Saturday, August 23, 2014

WATU WANASEMA NINI JUU YAKO?



                              

                                             JUMAPILI YA 21 YA MWAKA A
1.      Isaya 22: 19 – 23
2.      Warumi 11: 33 – 36
3.      Mathayo 16: 13 – 20



Aliwauliza wanafunzi wake, ‘Watu wanasema Mwana wa Mtu kuwa ni nani?’ “Kristu aliwauliza swali hili wafuasi wake ili katika majibu yao tujifunze kuwa wakati huo kati ya wayahudi yalikuwepo maoni mbalimbali juu ya Kristo; na mwishowe tufanye utafiti watu wana maoni gani juu yetu; wakitusema vibaya tupuzie; wakitusema vizuri tujiongezee fursa hizo,” alisema Origen Baba wa Kanisa.


Uwezi kuwazuia ndege wa mateso wasiruke juu ya kichwa chako, lakini unaweza kuwazuia wasijenge viota kwenye nywele zako. Ni methali ya Kichina. Watu watakusema. Si rahisi kuzuia hilo. Kama unafanya mambo mazuri usiyumbishwe na wanayosema juu yako. Usikubali ndege wajenge viota kichwani mwako. Nakubaliana na Askofu Mkuu Desmond Tutu wa Afrika ya Kusini aliyesema: “Mungu amekuita akijua wewe ni nani. Anakutaka ulivyo wewe na upekee wako. Usikubali wengine wakubadili.”  Kuna aliyekuwa kwenye tamasha anasikiliza wimbo alikuwa na bwana mmoja wanazungumza. Akamwambia bwana huyo: “Mwanamama anayeimba hana sauti nzuri sijui ni mke wa nani?” Akajibiwa. Ni mke wangu. Bwana huyo akasema: “Nlitaka kusema aliyetunga wimbo huo alitunga wimbo mbaya sijui ni nani?” Bwana huyo alijibu: “Ni mimi.” Mfano huu unaonesha huwezi kuwazuia watu kusema.

Wakikusema vibaya tumia maneno wanayosema kama mawe ya kuvukia. “Mtu aliyefanikiwa ni yule ambaye anaweza kujenga msingi imara akitumia matofari waliomrushia,” alisema David Brinkley (1920 – 2003) mtangazaji wa habari wa Amerika.  Yatumie maneno wanayokusema kama mawe ya kuvukia. Stephen Arnold Douglas (1813 – 1861) mwanasiasa wa Amerika katika kampeini za kuwania urais wa Amerika mwaka 1858 katika mchuano mkali na Abraham Lincoln (1809 – 1865) aliwaambia wapiga kura kuwa wasimchague Abraham Lincoln kwa vile alikuwa na kilabu ya kuuza pombe kali. Naye Abraham Lincoln aliwaambia wapiga kura kuwa ni kweli na mteja wake mkubwa alikuwa Douglas, yeye aliacha shughuli ya kuuza pombe kali lakini Douglas hakuacha shughuli ya kuwa mteja. Abraham Lincoln aliyatumia maneno aliyorushiwa kama matofari ya kujengea msingi wa kukubalika kwa wapiga kura.

Katika maisha utasemwa. “Ili kukwepa kusemwa usiseme lolote, usifanye lolote, usiwe yeyote,” alisema Aristotle. Yesu alijua kuwa watu walimsema. Kuna siku alitaka kujua maoni ya watu juu yake: “Yesu alipofika pande za Kaisarea Filipi, aliwauliza wanafunzi wake, ‘Watu wanasema Mwana wa Mtu kuwa ni nani?’ Wakamjibu, “Wengine wanasema kuwa ni Yohane Mbatizaji, wengine Elia, wengine Yeremia au mmojawapo wa manabii.’ Yesu akawauliza, ‘Na nyinyi je, mnasema mimi ni nani?’ Simoni Petro akajibu, ‘Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.’ (Mathayo 16:13-16). Yesu hakuuliza mafarisayo na wanasheria wanasema mimi ni nani? Hakuuliza makuhani na walawi wanasemaje? Alitaka kujua watu wa kawaida wanasemaje. Mafarisayo na wanasheria walisema ni mlafi kwa vile anakula na kunywa na watoza ushuru. Mafarisayo na wanasheria walisema anatumtumia Beelzebub mkuu wa pepo wabaya.

Licha ya kusemwa hivyo Yesu alizidi kuimarika.  “Watu wanaotusema vibaya wanatuimarisha. Hofu zetu zinatufanya tuwe jasiri. Wanaotuchukia wanatufanya tuwe na busara. Adui wetu wanatufanya tusibweteke. Vikwazo vyetu vinatufanya tuwe na shauku. Tulivyovipoteza vinatutajirisha. Maudhi yetu yanatufanya tupandishwe hadhi. Hazina zetu zisizoonekana zinatupa amani inayojulikana. Lolote lililopangwa dhidi yetu litafanya kazi kwa ajili yetu,” alisema Israelmore Ayivor

Watu wanasema wewe ni mkristu wa aina gani. Kuna aina mbali mbali za wakristu. Kuna wakristu wanaoitwa: “Nguzo.” Hawa wanakuja Kanisani kila siku, nakutoa sadaka. Kuna wakristu wanaoitwa “Wachangiaji.” Hawa wanatoa pesa kama wanampenda mchungaji na mtunza pesa. Kuna wakristu wanaoitwa: “Waegemeaji.”  Hawa wanafanya kazi lakini hawatoi chochote. Kuna wakristu wanaoitwa: “Watu wa Kila mwaka.” Hawa wanakuja Krismasi na Pasaka. Kuna Wakristu wanaoitwa: “Watu wa pekee.” Hawa wanasaidia na kutoa kila mara. Kuna wakristu wanaoitwa: “Sponji.” Hawa wanachukua baraka zote na huduma lakini hawasaidii. Kuna wakristu wanaoitwa: “Watembezi.”  Hawa wanatoka Kanisa hili na kwenda Kanisa lingine na hawasaidii. Kuna wakristu wanaoitwa: “Wambea.”  Hawa wanawesengenya watu wote isipokuwa Yesu Kristu. Kuna wakristu wanaoitwa “Yatima.” Watoto wanatumwa Kanisa kuja kusali lakini wazazi hawaji kusali. Kuna wakristu wanaoitwa: “Wanafiki.” Hawa ni watu ambao wanasema hawaendi kanisani kwa sababu kanisani kuna wanafiki. Je, watu wanasema wewe ni nani?  

UTASEMWA TU
Huwezi kuwakataza ndege wasiruke juu ya kichwa chako. Wataruka tu. Ila wasijenge viota kichwani. Hauwezi kuwakataza watu wasiseme juu yako. Yesu alitetwa, alinung’unikiwa, alikataliwa, alinenwa. Kama alivoagua Nabii Simeoni “Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa.” Yesu ni
ishara iliyopingwa na watu”. Mbele ya Kristu hakuna “Kutofungamana na upande wowote”. Kati ya mawili ni chaguo lako ama uko upande wake au kinyume chake. Yesu alipingwa, alibishiwa, alikuwa na wapinzani. Ukiwa wake kabisa siyo kusema umekingiwa kunung’unikiwa, au kutetwa. Yesu aliambiwa maneno ya matusi chungu nzima.
Mjinga: “Basi, Wayahudi wakashangaa na kusema, ‘Mtu huyu amepataje elimu naye hakusoma shuleni?” (Yn 7:15). Yesu hakuwa mjinga. Akiwa na umri wa miaka kumi na miwili aliketi katikati ya waalimu huko Yelusalemu. “Nao wote waliomsikia walistaajabia fahamu zake na majibu yake” (Lk 2:47).
MWENDAWAZIMU: Ana pepo; tena ni mwendawazimu! Ya nini kumsikiliza?” (Yn 10:20). MLAFI NA MLEVI: “Akaja mwana wa mtu; yeye anakula na kunywa, mkasema “Mwangalieni huyu mlafi na mlevi, rafiki ya watoza ushuru na wenye
dhambi!” (Lk 7:34).
MCHAWI: Lakini Wafarisayo wakawa wanasema, “Anawatoa pepo kwa nguvu ya mkuu wa pepo wabaya” (Mt 9:34).
MWOVU: Pilato aliwaendea nje, akasema, “Mna mashtaka gani juu ya mtu huyu?” Wakamjibu, “Kama huyu hangalikuwa mwovu hatungalimleta kwako”. (Yn 18:29-30).
NABII WA UWONGO: Walimfunga kitambaa usoni, wakawa wanamwuliza, “Ni nani aliyekupiga? Hebu bashiri tuone!” (Lk 22:64).

Yesu alikutana na watu wenye majungu, uzushi na fitina. Tukumbuke hawajawahi kujenga mnara katika historia ya dunia ya kuwaenzi wazushi, na waongo. Watu walimsema Kristu sembuse wewe. Mtu akiwa mkarimu, wanasema anajitangaza. Asipokuwa mkarimu wanasema ana gundi kwenye vidole, ni mnyimi, ni bahili. Mtu akitoa hotuba fupi sana wanasema hakujiandaa. Akitoa hotuba ndefu wanasema hatunzi muda. Akiwa mtoto mchanga wanasema ni malaika. Akiwa mtu mzima wanasema achana na yule shetani. Akiwa mcha Mungu wanasema ni mkatoliki zaidi ya Papa. Asipokuwa mcha Mungu wanasema shetani amemweka mfukoni. Akiaga dunia katika uri wa ujana wanasema angefanya mengi mazuri. Akifariki umri wa uzeeni wanasema miaka yake aliiharibu tu bila kufanya chochote. Watu watakusema tu. Miaka mitatu ya utume wa Yesu kwa Bikira Maria ilikuwa ni miaka ya majonzi, miaka ya masikitiko. Alishuhudia kutanda kwa wingu la wivu dhidi ya mwanawe, mlima wa matusi kwa mwanawe, mafuriko ya chuki dhidi ya mwanawe. Yote yaliutonesha moyo wake, yote yaliuchoma moyo wake. Binadamu si pesa ambayo hupendwa na kila mtu. Yesu Kristu hakupendwa na kila mtu. Naye hakuwa bendera ya kufuata upepo wa maneno ya watu. Alikuwa na msimamo. Huwezi ukampendeza na kumridhisha kila mtu. Baba mmoja na mtoto wake wa kiume walimpeleka punda Sokoni. Baba huyo alikaa juu ya mnyama na mtoto alitembea. Watu waliokutana nao njiani walilalamika, “Ni jambo baya sana: Pande la mtu, limekaa mgongoni mwa punda wakati mtoto mdogo anatembea”. Kusikia hivyo baba huyo alitelemka toka mgongo wa punda mtoto alichua nafasi yake. Watazamaji walitoa maoni yao. “Ni jambo baya sana: mzee anatembea, na mtoto amekaa”. Kusikia hivyo wote
wakawa wamempanda punda - wakawasikia wengine wakisema, “Ni ukatili ulioje: watu wawili wamekaa juu ya punda”. Kusikia hivyo wote walitelemka. Lakini watazamaji wengine waliotoa maoni, “Ni ujinga ulioje: punda hana kitu chochote mgongoni na watu wawili wanatembea”. Mwishowe, wote wawili walimbeba punda na hawakufika sokoni.
Yesu hakuyumbishwa na maneno ya watu kama mzee huyo na mtoto wake.

Watu hawapigi teke mbwa aliyekufa bali aliye hai. Watu hawautupii mawe mwembe usio na matunda. Ukiwa na “matunda” watu watakutupia mawe ya maneno ya kukukatisha tamaa.
Vumilia. Mvumilivu hula mbivu. Mama hupenda mtoto wake acheze ashangiliwe badala ya kuzomewa. Yesu alitukanwa. Matusi hayo ni Upanga uliochoma moyo wa Maria. Lakini alivumilia. Usiogope upinzani, kumbuka tiara huruka angani dhidi ya upepo na
si pamoja na upepo.


MABABA WAKANISA WASEMAVYO
Yesu alipofika pande za Kaisarea Filipi: “Anaongeza ‘Filipi’ ili kutofautisha na pande nyingine za Kaisarea kama Strato na anauliza swali hili akiwa Filipi. Hapa palikuwa mbali na wayahudi ili kuwaondoa wafuasi wake hofu zozote ili waongee kwa uhuru lilikokuwa kwenye akili zao. Filipi alikuwa ndugu wa Herod…ambaye alilipa jina mji la Kaiseria kwa heshima ya Kaiseria Tiberias,” alisema Mtakatifu Yohane Krisostomu. Watu wataongea mengi juu yako wakiwa huru, wakiwa mbali.

aliwauliza wanafunzi wake, ‘Watu wanasema Mwana wa Mtu kuwa ni nani?’ “Kristu aliwauliza swali hili wafuasi wake ili katika majibu yao tujifunze kuwa wakati huo kati ya wayahudi yalikuwepo maoni mbalimbali juu ya Kristo; na mwishowe tufanye utafiti watu wana maoni gani juu yetu; wakitusema vibaya tupuzie; wakitusema vizuri tujiongezee fursa hizo,” alisema Origen.

Wakamjibu, “Wengine wanasema kuwa ni Yohane Mbatizaji, wengine Elia, wengine Yeremia au mmojawapo wa manabii.’ “Ilikuwa rahisi kwa umati kukosea kwa kumfikiri a Yesu kuwa ni Eliya na Yeremia kama Herod alivyomfikiria kuwa ni Yohane Mbatizaji; nashangaa baadhi ya wahakiki wangejaribu kutafuta sababu ya makosa haya,” alisema Jerome.   

Yesu akawauliza, ‘Na nyinyi je, mnasema mimi ni nani?’ “Wafuasi baada ya kutoa maoni ya watu wa kawaida Yesu anawakaribisha wafikiria mawazo ya juu zaidi kumhusu yeye na hivyo linafuata swali ‘Na nyinyi je, mnasema mimi ni nani?’ Nyinyi ambao mmekuwa pamoja name kila mara na mmeona miujiza mikubwa zaidi ya watu wengi, hampaswi kukubaliana na maoni hayo. Kwa sababu hiyo hakuwauliza swali hilo alipoanza kuhubiri lakini baada ya kufanya miujiza mingi,” alisema Mtakatifu Yohane Krisostomu.

Simoni Petro akajibu, ‘Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.’ (Mathayo 16:13-16). “Anamuita ‘Mungu aliye hai,’ ukilinganisha na miungu wale wanaoheshimiwa lakini wamekufa; kama Saturn, Jupiter, Venus, Hercules na miungu wengine,” alisema Jerome. Yesu ni Mungu aliye hai.

Counter

You are visitor since April'08