Saturday, June 14, 2014

MAFIGA MAWILI HAYAIVISHI CHUNGU



                                                 
                                                         SHEREHE YA UTATU MTAKATIFU
1.       Kut 34: 4b -6. 8-9
2. 2 Kor 13: 11 -13
3.  Yn 3: 16 -18

Mungu wetu ni mkubwa. Yuko katika nafsi tatu: Baba Mwana na Roho Mtakatifu. Ana nguvu. Nakubaliana na Andrew Guzalds aliyesema: “Kuna nguvu zaidi katika neno moja kutoka kwa Mungu kuliko maneno yote ya adui yakiwekwa pamoja.” Ukiwa na Mungu huko upande wa wengi. Sala yako iwe hii: “Nakuomba ee Bwana wangu, ufuatane nasi” (Kutoka 34:9). Tafakari hadithi hii: Binti alimuaga mama yake, “naenda matembezi na marafiki zangu.” Mama yake akamwambia: “Mungu awe nawe katika Safari yako.” Kwa dharau na kiburi binti akajibu “mh mama gari imejaa labda huyo Mungu akae kwenye buti kama anaweza. Kwa kasi akawasha gari wakaondoka. Njiani wakapata ajali mbaya wote wakafa walitambuliwa tu kwa mavazi waliyovaa! Polisi walipofungua buti wakakuta mayai trey 2 yakiwa salama kabisa! Unajua kwa nini? Wewe Mungu umemweka wapi?
Kuna methali ya Wahaya wa Bukoba isemayo: “Fanya urafiki na mkubwa anamaliza kabisa tatizo la kukosa kitoweo.” Mungu mmoja katika nafsi tatu ni mkubwa fanya urafiki naye. “Kuna utupu au ombwe lenye sura ya Mungu katika kila mtu ambalo linaweza kujazwa na Mungu,” alisema Blaise Pascal.
Mungu wetu Mkubwa hata siku moja usimwambie kuwa dhoruba yako ni kubwa, tatizo lako ni kubwa bali iambie dhoruba: Mungu wangu ni mkubwa ni nafsi tatu, Mungu mmoja. Ukiwa na imani kwa Mungu mmoja nafsi tatu, utaiondoa milima. Lakini ukiwa na hofu milima itakuondoa. Uwe mwondoaji wa milima kwa kuamini katika Utatu Mtakatifu na kwa kusali hivi: “Nakuomba ee Bwana wangu, ufuatane nasi” (Kutoka 34:9).
Mafiga mawili hayaivishi chungu.Ni methali ya Kiswahili. Mafiga mawili hayawezi kukiivisha chungu; lazima yawe matatu. Tutakapo kufanikiwa lazima tuwe tayari kushirikiana na wenzentu.  Katika mtazamo huu wazee wetu walituachia busara: kidole kimoja hakivunji chawa. Jiwe moja haliinjiki chungu. Kuna kitendawili cha Wafipa wa Tanzania kisemacho: Tatu tatu mpaka Ulaya. Jibu ni mafiga. Haya ni mawe matatu. Ndoa inahitaji watatu: mme, mke na Mungu. Kwa kumuungiza Mungu kwenye ndoa, ndoa inadumu. Ni katika msingi huu tunasema: Familia inayosali pamoja hudumu pamoja. Umoja huu wa Utatu ni muhimu.  “Kwa kuungana tunasimama; kwa kugawanyika tunaanguka,” alisema John Dickson. Tafakari methali ya Tanzania isemayo: Mkono mmoja haulimi shamba.
Siku zilizopita nilipokea ujumbe katika simu wenye maneno haya: “Kuna siri gani katika namba 3? Shetani alimjaribu Yesu mara 3. Yesu alianguka na msalaba mara 3. Petro alimkana Bwana Yesu mara 3. Jogoo aliwika mara 3. Yesu alifufuka si ku ya 3. Wanawake walienda kaburini siku ya 3 nao walikuwa 3. Matanga huanuliwa siku ya 3. Mafiga ya kupikia huwa 3. Mashindanoni namba za ushindi ni 3. Nyakati zinagawanyika mara 3: wakati uliopita, uliopo na ujao. Wazo, neno na tendo vinakamilisha uwezo wa binadamu navyo ni vitatu. Kuna nafsi 3 katika sarufi: Mimi, Wewe na Yeye. Nafsi za Mungu ni 3: Baba, Mwana na Roho Mtakatifu. Nini maana ya 3? Namba tatu ni namba ya ukamilifu na utimilifu. Namba tatu inawakilisha kitu kizima, cha kweli na kamilifu. Inadokeza uimara, uthabiti, uhakika.
Jumapili ya leo wakatoliki kote duniani wanasherehekea Sherehe ya Utatu Mtakatifu. Inahusu imani kuwa Mungu ni mmoja katika nafsi tatu: Baba, Mwana na Roho Mtakatifu. Ni kama mafiga matatu. Wakatoliki hubatizwa kwa jina la Baba, na la Mwana na la Roho Mtakatifu na wala sio kwa majina ya Baba na Mwana na Roho Mtakatifu. Hapa hakuna suala la hesabu za kujumlisha ambapo moja kujumlisha na moja kujumlisha na mojo ni tatu. Ikumbukwe kuwa moja kuzidisha na moja kuzidisha na moja  ni moja. Hapa hatuingizi hoja ya mahesabu. Ieleweke hivi mimi ukisoma makala yangu kwenye gazeti unaniita mwandishi wa makala maalum (columnist), kanisani waumini wananiita padre, chuoni wanafunzi wananiita mwadhiri. Hatuko watatu ni mmoja.
Katika kufanikisha mambo kuna nguvu ya wingi au nguvu ya namba. Tunaona nguvu ya wingi katika uumbaji. “Mungu akasema: Tumfanye mtu kwa mfano wetu, afanane nasi” (Mwanzo 1:26). Ni Utatu  Mtakatifu uliosema “tumfanye mtu,” katika kitabu cha Mwanzo. Inavyoonekana hata mwanzoni mwa Injili Utatu Mtakatifu ulisema, “tumkumboe mtu.” Ili kufanikisha mambo. Ili kufanikiwa lazima kufikiria katika msingi wa “sisi.”  Nafsi tatu zinafikiria katika msingi wa sisi. Nakubaliana na Ralph Chaplain Yusufu aliyesema: “Hauwezi ukawa na usalama, hata ukijaribu namna gani; kama haufikiri kwa msingi wa “sisi” badala ya mimi.” Lorii Myers alikuwa na mawazi hayo aliposema: “Sisi ni sawa na nguvu.”
Kutatua tatizo la kutozaa la Abrahamu na Sara palikuwepo na nguvu ya namba au nguvu ya umoja. “Mgeni akamwambia, ‘Nitarudi kwako mwaka ujao, wakati huu; na hapo mkeo Sara atakuwa na mtoto wa kiume” (18: 10). Sara na Abrahamu walikuwa wamezeeka lakini kwa Mungu hakuna lisilowezekana. Abrahamu alitembelewa na utatu mtakatifu. Tafakari vizuri haya hizi: “Bwana akamtokea Abrahamu” (Mwanzo 18: 1); “Akainua macho akaona watu watatu wamesimama mbele yake” (Mwanzo 18:2). Ni Bwana mmoja halafu watu watatu. Kutatuliwa tatizo la kutozaa ni ufunuo wa uwepo wa Mungu katika nafsi tatu. Tunahitaji nguvu ya Utatu Mtakatifu tufanikiwe ambayo inaelezwa katika somo la pili: “Neema ya Bwana Yesu Kristo, na upendo wa Mungu Baba, na Ushirika wa Roho Mtakatifu viwe nanyi nyote” (2 Kor 13:13).

NEEMA YA BWANA YESU KRISTU
Mt. Gregory wa akizungumzia juu ya ubatizo alisema ni: “Neema: kwani hutolewa hata kwa wahalifu.” Ukweli kuwa neema hutolewa hata kwa waalifu ni ukweli ambao tunauona msalabani. Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo ilitolewa kwa mwizi Dismasi. Tunahitaji neema ili kufanikiwa. George W. Bush aliwahi kusema: “Naamini katika neema, kwa sababu nimeiona; katika amani kwa sababu nimeionja; katika msamaha, kwa sababu nimehuitaji.” Neema ya Bwana Yesu inaonjeka. Ili kuonja neema ya Bwana wetu Yesu lazima kushirikiana nayo. Kuna ambaye alitaka kushinda bahati nasibu ya Kampuni ya Simu ya Tigo. Kila mara aliomba kushinda. Alisali kwa Bwana wetu Yesu Kristu. Usiku alitokewa katika ndoto. Yesu alimwambia: nataka ushinde lakini nunua vocha. Alitaka naye atoe mchango wake. Ni lazima kushirikiana na neema ya Mungu.

UPENDO WA MUNGU BABA
Kilichojaa hufurika. Ni methali ya Watanzania. Mungu Baba amejaa upendo na unafurika. “Kwa maana  jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe wa pekee, ili kila mtu amsadikiye asipotee, bali awe na uzima wa milele (Yn 3:16). Martin Luther aliita haya hii: “Injili katika mfano mdogo.” Upendo wa Mungu unajieleza katika kumtuma Mwana wake wa Pekee. Kutoa ni matokeo ya upendo. Unaweza kupenda bila kutoa. Lakini hauwezi kupenda bila kutoa.
Hata katika matatizo kuna upendo wa Mungu. Methali ya Kiyiddishi inasema yote: “Yule ambaye Mungu anampenda anamwaadhibu.” Mateso yanaweza kuwa sehemu ya upendo wa Mungu. “Mungu alikuwa na Mwana mmoja bila dhambi, lakini hakuwa na yeyote bila mateso,” alisema Mt. Augustini. Kuna kijana mdogo ambaye alimuua bata wa baba yake. Mkubwa wa kijana huyo akasema: Chochote ninachotaka unifanyie utanifanyia, vinginevyo nitakushitaki kwa Baba kuwa uliua bata. Siku ilifuata kijana mkubwa alikuwa na zamu ya kuosha vyombo. Akamwambia mdogo aoshe vinginevyo alisema: nitakushitaki kuwa ulimuua bata. Alikuwa na zamu ya kuosha nguo akamwambia mdogo asipoosha nguo atamshitaki kwa baba yake.  Mambo yaliendelea hivyo mpaka mtoto mdogo alipoamua kwenda kuripoti kwa baba yake kuwa alimuua bata. Baba alimwambia nilikuona ulipofanya tendo hilo. Nilingoja uje kwangu usiwe mtumwa wa kaka yako. Niliishakusamehe. Huu ni mfano wa upendo wa Mungu Baba.
USHIRIKA WA ROHO MTAKATIFU
Kama hewa ilivyo kwa mwili wa binadamu ndivyo Roho Mtakatifu alivyo katika maisha ya kiroho. Roho Mtakatifu yupo nyuma ya pazia anafanya mambo. Anaunganisha pointi, matukio anapanga kalenda. Omba kuwa na ushirika naye. Tutumie mafiga haya matatu: Neema, Upendo na Ushirika.

HITIMISHO
Tunahuitaji Utatu Mtakatifu. Tuuiige. Tujifunze kufanya mambo kwa pamoja. “Sala usafiri kwa haraka tunaposali pamoja.” Ni methali ya Kilatini.

Counter

You are visitor since April'08