Saturday, July 12, 2014

MOYO WAKO UKOJE?

                                                          
                                                          JUMAPILI YA 15 MWAKA A

1. Isaya 55: 10-11
2.Warumi 8: 18-23
3. Mathayo 13: 1-23  (Mt 13: 1-9)

Ni moyo unaompelekea mtu mbinguni au motoni.” Ni methali ya Kiafrika.  Mungu hatazami sura ya nje anatazama yaliyomo moyoni. Mwenyezi Mungu alimkataa Eliabu hasiwe mfalme wa Israeli kwa vile Mungu hatazami sura ya nje, hatafuti warembo wa sura bali warembo wa moyo. Tunasoma katika Biblia, “Usiangalie sura yake na urefu wa kimo chake. Mimi nimemkataa kwani siangalii mambo kama wanavyoangalia binadamu wenye kufa. Binadamu huangalia uzuri wa nje, lakini mimi naangalia moyoni” ( 1 Samueli 16: 7). Katika Injili ya leo tunapewa aina nne za mioyo.

1.       MOYO WENYE TRAFIKI
Moyo wenye trafiki ni kama wapita njia ni wengi, magari ni mengi, baisikeli ni nyingi, boda boda ni nyingi. Katika Injili ya Mathayo tunaambiwa: “Mpanzi alikwenda kupanda mbegu. Katika kupanda, mbegu nyingine zilianguka kando ya njia. Wakaja ndege wa angani wakazidonoa” (Mathayo 13: 4). Moyo wetu ni kama njia. Kuna trafiki. Hoja si kuwepo kwa trafiki hoja ni namna ya kukabili trafiki. Trafiki isikuhumize kichwa. Mfano kwenye maisha ya ndoa ni kama msongamano wa magari ambapo hauchi nafasi kubwa ukiacha nafasi kubwa sana mwenye daladala anaingia. Ni bumper to bumper. Katika trafiki hiyo uenda kuna marafiki. Biblia yasema: “Msidanganyike! Urafiki mbaya huharibu tabia njema” (1 Wakorintho 15: 33).  Ni katika mtazamo huo inasemwa niambie rafiki yako nitakwambia tabia yako.  Kuna urafiki ambao unaunganishwa na jambo baya ukitoa jambo hilo baya hakuna urafiki. Wengine wanaunganishwa na ulevi, ukitoa ulevi hakuna urafiki. Wengine wanaunganishwa na umbeya, ukitoa umbeya hakuna urafiki. Urafiki wa kweli lazima uunganishwe na jambo zuri au na tabia nzuri.
Kuna watu wawili waliokuwa wanamjadili tajiri aliyefilisika. Mmoja akasema, “Tangia afilisike, nusu ya rafiki wake hawamtembeli tena, hawamjulii hali tena.” Mwingine akauliza habari juu ya nusu ya rafiki wake wengine. Mwenzake akamjibu: “Hawajui kama amefilisika.” Biblia yasema: “Kuna rafiki aliye mwenzi wa mezani, wala hatadumu karibu nawe siku ya taabu yako (Yoshua bin Sira 6:10). Rafiki katika taabu huyo ni rafiki wa kweli. Tusipokubali trafiki ituathiri mioyo itakuwa udongo mzuri. Simoni Petro alipotaka Bwana wetu Yesu Kristu aondokane na mpango wa kutukomboa Bwana Yesu alisema: “Ondoka kwangu” shetani.

2.       MOYO  WENYE MIAMBA AU MOYO MWAMBA
“Mbegu imeanguka kwenye mwamba” (Mathayo 13: 20). Mwamba haupenyeki. Ni moyo sugu. Dhamiiri imekufa. Mtu hayuko tayari kusamehe. Moyo unaweza kuwa mwamba kutoka na mabaya mtu aliyotendewa bila kusamehe. Mzee Joe alikuwa kufani kwenye kitanda cha mahuti. Kwa muda wa miaka mingi alikuwa hapatani na Bill, ambaye zamani alikuwa mmoja wa marafiki zake. Akitaka kunyosha mambo yake kabla ya kuaga dunia alimtuma Bill waongee na kumaliza mambo. Bill alipofika, Joe alimwambia kuwa anaogopa kwenda mbinguni akiwa na kinyongo naye. Kwa kusita na kwa kujikaza Joe aliomba msamaha kwa mambo aliyoyasema na kuyatenda. Alimwaakikishia Bill kuwa amemsamehe kwa makosa yote aliyomtendea. Mambo yote yalionekana kwenda vizuri mpaka hapo Bill alipojiandaa kuondoka. Alipokuwa anatoka chumbani, Joe alimuita, “Lakini kumbuka, nikipona, haya yote niliyosema hayana maana wala uzito.”
Yesu alisisitiza sana hitaji la kuwasamehe wengine kama tunavyosoma katika Biblia “Kisha Petro akamwendea Yesu, akamwuliza, ‘Je, ndugu yangu akinikosea, nimsamehe mara ngapi? Mara saba?’ Yesu akamjibu, ‘Sisemi mara saba tu, bali sabini mara saba.’” (Mathayo 18:21” Kusamehe mara sabini na saba kunamaanisha kusamehe kila mtu kila mara. Usipofanye hivyo moyo wako unakuwa mwamba.  Usiposamehe unafanya moyo wako uwe mwamba usiopenyeka.

“Jicho kwa jicho” mtazamo huo  utawaacha watu wengi wakiwa vipofu. “Jino kwa jino” mtazamo huo utawaacha watu wengi wakiwa vibogoyo. Kisasi kilicho bora ni kusahau. Ndivyo isemavyo methali ya Kiswahili. Lakini kisasi kilicho bora zaidi ni kusamehe.  Na pia kisasi kilichobora zaidi ni kutokuwa kama yule aliyekufanyia jambo baya ili pasiwepo watu wabaya wawili, yeye aliyekufanyia ubaya na wewe unayeshindwa kujibu ubaya kwa wema. Nelson Mandela alikuwa na haya ya kusema juu ya kusamehe waliomtendea vibaya: “Nilivyotembea kutoka mlangoni nakuelekea lango ambalo likuwa natokea na kwenda kwenye uhuru wangu, nilijua kuwa kama nisingeacha ukali wangu na chuki nyuma yangu, ningeendelea kuwa gerezani.” Kusamehe ni kumfungua mfungwa utagundua mfungwa ni wewe. Kabla ya kusamehe unakuwa kwenye gereza la chuki na kulipiza kisasi. Kumbuka chuki umchoma anayeitunza. “Msamaha ni manukato ambayo ua huacha kwenye kisigino kilicholikanyaga,” alisema Mark Twain. Kutosamehe ni kurudi nyuma. Nakubaliana na Libba Bray aliyesema: “Hatuwezi kurudi nyuma. Tunaweza tu kwenda mbele.”  MSAMAHA NI BREKI HAKUNA HAJA YA KUGONGA.
Mungu sio Adui wa Adui Zako
Martin  Niemoller alitoka katika gereza la Hitler akisema, “Ilininchukua muda mrefu kujifunza kuwa Mungu sio adui wa adui zangu. Na sio adui  wa maadui zake.” Kama unapenda watu wakupende nawe uwapende. Injili ya leo inatutaka tuwapende adui zetu: “Mmesikia kwamba imenenwa, ‘umpende jirani yako, na umchukie adui yako.’ Mimi lakini nawaambieni, wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowadhulumu…” (Mathayo 5:43-44).  Adui mpende. Ni methali ya Kiswahili. Usimchukie hasidi au adui yako. Adui zetu yafaa kuwachukulia makosa yao watutendeavyo. Huenda wakatubu na kuacha uovu wao. Tunaaswa na methali ya Kiswahili, Adui aangukapo mnyanyue. Ni methali nyingine ya Kiswahili kuhusu kumpenda adui na kumtendea mema. Ni ubinadamu kumsaidia adui yako akiwa na shida. “Tunapowachukia maadui wetu tunawapa uwezo juu yetu: uwezo juu ya usingizi wetu, hamu yetu ya chakula, shinikizo letu la damu, afya yetu na furaha yetu.” (Dale Carnegie) “Jinsi miti yote inavyojulikana kwa vivuli vyake, ndivyo hivyo watu wazuri wanajulikana kwa maadui wao.” (Methali ya Kichina).

3.       MOYO WENYE MIIBA
Bwana Yesu Kristu alitoa tafsiri ya miiba: “Mbegu imeanguka kati ya miiba kwa mtu anayelisikia neno, lakini shughuli za dunia na ulaghai wa mali hulisonga neno” (Mathayo 13:22).  Miiba ni shughuli nyingi na ulaghai wa mali. Shughuli nyingi ni miiba katika kutekeleza neno la Mungu. Shetani anaweza kukushawishi ili uwe na shughuli nyingi ili usishughulikie jambo lilo muhimu. Eva alikuwa msaidizi wa Adamu na Adamu msaidizi wa Eva katika raha na shida katika magonjwa na afya. Lakini Eva alipokuwa anajaribiwa na Adamu, Adamu alikuwa na shughuli nyingi hakuwa pamoja na Eva. Pengine shughuli nyingi zinaweza kuwa namna ya uvivu. Nina shughuli nyingi sitaenda Kanisani. Hapo kuna uvivu wa kwenda Kanisani. Miiba hipo nje. Miamba hipo ndani.


4.       MOYO WENYE UDONGO WENYE RUTUBA
“Mbegu imeanguka katika udongo wenye rutuba kwa mtu anayelisikia neno na kulitunza moyoni. Akazaa na kutoa matunda, huyu mia, na huyu sitini, na mwingine thalathini” (Mathayo 13: 23). Hapa kuna udongo uliotayari kulimwa. Utayari ni jambo muhimu. Kuna hadithi ya Bwana aliyekuwa tajiri sana. Alipofika mbinguni alikaribisha kwenye nyumba ya nyasi. Alipinga sana. Aliambiwa hiyo ndiyo nyumba umeandaliwa. Aliuliza, “Hiyo mansion pale ni ya nani?” “Aliambiwa ni ya mpishi wako.”  “Inakuwaje ana nyumba nzuri sana kunizidi. Aliambiwa nyumba hapa zinajengwa kutokana na vifaa unavyotuma mbinguni. Wewe ulituma nyasi na miti.  Ukichukua glasi ya kuweka maji  ukakuta ni chafu ina mende waliokufa hauwezi kuweka maji. Ukitaka kunywa supu ukakuta bakuli ni chafu hauwezi kuweka supu yako. Mungu anataka kukupa neema lakini anajiuliza niweke wapi neema hizi? 

Counter

You are visitor since April'08