Saturday, September 6, 2014

UJIPENDE USIJEPENDELEE



                                              
                                        JUMAPILI YA MSAMARIA MWEMA
                                    Jumapili ya 23 ya Mwaka A
1. Ezekieli 33: 7-9
2. Woroma 13: 8-10
3. Mathayo 18: 15-20

“Msiwiwe na mtu chochote, isipokuwa kupendana…Mpende jirani yako kama nafsi yako…” (Woroma 13: 8-10)
Mama anayenyonyesha mtoto akiamua kunyonya titi lake mwenyewe na kunywa maziwa ya mtoto jambo hilo halikubaliki. Ni kujipendelea. Mama huyo amejipenda kupita mipaka ya kujipenda. Jambo la msingi ujipende lakini usijipendelee. Kumsaidia mtu hakumaanishi kutojijali au kutojitunza. Anayejihukumu husema yeye ni mzuri wa sura. Hizo ni methali za Afrika ambazo zinasisitiza umuhimu wa kujipenda. Inashangaza kuona kuwa fundi seremala licha ya kutengeneza viti vya kukalia yeye hana kiti hata kimoja nyumbani. Huyo hajipendi. Mtengeneza vyungu vya udongo vya kupikia yeye anakula chakula kutumia kipande cha chungu kilichovunjika. Huyo hajipendi. Itashangaza kuona kuwa mjenzi wa nyumba nzuri sana yeye ana nyumba ya makuti ambayo inaweza kuanguka wakati wowote.
 Jambo la katikati ni kujipenda. Jambo baya kulia kabisa ni kujipendelea, uchoyo, ubinafsi na umimi. Ni kujipendelea kupita kiasi. Jambo baya kushoto kabisa ni kutojipenda, kutojijali, kutojitunza. Kujipendelea ni kujifikiria wewe mwenyewe tu. Kutojipenda ni kujipunguzia heshima au hadhi. Kutojipenda ni kujidhalilisha. Mtu ambaye hajipendi ni mtu ambaye anajidanganya yeye mwenyewe.
Kuna methali isemayo: Watu wanajilamba vidole (sababu ya kutoshiba) wewe unasema mbwa wangu aitwaye simba hajala. Ni methali ambayo inaelimisha umuhimu wa kumtanguliza kwanza binadamu mwenye shida kama mwenye njaa. Njaa ina matokeo mabaya mengi. Mtu mwenye njaa ni mtu mwenye hasira. Ni methali yaw a Igbo wa Nigeria. Utamu haumalizi njaa. Ni methali ya Kenya. Kuna mwanaume mmoja alimwambia mke wake: Haupiki chakula kizuri kama mama yangu.” Naye mwanamke alijibu: “hauna fedha kama baba yangu.” Anayepika vizuri anapika alivyoletewa. Pengine chanzo cha ugomvi huo ni njaa.
Ni mtu mbaya ambaye ni mzuri tu kwa ajili yake tu. Ni ujumbe ambao tunaupata kutoka katika methali ya Haiti isemayo: wewe ni mbaya, kama ni mzuri kwa ajili ya nafsi yako tu. Methali hii inambainisha mtu anayejipendelea. Hatuna budi kujipenda. Kumsaidia mtu hakumaanishi kutojijali. Ni methali ya Mamprussi. Wakati kuna watu wanakula na kusaza kuna ambao wanalala usiku wakiwa na matumbo matupu. “Njaa ni aibu kubwa katika dunia ya leo,” alisema Baba Mtakatifu Yohani Paulo wa II. Biblia yasema “Msiwiwe na mtu chochote, isipokuwa kupendana…Mpende jirani yako kama nafsi yako…” (Woroma 13: 8-10). Tuna deni la kuwalisha wenye njaa. Kuwalisha wenye njaa ni kuwapenda. Baba Mtakatifu Francis, siku ya kuzindua kampeni dhidi ya njaa duniani tarehe 10/12/2013 alisema hivi: “Naalika taasisi zote ulimwenguni, makanisa na kila mtu mmoja, kama familia moja, kuzungumza kwa sauti kuwatetea wale wote wanaoteseka kimya kimy kwa NJAA, ili sauti yetu kubwa iwe kishindo kinachoweza kuutikisa ulimwengu.” Kadiri ya tafiti zilizofanyika, njaa inaua mtu mmoja kila sekunde tano duniani.
Ulimwengu una mali za kumtosha kila mtu, lakini hauna mali za kuwatosha wanaojipendelea. Ni katika mtazamo huo naweza kusema ulimwengu una chakula cha kumtosha kila mtu lakini hauna chakula cha kuwatosha wanaojipendelea. Naye Baba Mtakatifu Francis amekuwa na haya ya kusema: “Ni jambo la kuiabisha na kuleta huzuni kubwa kufahamu kwamba watu wengi duniani wanateseka kwa njaa wakati ulimwengu unacho chakula cha kutosheleza kulisha kila mtu. Hali ya watu kutokuwa na nafasi sawa ya kupata chakula ndiyo kiini cha janga la njaa duniani. Hali hii inazidi kuwa mbaya wakati mashirika makubwa yanapoficha chakula ili kipande bei, kuhamasisha ukulima wa mazao ya kuzalisha nguvu za kuendesha mitambo ya machine kama ‘jatorpher,’ utupaji wa chakula kinachofaa kwa matumizi ya binadamu na ugumu wa kufikia masoko. Haki ya kupata chakula inalinda haki ya msingi ya binadamu ya kutokuwa na njaa.”
 Bwana Yesu alipofanya muujiza wa kuongeza mikate mitano na samaki wawili na kulisha umati wa watu zaidi ya elfu tano watu waliposhiba aliwaambia wanafunzi wake, “Kusanyeni vipande vilivyobaki visipotee bure.” Maneno hayo ni changamoto kwetu kukusanya chakula kinachobaki kisipotee bure maana kuna ambao wanaenda vitandani matumbo matupu.
Nakumbuka sala ya mkristu moja nilipoalikwa katika sherehe ya kuanza  mwaka mpya. Chakula kilikuwa kingi na cha kila aina, yaani meza ilikuwa imechafuka. Mwenyeji wetu alisali hivi, “Baba wa Mbinguni nakushukuru kwa mambo matatu:chakula, hamu ya kula, na watu wakula chakula hiki. Kuna watu wenye hamu ya kula lakini hawana chakula, kuna ambao wana chakula lakini hawana hamu ya kula, kuna ambao wana chakula na hamu ya kula lakini hawana watu wa kula chakula…”Walioathirika na baa la njaa wana hamu ya chakula na watu wa kula chakula lakini shida ni uhaba wa chakula. Unapowasaidia wenye njaa unajipenda maana unajiwekea pointi mbinguni. Unaposhindwa kuwasaidia wenye njaa unajipendelea.
“Si rahisi kuzungumzia amani pale ambapo watu wanateseka kwa sababu ya njaa,” alisema Papa Benedict XVI wakati pia akishutumu wingi wa fedha unaotumika katika kununulia silaha. Ujumbe huu Baba Mtakatifu aliutoa alipozungumza na maafisa wa ubalozi siku ya Jumatatu tarehe 9 mwezi wa Januari 2006.
TUMEUMBWA KUPENDA NA KUPENDWA
 Mtu anaweza kulipa deni la dhahabu, lakini mtu huyo atakufa akiwa katika deni la upendo milele yote. Ndivyo isemavyo methali ya Malaya. Ukiwa unadaiwa shilingi elfu kumi unaweza kulipa lakini sio rahisi kulipa deni la upendo la mke wako, baba yako, mama yako, mme wako, mtoto wako au  mfadhili wako. Licha ya ukweli huo tumeumbwa kupenda na kupendwa. Katika Biblia tuna amri mbili za upendo. Amri ya kwanza ya upendo ni: Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, kwa akili zako zote na kwa roho yako yote. Na  amri ya pili ya upendo ni mpende jirani yako kama unavyojipenda (Mathayo 22: 34 -40).

 Usipopenda unakuwa haujatimiza mojawapo la lengo la kuumbwa kwako. Kama kitabu hakiwezi kusomwa au kosomeka hakijatimiza lengo la kuandikwa kwake. Kama kengele haitoi sauti inapogongwa imeshindwa kufukia malengo ya kutengenezwa kwake. Kama chakula hakiwezi kuliwa au hakiliki hakijafikia lengo la kupikwa kwake. Hivyo hivyo kama binadamu hawezi kupenda na kupendwa ameshindwa kufikia lengo la kuumbwa kwake.

Hasiyekujua hakuthamini. Hatuwezi kumpenda Mungu kama hatumjui. Tunamjua Mungu kupitia mambo mengi. Tukisoma vitabu vitakatifu tunamjua Mungu. Hauwezi kumpenda jirani yako kama haumjui. Asiyekujua hakuthamini. Kuna mtu aliyeaniambia, “Padre usinitambulishe kwa huyo jamaa. Maana nataka kuendelea kumchukia. Nikimjua nitampenda.” Nilichukua nafasi hiyo kuelezea athari na matokeo ya chuki. Chuki humchoma anayeitunza.
Ukimjua Mungu utampenda. Kuna fundi aliyekuwa juu sana ya jengo alitaka mafundi chini wampandishie matofari. Alitupa chini shilingi ishirini toka juu. Fundi aliyekuwa chini aliokota pesa hiyo na kuweka mfukoni hakutazama juu. Alitupa tena “mbao,” fundi mwingine akaiokota bila kutazama juu. Baadaye alitupa jiwe dogo likamgonga fundi mmoja chini. Fundi huyo alitazama juu kwa vile alihumizwa kidogo. Mungu anaweza kutuletea mateso kwa vile anataka kututumia ujumbe Fulani. Mateso hayo yanaweza kuwa ni alama ya upendo. Mama umunywesha mtoto wake dawa chungu ili apone kwa sababu anampenda mtoto wake. Tukijua kuwa Mungu wetu ni Mungu wa namna hiyo tutampenda.
Amri ya pili ya upendo inasema, “Mpende jirani yako kama nafsi yako.” Ni lazima kujipenda na sio kujipendelea ili uweze kuwapenda wengine kama unavyojipenda. Kula chakula ni kujipenda lakini kula robo tatu ya chakula na kumwachia mwenzako aliye na tumbo kama wewe na hamu kama wewe robo tu ya chakula ni kujipendelea. Kuwa na ardhi ni kujipenda, lakini kuwa na ardhi kama jimbo zima la uchaguzi ni kujipendelea.



Counter

You are visitor since April'08