Saturday, June 21, 2014

SHUKURU USIKUFURU



                                              
SHEREHE YA MWILI NA DAMU TAKATIFU YA BWANA WETU YESU KRISTU
1. Kumb. 8: 2-3, 14-16
2. 1 Wakorintho 10: 16-17
3. Yn 6: 51 – 58

Ingawa tuna mioyo midogo lakini inaweza kubeba jambo kubwa nalo ni shukrani. “Tunapotoa kwa furaha na kupokea kwa shukrani, kila mtu anabarikiwa,” alisema Maya Angelou.  Kuna methali isemayo, “Hasiyeshukuru kwa jambo dago apewalo hatashukuru kwa jambo kubwa.” Leo hii wakatoliki sehemu zote duniani wanaandamana kusherehekea sherehe inayojulikana kama “Mwili na Damu ya Kristu.” Kwa jina lingine sherehe hii inajulikana kama “Sherehe ya Ekaristi Takatifu.” Neno “Ekaristi” linatokana na neno la Kigiriki ambalo linamaanisha shukrani. Ni sherehe inayohusu kumshukuru Mungu na utamaduni wa kushukuru. Kushukuru ni kitovu cha sherehe hii. Shukuru kwa kila jambo. Sherehe ya Leo ya wakatoliki inahusu utamaduni wa kushukuru. Waluhya wana methali isemayo, “Nyama choma haiwezi kuwa tamu ukamsahau aliyeichoma.” Methali hii inakazia kuwa na utamaduni wa kushukuru. Kama umepewa sio siri. Watu wanaona jinsi Mungu alivyokubariki na hivyo kwa mantiki hii wakatoliki wanaandamana hadharani kuonyesha shukrani yao
 Sherehe hii inapata nguvu kutoka katika maneno ya Biblia, “ Ndipo Wayahudi wakaanza kubishana kati yao: “Anawezaje huyu kutupa mwili wake, tule?’ Yesu akaambia, ‘Kweli nawaambieni, msipokula mwili wa mwana wa Mtu na kunywa damu yake, hamtakuwa na uhai ndani yenu.” (Yohane 6: 52-53) Jambo hili la kula mwili na kunywa damu ya Yesu lilizua utata mkubwa katika historia ya Kanisa Katoliki. Mwanzoni wakristu walishitakiwa kuwa ni watu wala watu. Ni kama Wayahudi waliojiuliza, “anawezaje huyu kutupa mwili wake?”
 Jambo hili linaeleweka hivi. Kama maji na madini yangekuwa na uwezo wa kusema yangeiambia mimea usipokunywa maji na kula madini hamtakuwa na uhai ndani yenu. Kama nyasi na maji vingekuwa na uwezo wa kusema vingewaambia wanyama kama ng’ombe na mbuzi msipokula majani na kunywa maji hamna uhai ndani yenu. Katika msingi huu kwa vile binadamu ana mwili na roho Yesu alisema msipokula mwili wangu na kunywa damu yangu hamtakuwa na uhai ndani yenu.  Kushiriki katika karamu ya Bwana ni muhimu.
Leo hii tunapewa changamoto ya kushiriki. Katika neno kushiriki tunapata neno ushirikiano. “Tunapomshukuru Mungu kwa kiokombe kile cha baraka, je, huwa hatushiriki damu ya Kristo? Na tunapoumega mkate, je, huwa hatushiriki mwili wa Kristo? Kwa kuwa mkate huo ni mmoja, sisi, ingawa ni wengi, tu mwili mmoja; maana sote twashiriki mkate huohuo.” (1 Wakorintho 10: 16-17) Basi kushiriki kwetu kusiishie Kanisani tushiriki katika Jumuiya Ndogo Ndogo. Tushiriki katika maendeleo ya Taifa.
Suala la sherehe ya leo na shukrani lina msingi wake katika Biblia. “Saa ilipotimia, Yesu akakaa kula chakula pamoja na mitume wake…Kisha akatwaa kikombe akashukuru, akasema, ‘Pokeeni, mgawanyiane…halafu akatwaa mkate, akashukuru, akaumega, akawapa akisema, “Huu ni mwili wangu unaotolewa kwa ajili yenu. Fanyeni hivi kwa kunikumbuka.” (Luka 22: 14-19) Yesu alishukuru alipochukua mkate na divai. Ekaristi inamaanisha shukrani na mkate na divai hutumika. Wakristu ambao wanashiriki kumbukumbu ya Karamu ya Mwisho ya Yesu kwa kuandamana leo wanakumbushwa kuwa na utamaduni wa kushukuru maana ndio kiini cha sherehe ya leo.
Hellen Keller ambaye alikuwa kipofu na kiziwi aliandika hivi: “Kila mara nimefikiria ingekuwa baraka kama kila mtu angekuwa kipofu na kiziwi kwa siku chache wakati wa siku zake za kwanza za utu uzima. Giza lingemfanya akiri uzuri wa mwanga; ukimya ungemfundisha furaha ya sauti.”  Kuna vitu ambavyo tunavyo lakini hatukiri uzuri wake na umuhimu wake mpaka tumevipoteza. “Hatuna budi kupata muda wa kutulia na kushukuru watu ambao wameleta tofauti katika maisha yetu,” alisema John F. Kennedy.
 Katika hadithi  za Aesop kuna hadithi juu ya mtumwa aliyeitwa Androcles ambaye alitoroka toka kwa Bwana wake na kukimbilia msituni. Alipokuwa akitangatanga alikutana na simba ambaye alikuwa amelala chini akinguruma na kutoa sauti ya uchungu. Mwanzoni alitaka kukimbia lakini aligundua simba hakumfukuzia. Alirudi nyuma na kumwendea. Alipomkaribia, simba alionyesha kwato zake au mguu wake ambao ulikuwa umevimba na ukitoa damu. Androcles aligundua palikuwepo na mwiba mkubwa ambao ulikuwa umeingia ndani na ulikuwa unamsababishia maumivu makali. Aliutoa mwiba huo na kuufunga vizuri mguu wa simba ambaye aliweza kusimama na kulambalamba mkono wa Androcles kama mbwa. Simba alimpeleke Androcles kwenye pango lake na kila siku alimletea nyama ya kula na kuweza kuishi. Lakini baadaye Androcles na Simba walikamatwa. Androcles alipewa adhabu ya kutupwa kwenye kibanda cha simba huyo ambaye siku nyingi aliwekwa kwenye kibanda bila chakula. Mfalme na watu wa ikulu ya mfalme walikuja kushuhudia simba akimrarua Androcles. Simba aliachiliwa kutoka katika kibanda chake na kumwendea huyo binadamu akinguruma. Alipomkaribia Androcles alimtambua na kuanza kulamba lamba mikono yake kama mbwa rafiki. Mfalme alishangaa alimuomba Androcles amueleze maana ya hayo yote. Androcles alimweleza mfalme kila kitu. Mtumwa alisamehewa na kuachwa huru  na simba aliachiliwa arudi msituni. Hayo ni matunda ya kutenda wema kwa Androcles na kushukuru kwa simba. Shukrani ni mtaji. Shukrani ina malipo.

Hata unapokosewa unajifunza kitu fulani. “Msamaha wa kweli ni pale unapoweza kusema, ‘Nashukuru wa uzoefu huo,’” alisema Oprah Winfret. Biblia inatwaambia: “Shukuruni katika kila jambo; maana hayo ni mapenzi ya Mungu kwenu katika Kristo Yesu” (1 Wathesalonike 5: 18). Rick Warren katika kitabu chake Maisha Yanayoongozwa na Malengo alikuwa na haya ya kusema juu ya haya hiyo: “Mungu anakutaka umshukuru kwamba atatumia matatizo yako kutimiza malengo yake.” Kusema kweli kutomthamini mwenzako ni kukufuru maana kushukuru ni kuthamini. Kutoshukuru ni kosa kubwa kuzidi kulipa kisasi. “Kutoshukuru ni kosa la kudharauliwa zaidi ya kulipa kisasi, ambacho ni kulipa baya kwa baya, wakati kutoshukuru ni kulipa baya kwa wema,” alisema William Jordan. Tujenge utamaduni wa kushukuru. Afrika yenye utamaduni wa kushukuru inawezekana.
Kushukuru ni kumsifu Mungu. Mungu kama amekujalia watoto, akili, utajiri, amani moyoni, jina jema, mke, mme, mshukuru ukimsifu. Zingatia maneno haya, “Mtukuzeni Bwana  pamoja nami, na tuliadhimishe jina lake pomoja .” (Zaburi 34:3) Mkumbuke Mungu. Hakuna haja ya kujidai sana sote ni “CHAKUPEWA.” “Nani amekupendelea wewe? Una kitu gani wewe ambacho hukupewa? Na ikiwa umepewa, ya nini kujivunia kana kwamba hukupewa?” (1 Wakorintho 4:7).   Kuna methali isemayo, “Aliyekupa wewe kiti ndiye aliyenipa mimi kumbi.” Na aliye na kidogo akitumie kupata kikubwa.
Kushukuru ni kuthamini zawadi uliyopewa. Kama Mungu ametupa zawadi ya amani, kushukuru ni kuthamini zawadi hiyo. Kama Mungu amekupa zawadi ya mke, shukuru ni kuthamini zawadi hiyo. Kama Mungu amekupa zawadi ya mme, shukuru ni kuthamini zawadi  yaani mme. Kama unamshukuru Mungu kwa kuwa Mkenya, basi itendee Kenya mambo mazuri. Kama unamshukuru Mungu kwa vile wewe ni mtanzania itendee Tanzania mambo mazuri.
Kushukuru ni kuomba tena. Ukipata shukuru. Kuna Baba mmoja ambaye alikuwa anatembea kando ya Bahari ya Indi na mtoto wake wa kiume. Mara wimbi likamchukua mtoto wake wa kiume lakini akaokolewa na mvuvi Msamaria mwema. Badala ya kushukuru Baba huyo alimuuliza mvuvi, “Mtoto wangu alikuwa na kofia umeiweka wapi?” Huo ni ukosefu wa shukrani. Sherehe ya Ekaristi ambayo inamaanisha shukrani ni changamoto kwa wakristu wote kuwa na moyo wa shukrani na sio na moyo wa punda. Shukrani ya punda ni mateke.


Counter

You are visitor since April'08