mbele anawaonea watoto wake huruma aubeba msalaba.  Mungu hakupi msalaba wa kubeba unaozidi uwezo wako. “Msalaba Mungu anaokutumia ameutathimini kwa macho yake yanayojua yote, ameuelewa kwa akili yake ya kimungu, ameujaribu na haki yake yenye hekima, umeupa joto kwa mikono yake ya upendo, ameupima kwa mikono yake kujua kuwa haupitilizi ukubwa hata kwa inchi moja na haupitilizi uzito hata kwa ratili moja, “ alisema Mtakatifu Francis de Sales. Wajibu ni msalaba lakini unabebeka: wajibu wako kwa umma, kwa familia, kwa Mungu na kwako wewe ni msalaba lakini unabebeka.

Msalaba unabebwa kila siku.  Lakini si kila siku ni kila saa. “Na sisi, kwa nini tumo hatarini kila saa? Siku kwa siku nipo taabani” (1 Wakorintho 15:30-31). Inavyoonekana ni jambo gumu kufa kila siku kuliko kufa mara moja. Ina maana kila mara unatoa sadaka ya kitu fulani iwe hata muda wako kwa ajili ya wengine. Mfanyakazi ofisini anabeba msalaba wake wa kazi kila saa. Anaporudi nyumbani kama ana wazazi wa kuwatimizia aja zao anafanya hivyo, kama ana mwenzi wa ndoa anamjali, kama ana watoto anasikiliza shida zao. Ni kila siku karibu ni kila saa kuubeba msalaba.

Sala: Ee Bwana wetu Yesu Kristo nisaidie ili hamasa na nguvu zangu vitoke kwenye kujikatalia na msalaba. Amina.

Counter

You are visitor since April'08