Saturday, September 13, 2014

UKIUBEBA VIZURI MSALABA MSALABA UTAKUBEBA



                          
                                               SIKUKUU YA KUTUKUKA MSALABA
                                                        JUMAPILI YA 24 YA MWAKA A
“Hakuna msalaba, hakuna Mkristo,” alisema  Profesa Mchungaji Daniel Deutschlander wa Ujerumani. Msalaba ni kitambulisho cha mkristo. “Muumini yeyote ambaye hajaukabili msalaba, bado hajawa mfuasi wa Kristo,” alisema  S. E. Entsua-Mensah mchungaji anayeishi Kumasi Ghana. Msalaba unavyotumika hapa haumaanishi mti bali mateso, matatizo, shida, udhia, karaha, sononeko, huzuni na maumivu. Binadamu naye anaweza kuwa msalaba licha ya kuwa neema. Mtoto anaweza kuwa msalaba kwa mzazi. Mke anaweza kuwa msalaba kwa mumewe. Mume anaweza kuwa msalaba kwa mke wake. Wajibu kwa umma na kwa Mungu ni msalaba. “Daima imani hubaki kuwa jambo la msalaba,” ameandika hivyo Papa Francis Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki kwa sasa katika kitabu chake Furaha ya Injili.  Kuna mke wa mtu alipata ujumbe kwenye simu ya mkono toka kwa mpango wa kando au nyumba yake ndogo uliosema hivi:”Nimekuacha tangia leo.” Mwanamke huyo akaanza kulia. Mme wako akamuuliza: “Ni ujumbe gani huo uliosoma halafu unaanza kulia.” Mwanamke akasema: “Ni ujumbe kuhusu namna ya kupika.” “Sasa kuna jambo la kukufanya ulie?” Mwanamke akasema: “Nimefikia kwenye sehemu ya kukata vitunguu. Na unajua vitunguu vinafanya mtu atoke machozi.” Usanii wa namna hiyo ni msalaba. Mwanamke wa namna hiyo ni msalaba.
Wasafiri nao wanaweza kuwa msalaba. Methali ya Kiswahili inasema yote: Msafiri kafiri. Kuna mtu amenitumia ujumbe huu kwenye simu ya mkononi: “Jamaa alikuwa kwenye daladala (Matatu) pembeni kuna dada mrembo kaka. Kamlia timing kwa muda kisha halafu akamuuliza ‘Samahani dada unaitwa Google?” Dada akamjibu: “Hapana, kwa nini umedhani naitwa hivyo?” Jamaa: “Una kila kitu ninachokitafuta.” Msafiri mwenzako anaweza kuwa msalaba.
Swali linabaki tubebeje msalaba? Tusiubebe kwa manung’uniko. Wana wa Israel baada ya Mungu kuwatendea miujiza walipopata na matatizo walinung’unika: “Njiani watu wakakata tamaa. Wakawanung’unikia Mungu na Musa. ‘Kwa nini mmetutoa Misri tuje tufe huku jangwani? Maana huku hakuna mkate wala maji; tumechoka na chakula hiki dhaifu!” (Hesabu 21: 4-5). Chakula walikuwa nacho lakini walikiita dhaifu.  “Maelekeo yetu tukiwa kwenye mateso ni kumgeukia Mungu. Ni kuwa na hasira na kuwa wakali na kuikunjia mbingu ngumi na kusema, ‘Mungu, haujui mateso yanavyofanana! Uelewi! Hauna wazo lolote juu ya yale ninayoyapitia. Uelewi ni kwa kwa kiwango gani inahumiza.’ Msalaba ni njia ya Mungu ya kuondoa mashitaka yetu, visingizio na hoja zetu kwake. Msalaba ni Mungu anachukua mwili na damu na kusema, ‘Na mimi pia,” alisema Mchungaji Rob Bell (Alizaliwa mwaka 1970. Alitajwa mwaka 2011 na gazeti  la Time Magazine la Amerika kuwa ni mmoja kati ya watu 100 duniani wenye ushawishi mkubwa).
“Mateso yanatualika kuweka maumivu yetu katika mikono mikubwa. Katika Kristu tunamwona Mungu akitutesekea. Na kutualika kushiriki katika upendo wa Mungu unaoteseka kwa ajili ya ulimwengu unaohumiza . Maumivu yetu madogo na yanayotuzidi nguvu ya maisha yetu yanaunganishwa kwa ukaribu sana na maumivu makubwa ya Kristo. Mateso yetu ya kila siku yanatia nanga katika mateso makubwa na kwa hiyo kuna matumaini makubwa,” alisema Padre  Henri J.M. Nouwen
Ubebe kwa uvumilivu na subira bila kutarajia matokeo ya mara moja. Papa Francis amekuwa na haya ya kusema katika kitabu chake Furaha ya Injili: “Shauku inayokithiri iliyopo leo hii kuhusu matokeo ya mara moja inawafanya wahudumu wa uchungaji waone vigumu kuvumilia jambo lolote linaloonekana kama vile linakosa makubaliano, lina uwezekano wa kushindwa, kuna maoni ya upinzani, ni msalaba.” Jani la chai likiwa kwenye maji moto linabadili rangi ya maji. Badili mambo kwa uvumili wako. Huko ni kubeba vizuri msalaba. Stempu haitoki kwenye bahasha mpaka bahasha imemfikia mlengwa. Huu ni mfano wa kubeba msalaba kwa uvumilivu.  Yesu hakushuka toka msalabani.
Ubebe bila kukata tamaa na kwa upole. Papa Francis ameandika hivi katika kitabu chake, Furaha ya Injili:  “Pamoja na kutambua unyonge wetu kwa uchungu mkubwa, ni lazima tusonge mbele bila kukata tamaa, tukizingatia kile ambacho Bwana alimwambia Mtakatifu Paulo: “Neema yangu inakutosha, maana nguvu yangu hufanywa kuwa kamilifu katika udhaifu’ (2 Kor 12:9). Daima ushindi wa Kikristo huwa ni msalaba, lakini ni msalaba ambao wakati huo huo ni bendera ya ushindi inayobebwa kwa upole wenye guvu dhidi ya mashumbulizi ya uovu.” Tumebebe msalaba kwa upole na matumaini.  Kuubeba vizuri msalaba ni kufikiria juu ya wengine badala ya kufikiria juu ya mateso yako tu. “Ingawa Yesu alikuwa katika mateso msalabani, alifikiria juu ya kuwaombea watesaji wake, kutunzwa kwa mama yake, kuratibisha wokovu wa mwizi,” alisema Thomas Dubay. Akili yako unapoiweka kwenye mateso ya wengine inasaidia kubeba vyema ya kwako. “Msalaba ni mahali ambapo mbingu inakutana na dunia na neema inalipuka. Msalaba sio mahali ambapo Yesu anakabili mateso yetu tu, bali anakuwa mateso yetu ili kubadilisha dunia,” alisema Mchungaji Matt Farlow wa Kanisa la New Wine, New Wineskins. Tubebe msalaba kwa hekima tukitafuta suluhisho la matatizo. Tubebemsalaba kwa upole hasira haisahidii. Tubebe msalaba kwa imani. Tubebe msalaba kwa uvumilivu tukitafuta suluhisho la matatizo.
NYOKA  WA  SHABA  AL IYEINULI WA NA MWANA WA MTU AL IYEINULIWA
Kuna kitendawili kisemacho: “Viwili vyafanana”. Jibu ni Meli na Pasi. Viwili vyafanana ni nyoka wa shaba aliyeinuliwa, aliyetundikwa na Mwokozi aliyeinuliwa. “Kama vile Musa alivyomwinua juu nyoka wa shaba kule jangwani, naye Mwana wa mtu atainuliwa juu vivyo hivyo ili kila anayemwamini awe na uzima wa milele. (Yohane 3:14) Mwinjili Yohane hueleza nyoka wa shaba kama mfano wa
Kristo aliyeinuliwa msalabani. Tunasoma hivi katika kitabu cha hesabu, “Watu wakamnung’unikia Mungu, na Musa, “Mbona mmetupandisha huku kutoka nchi ya Misri, ili tufe jangwani? Maana hapana chakula, wala hapana maji, na roho zetu zinakinai chakula hiki dhaifu”. Bwana akatuma nyoka za moto kati ya watu, wakawauma, watu wengi wakafa. Watu wakamwendea Musa, wakasema, “Tumefanya dhambi kwa sababu tumemnung’unikia Mungu, na wewe; utuombee kwa Bwana atuondolee nyoka hawa”. Basi Musa akawaombea watu. Bwana akamwambia Musa, “Jifanyie nyoka wa shaba ukamuweke juu ya mti, na itakuwa kila mtu aliyeumwa aitazamapo ataishi. Musa akafanya nyoka ya shaba, akaiweka juu ya mti; hata ikiwa nyoka amemuuma mtu, alipoitazama ile nyoka ya shaba, akaishi” (Hes.21 :4-9).
UFANANO
Nyoka wa shaba hakuwa wa sumu, ingawa alikuwa na sura ya nyoka. Ingawa Yesu alionekana kama mnyang’anyi, alionekana kama mdhambi hakuwa na dhambi. “Hapakuwa na hila kinywani mwake” (Isaya 53:9). Kama nyoka wa shaba alivyoinuliwa Yesu aliinuliwa msalabani. Aliyemtazama nyoka alipona. Majeraha ya sumu yalitibiwa. Yesu anatibu majeraha ya dhambi. Ingawa nyoka wa shaba alikuwa ni nyoka lakini ni wa shaba. Yesu alikuwa mtu lakini ni Mungu,ni Mungu mtu.

TOFAUTI
Zipo tofauti kati ya nyoka wa shaba aliyeinuliwa na Yesu aliyeinuliwa. Jukwaa la nyoka aliyeinuliwa ni jangwa. Jukwaa la Yesu aliyeinuliwa ni Kalvari. Watazamaji upande wa nyoka wa shaba ni wana wa Israeli. Upande wa Yesu aliyeinuliwa ni dunia nzima. Jamii yote ya binadamu inamtazama Yesu msulubiwa. Wana wa Israeli waliomtazama nyoka aliyeinuliwa walitibiwa kimwili baadaye, miaka kupita, siku kupita walikumbwa na kifo cha kawaida. Kifo hakina kalenda na hakuna atakayesahaulika. Yesu aliyeinuliwa hatibu tu magonjwa ya kimwili na ya kiroho pia. Yeyeanatoa maisha ya milele.
KUTAZAMA NI KUSADIKI
“Kutazama” katika Injili ya Yohane kuna maana ya kusadiki. Kumtazama Yesu aliyeinuliwa ni kumsadiki. “Watamtazama yeye waliyemchoma” (Yohane 19:37). Akida wa kirumi ni mfano wa wapagani waliomsadiki Yesu kwa kumtazama. “Basi yule akida, na hao waliokuwa pamoja naye wakimlinda Yesu, walipoliona tetemeko la nchi na mambo yaliyofanyika, wakaogopa sana, wakisema, hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu” (Mt. 27:54). Kuamini siyo kutaja maneno ya kanuni ya imani bali kuyaishi.
 MATATIZO NI MSALABA
 Katika nchi yangu kwanza unakwenda gerezani halafu unakuwa rais baadaye,” alisema Hayati Nelson Mandela aliyeaga dunia akiwa na umri wa miaka 95. Wajibu wa Hayati Nelson Mandela kwa umma na uzalendo vilikuwa ni msalaba. Aliuchukua msalaba huu ukamchukua hadi ikulu. Kuna upande mzuri wa msalaba kama matatizo. Ni katika msingi huu Yesu alisema: “Mtu asiyechukua msalaba wake na kunifuata, hanistahili” (Mathayo 10: 36). “Huwezi kukwepa msalaba, popote unapokimbilia; popote unapokwenda, kila mara utaukuta. Ukiuchukua msalaba kwa kuupenda, utakuchukua na kukupeleka unapopatamani: yaani kule ambapo patakuwa na mwisho wa mateso, ingawa hapa hakuna mwisho wa mateso. Ukiuchukua bila kupenda, unaufanya uwe mzigo kwako kuchukulika…ukiuutupa kwa nguvu msalaba mmoja bila shaka utakutana na mwingine labda mzito zaidi,” alisema Thomas á Kempis.
Picha ya matatizo kama msalaba tunaipata katika sala ya Kanisa Katoliki ambayo husaliwa Ijumaa Kuu na kipindi cha Kwaresima: “Ee Yesu mkarimu, mimi pia ninao msalaba wangu: jirani zangu, mwenzangu wa ndoa, watoto, wazazi wangu, kazi zangu, joto, baridi,   njaa,   kiu,,, vishawishi, magonjwa na matatizo mengine ya maisha, wajibu wangu kwa Mungu, kwa umma na kwa Kanisa hayo yote ni msalaba. Unipe ukarimu wako ee Yesu, niyapokee bila kunung’unika na kuyabeba vema.”
Mwenzako wa ndoa anaweza kuwa msalaba. Kuna mwanaume aliyemsikia mchungaji anahubiri juu ya maneno ya Yesu: anayetaka kuwa mfuasi wangu abebe msalaba wake na anifuate. Mwanaume alipofika nyumbani alimbeba mke wake. Akampitisha sebuleni, bafuni, jikoni, barazani. Mwanamke alishangaa na kusema: ulinibeba siku ya kufunga ndoa. Mchungaji amefundisha nini Kanisani unanibeba namna hii leo hii. Mwanaume huyo alisema: mchungaji amefundisha tubebe misalaba yetu.  
Usijitengenezee msalaba. Kuna misalaba ya kujichongea. Kujiingiza kwenye mambo ya watu wengine, sio kwa sababu ya Yesu. Ukisikia mwanamke anasema sitaolewa tena na mwanamme huyu. Usiijiingize katika ugomvi wao na kuanza kuchochea. Ni kama kusema shuka kutoka kwenye msalaba wa ndoa. Ukipata matatizo huko umejiingiza kwenye ndoa ya watu si kujenga bali kubomoa. Ndugu wakigombana chukua jembe ukalime wakipatana chukua kapu ukavune. Usichochee ugomvi kati ya ndugu wakipatana watakugeuka na wewe utakuwa umejichongea msalaba. Wasaidie kupatana. Usichochee mafarakano. Kuwa na kiburi ni kujitengenezea msalaba. Kutukana watu ni kujitengenezea msalaba.  

Kuna kijana wa miaka thelathini aliyemua baba yake na mama yake. Baada ya kutolewa hukumu aliulizwa kama anaweza kujitetea. Aliomba kupunguziwa miaka akiota hoja yeye ni  mwana yatima hana baba wala mama. Huu ni msalaba wa kujitakia sio kwa sababu ya Yesu. Kuna aina mbili za misalaba: msalaba wenye Yesu Kristu na msalaba usio na Yesu Kristo.  Msalaba wenye Yesu ni pale ambapo unatazama matatizo yako kwa kutumia miwani ya Yesu yaani hakuna Jumapili ya Paska bila Ijumaa Kuu. Ripoti kwa Yesu matatizo yako. Mweke Yesu katika matatizo yako. Msalaba usio na Yesu ni pale ambapo unashindwa kuripoti matatizo yako kwa Yesu. Haubebi mtazamo wa Yesu wa Ijumaa Kuu kwanza Jumapili ya Paska baadaye.
Matatizo ni m\salaba. Kuna ishara ya msalaba. Matatizo yanaweza kuwa ishara ya mafanikio siku za mbeleni. Dalili ya mvua ni mawingu. Dalili ya mafanikio inaweza kuwa matatizo. Kabla ya kufika bandarini kuna mawimbi makali na makubwa. Unaweza kuwa mtu mwema lakini ukateseka. Kwa nini watu wema huteswa na wengine au na jirani. Jirani yako anaweza kuwa msalaba. Sababu ni kuwa watu wema wanafanya mambo mazuri tofauti na wengine. Watu kama hawakuelewi watakutesa. Utendaji kazi wa watu wema unawaibisha wavuvi. Watu katika ofisi wakiamua kubadili  mambo ofisini na wewe haushiriki watakutukana. Watu wema ni kikwazo kwa mipango ya watenda maovu. Utasikia watu wanasema ficha ficha, fulani amekuja. Watu wema hawabadili misimamo yao. Mfano wa Danieli. Mfalme alitaka Danieli abadili msimamo wake. Hakubadili. Alitupwa katika shimo la simba. Lakini kwa mihujiza Mungu alimtoa. Ukiubeba msalaba vizuri utakubeba. Mwanamke anamkataa bosi na kumwambia mme wangu ananitosha na kuniridhisha. Ofisini mwanamke huyo anateswa sababu ya msimamo wao, kwa sababu ya jina la Yesu. Aliapa Kanisani kwa jina la Yesu. Akibeba vizuri msalaba. Msalaba utambeba.


Counter

You are visitor since April'08