Saturday, November 11, 2017

KUTOJIANDAA NI KUJIANDAA KUSHINDWA




                                                    
                         “Basi, kesheni, kwa sababu hamjui siku wala saa” (Mathayo 25: 13) jmggyt
  1. Hek 6: 12-16
  1. 1 Thes 4: 13-18
  1. Mt 25: 1-13

UTANGULIZI
Mafuta: Yanaweza kuwa na tafsiri nyingi. “Busara ni kama ufuta; unaukaanga kadiri unavyokula” (Methali ya Batoro, Uganda). Taa zetu hazina budi kuwa na mafuta. Mafuta ni busara. Kujiandaa ni busara. Pia mafuta yanaweza kueleweka kama upendo hai. Ndio huo unaoleta tofauti baina ya wanawali wapumbavu na wenye busara. Kadiri ya Mt. Augustino, “Mafuta yanamaanisha furaha.”  Kufuatana na ukweli huo, “Mungu wako, amekupaka mafuta, kwa mafuta ya furaha, kuliko wenzako” (Zaburi 45:8). Mafuta kuwekwa kwenye vyombo ni furaha iliyotunzwa moyoni na kwenye dhamiri.
Taa: Taa inaweza kuwa na tafsiri nyingi. Taa ni imani. Taa ni matendo mema. tKadiri ya Baba wa Kanisa Mt. Augustino:  “Taa wanazobeba mikononi ni matendo yao ambapo ilisemwa, ‘mwanga wenu uangaze mbele ya watu.’” (Mt 5:6).
Mabikira: Wanaojiandaa wanalinganishwa na mabikira watano wenye busara na wale ambao hawajiandai wanalinganishwa na mabikira wapumbavu.
Bwana harusi: Ni Yesu. Yesu anakuja namna mbili. Anapomchukua mtu mmoja. Namna ya pili atakapokuja kuwahukumu wazima na wafu. Hakuna anayemjua mjumbe wa kifo atakuja lini. Ni busara kila tufanyalo katika maisha tujiulize, “Halafu?” Kama hadithi ya vijana wawili. Kijana mmoja alimuuliza mwingine. “Utafanya nini ukikua?” “Nitachukua somo la biashara.” “Halafu?” “Nitatafuta kazi.” “Halafu?” “Nitapata fedha nyingi kama mshahara.” “Halafu?” “Nitatafuta msichana nioe” “Halafu?” “Nitakuwa na watoto.” “Halafu?” “Nitawalea watoto” “Halafu?” “Nitakuwa babu?” “Halafu?” “Labda nitafanywa chifu.” “Halafu?” “Nitatawala watu.” “Halafu?” “Nitazeeka.” “Halafu?” ““Halafu?”, halafu, halafu, halafu usiulize zaidi ya hapo.” “Bila shaka uwe unafikiria kuwa siku moja utakufa.” Lakini tumaini linabaki kuwa kifo sio nukta, sio kikomo, bali ni alama ya mkato hadithi ya maisha inaendelea. Kutojiandaa ni kujiandaa Kutokuwa katika wateule. Jiandae.
MAHUBIRI YENYEWE
 “Ukinipa saa sita ili niukate mti, nitatumia saa nne za awali kulinoa shoka langu,” alisema  Abrahamu Lincoln (1809-1865). Hiyo ni busara. Hayo ni mafuta katika taa. Somo la meneno hayo ya Abrahamu ni kuwa kujiandaa kunatangulia mafanikio. Kwa kushindwa kujiandaa, unajiandaa kushindwa. Kuna mambo ambayo yanawafanya watu wasijiandae.
Kwanza ni kuwa katika eneo la faraja. Ili ni eneo ambapo watu wanajiona wako salama, wamefarijika. Hawataki kujisumbua. Kazi ya kweli ya kupigia debe ufalme wa mbinguni au maendeleo ni kuwasumbua waliofarijika na kuwafariji waliosumbuka. Lazima kutoka katika eneo la faraja ambalo linakufanya usifanye lolote la maana na kujiandaa.  Ili kuleta mabadiliko ni lazima kuvunja uzio na ukuta wa eneo la faraja inayokufanya kubweteka. Toka ndani ya sanduku. “Faraja ni mtego wako mkubwa na kutoka katika eneo la faraja ni changamoto yako kubwa,” alisema Manoj Arora. Katika Biblia tuna watu waliovunja ukuta wa eneo la faraja ni Musa: “ Kwa nguvu ya imani, Musa alipofikia utu uzima, alikataa kuitwa mwana wa binti Farao” (Waebrania 11: 24). Musa alikuwa kwenye eneo la faraja la kuitwa mwana wa binti Farao. Mambo mawili yalimfanya  kuacha eneo la faraja: nayo ni nguvu ya imani na utu uzima.
Kuna nguvu ya imani. Katika kitabu cha maombi tunasali hivi: “Iliwalazimu wanawali kuwa na taa, yaani, imani: Utuangaze kutumia imani kama taa ya njia ya kweli katika maisha yetu ya kila siku.” Musa alitumia imani kama taa nasi tutumie imani kama taa.
Kuna utu uzima. Wanawali wapumbavu hawakutenda kama watu wazima. Kuna mwanaume alimuuliza mke wake utaweza kweli kwenda Dubai kuchukua mzigo wa biashara bila kusumbuliwa na wanaume huko? Mwanamke alimjibu mume wake: “Mimi ni mtu mzima.” Kuna kijana ambaye alihama kwa kaka yake akaanza kupanga nyumba. Kaka yake alimuuliza utaweza kuyamudu maisha. Alimjibu: “Mimi ni mtu mzima.” Ni utu uzima    ambao unakufanya kung’amua kuwa: mtegemea cha nduguye hufa akiwa maskini. Kuna kijana alikuwa anaenda kuanza masomo chuo kikuu, mzazi akamwambia tusindikize hadi Dodoma. Alimjibu mzazi: “Mimi ni mtu mzima. Hakuna haja ya kunisindikiza.” Mfalme alikuwa na mtumishi ambaye alimdharau na kumuona kama mtoto. Siku moja alimpatia fimbo akasema ukimuona mtu mzima ambaye hajiandai jua ni kama mtoto mpe fimbo hii. Mtumishi alizunguka hakumpata mtu wa namna hiyo. Siku moja alisikia mfalme yupo kitandani anaumwa sana kiasi cha kuchungulia kaburi. Alienda na kumuuliza: ukifa huko unakokwenda umeishajitengenezea marafiki? Mfalme alisema: “Hapana.” Mtumishi alimpa fimbo na kumwambia: “Wewe sio mtu mzima.”  

Jambo la pili  linalotufanya tusijiandae ni kusitasita. Kuna mtu ambaye alisema: “Kusitasita ni chanzo cha matatizo yangu yote. Hata hivyo sijui vizuri maana ya neno kusitasita kesho nitatazama maana yake kwenye kamusi.” Kutojiandaa ni kujiandaa kushindwa. Ngoja ngoja huumiza tumbo. Asubuhi ni wakati wa kuweka kipimo cha kasi utakayotumia. Kuna nguvu ya kufanya mambo mapema. Kuna mtu aliyeambiwa kuna ng’ombe dume watatu kwenye zizi, ukiweza kukamata mkia wa mmojawapo utapewa zawadi ya milioni mbili. Ng’ombe wa kwanza kujitokeza alikuwa mkali, macho makali, mnene na wa kutisha. Mtu huyo akaogopa kushika mkia wake. Wa pili kujitokeza alikuwa mkali zaidi na wa kutisha zaidi. Mtu huyo akangoja wa tatu. Wa tatu alikuwa amekonda, hana nguvu. Mtu huyo akasema nitashika mkia wa huyo. Bahati mbaya hakuwa na mkia. Alishindwa kufanya mambo mapema. Adui ya nguvu ya mapema ni kusitasita.
Jambo la tatu ambalo linatufanya tusijiandae ni mazoea mabaya. Kuna methali ya Tanzania isemayo, “Huwa nazaa watoto namna hii, aliuawa na mimba ya tisa.” Mazoea yanaweza kupofusha macho yetu, na kutufanya viziwi. Ukimtia chura kwenye maji moto ataruka ili atoke. Lakini ukimtia kwenye maji baridi na kupasha joto pole pole. Chura hatajua ni lini maji yamekuwa ya moto. Mazoea yanamfanya mtu hasishtuke.  Mazoe ya kutenda mema yatakusaidia.
Jambo la nne  linalotufanya tusijiandae ni inesha au ubaridi  au kingungumizi cha kuanza. “Watu wengi hushindwa kwa sababu hawaanzi. Hawaishindi inesha. Hawaanzi,” alisema Ben Stein. Jiulize umefikaje ulipo: kwa kuelea au kwa kupiga makasia. Kama ni kwa kuelea utakuwa hauna mwelekeo na dira. Kama kwa kupiga makasia ina maana unafanya kitu fulani. Palipo na inesha kuna kushindwa kuonesha hisia kali au shauku. Hakuna bashasha. Inesha ni kutofanya lolote. Kuna hadithi ya fisi aliyetoa kipande cha nyama kwenye sufuria. Kilikuwa ni cha moto. Kilimchoma midomo. Fisi wenzake wakamwambia, “Tema.” Akawajibu. “Niteme utamu.” Wakazidi kumshauri, “Meza.” Akawajibu, “Nimeze moto.” Huu ni ubaridi unaoletwa na kukosa uamuzi.
Kujiandaa ni kujiandaa kushinda. Mwanamke mmoja alikuwa akifanya kazi katika kiwanda cha kusindika nyama. Siku moja baada ya kumaliza kazi zake pale kiwandani alienda katika chumba chenye freezer (cold room) ambako nyama zilikuwa zikihifadhiwa kukagua baadhi ya bidhaa.​ Kwa bahati mbaya wakati yupo kwenye hicho chumba katika harakati za hapa na pale akausukuma mlango, ukajifunga. Hakukuwa na msaada wowote wa kuweza kuufungua mlango ule. Alianza kulia na kupiga kelele za kuomba msaada wa kufungiliwa, lakini kelele zake hazikuwa rahisi kusikika nje ya hicho chumba kidogo, na wafanyakazi wote pale kiwandani walikuwa wameishaondoka. ​Masaa mawili baadae akiwa katika hali ya kukaribia kukata roho kutokana na baridi kali iliyoko kwenye hicho chumba. ​Ghafla mlinzi wa geti la kiwanda hicho alifungua mlango alimokuwamo yule mwanamke.​ Alitahamaki kumkuta mwanamke yule katika hali ile mbaya.
Basi jitihada za kumpa huduma ya kwanza kumpeleka hospitali ikafuata. Baada ya kutolewa hospitalini alipata wasaa wa kumuuliza yule mlinzi ilikuwaje akafungua mlango wa cold room wakati ilikuwa si ratiba yake na vile vile ilikua si kazi yake? Maelezo ya yule mlinzi yakawa kama ifuatavyo:
​''Nimefanya kazi kwenye hiki kiwanda kwa miaka 38 sasa, mamia ya wafanyakazi wanatoka na kuingia kiwandani lakini wewe peke yako kati ya wote ndiye uliyekuwa ukithubutu kunisalimia asubuhi na kuniaga kila jioni unapoondoka kiwandani. Ulipokuja kazini asubuhi ulinisalimia kama kawaida na kunijulia hali. Lakini baada ya kazi na wafanyakazi kuanza kutoka kurudi, nilitegemea kusikia salamu yako, niliendelea kusubiri lakini cha ajabu mpaka watu wote wakawa wametoka na wewe sikuona sura yako. Nilianza kuingiwa na maswali mengi, na ndipo nikapata wazo la kuanza kuzunguka maeneo yote ya kiwanda na baadae chumba baada ya chumba. Na ndipo nilipokukuta kwenye chumba cha barafu.​ Funzo ni kuwa tenda mema kuna kesho. Ishi vizuri na kila mtu, mheshimu kila mtu bila kujali hadhi yake, ukubwa wala udogo wake, kwani hujui kesho atakua wapi katika kuwa sababu ya MSAADA kwako.
HITIMISHO: Maisha ya kikristo yanadai kazi, kuwa macho na kuwa tayari.

Counter

You are visitor since April'08