Saturday, December 6, 2014

FADHILA INASIMAMA KATIKATI




                                                     Jumapili ya 2 ya Majilio
1. Isaya 40: 1-5, 9-11
2. 2 Peter 3: 8-14
3. Marko 1: 1-8

Barabara ya maisha ambayo haina fadhila ni barabara ambayo haikunyoka. “Dhahabu yote iliyoko chini au kwenye ardhi haitoshi katika kubadilishana na fadhila,” alisema Plato.   Fadhila ni kama unyenyekevu, subira, ukarimu, msamaha, upole. Kama hayo yapo katika maisha ni kuwa barabara ni tambarare. Kinyume chake ni tabia mbaya, uovu  au vilema kama majivuno, uvivu, uchoyo na hasira. Kama hivyo vipo barabara ya maisha ina mabonde. Mbeuzi mmoja yaana mtu mwenye tabia ya kudharau mambo nyakati za  Dk Johnson alichukulia msimamo kuwa  hakuna tofauti kati ya fadhila na tabia mbaya au kilema.  Dk. Johnson alipopata habari hizo alisema: “Mtu wa namna hiyo akitoka kwenye nyumba  yetu hesabu kama vijiko vimekamilika.” Lakini barabara ya maisha inaweza kuwa na milima. Fadhila ikizidi kupita kiasi au kupindukia ni milima.

Wito wa Injili ya Marko ni: “Itengenezeni njia ya Bwana, yanyosheni mapito yake” (Marko 1: 3). Kunyosha mapito ni kufikia mabonde ya vilema na kushusha milima ya kuzidisha fadhila kupindukia, ili tuwe na tambarare ya fadhila. Hivyo unavyojiandalia Krismasi andaa njia kukutana na Njia. Yesu Kristu ni Njia. Ni fadhila yenyewe. Fadhila inasimama katikati ya kasoro na ziada kupindukia. Fadhila ya busara inasimama katikati ya uzembe na ulaghai. Busara ikizidi sana ni ulaghai. Upungufu, dosari katika masuala ya busara ni uzembe. Hapana hakuna utafiti unafanyika. Ukarimu ni fadhila ambayo inasimama katikati ya uchoyo na kutapanya hovyo. Krismasi tunayoingojea sio kipindi cha kutapanya hovyo. Wengine wanatapanya hovyo mpaka wanatumia karo za watoto wao.

Unyenyekevu unasimama katikati ya majivuno na kujidhalilisha. Majivuno ni bonde. Unyenyekevu ni tambarare. Kujidhalilisha ni mlima. Unyenyekevu ukizidi kupindukia ni kujidhalilisha. Fadhila ya ujasiri inasimama katikati ya ujasiri wa kipumbavu au ujasiri bila busara na woga. Ugumu ni namna ya kupima ni hapa busara inapohitajika. Woga ni bonde. Ujasiri bila busara ni mlima.
“Anaamrisha mabonde yafukiwe, vilima na milima kusawazishwa, kuonesha kuwa kanuni ya fadhila haipungukiwi uzuri na wala haivuki na kupita kiasi,” alisema Baba wa Kanisa Gregory wa Nyassa.  Bonde na milima vinaonyesha kuzidisha na kuharibu fadhila ama kupunguza na kuharibu fadhila. Mfano wa bonde la ukarimu ni uchoyo. Mlima wa ukarimu ni kutapanya hovyo.Bonde katika barabara ya unyenyekevu ni majivuno. Mlima katika barabara ya unyenyekevu ni kujidhalilisha. Kinachoitajiwa ni tambarare yaaani ukarimu, unyenyekevu na ujasiri


Bonde
Tambarare
Mlima
Uchoyo
Ukarimu
Kutapanya Hovyo
Woga
Ujasiri
Ujeuri/uchokozi/Kutojali
Majivuno
Unyenyekevu
Kujidhalilisha
Ulevi
Kiasi
Kutojali afya
Uzembe
Busara
Ulaghai
Kukosa Subira
Subira
Kutojali


Tambarare ya Subira
Subira inasimama katikati ya kukosa subira na hali ya kutojali. Kuna methali za Kiswahili zinazosisitiza tuwe na fadhila ya subira: Subira ni ufunguo wa faraja. Subira huzaa mwana mwema. Subira huvuta heri. Kukosa subira ni bonde. Subira ni tambarare. Hali ya kutojali tena ni mlima. Nyosheni njia. Mwanafalsafa wa Kigiriki Aristotle alisema, “Mizizi ya subira ni michungu, lakini tunda lake ni tamu.” Inasemwa mvumilivu hula mbivu akivumilia sana anakula chungu. Subira ikizidi ni hali ya kutojali. Kukosa subira ni tabia ya watoto. Wanachotaka wanataka wakipate haraka: kama ni baisikeli ya kuchea, kompyuta ya kuchezea, pipi, andazi. Mtume Petro anatuhimiza tuwe na subira: “Lakini, wapenzi, msilisahau neno hili, kwamba kwa Bwana siku moja ni kama miaka elfu, na miaka elfu ni kama siku moja. Bwana hakawii kutimiza ahadi yake” ( 2 Petro 3: 10). Mtume Paulo anatutaka tuwe na subira kwa vile Mungu wetu ni Mungu wa Subira. Ufisadi unaweza kutokana na kutokuwa na subira: unataka kuwa na gari zuri sasa, nyumba nzuri sasa, simu ya gharama sasa. Subira ni kutofia madogo ya sasa, unangoja makubwa. Kuna mtu aliyekuwa na mazungumzo na Mungu, “Bwana nimekuwa nikishangaa juu ya muda. Miaka elfu moja kwako ni kama nini?” Mungu alimjibu, “Kwangu miaka elfu moja ni kama sekunde moja.”  Mtu huyo aliuliza, “Je kuhusu pesa? Dola milioni moja kwako ni kama nini?” Mungu alimjibu, “Kwangu dola milioni moja ni kama shilingi moja.” Mtu huyo alifurahi sana na kuwa na shauku na kusema, “Bwana unaweza kunipa hiyo shilingi moja?” Mungu akamwambia, “Hakuna shida, lakini utangoja sekunde moja.” Jua kwa Mungu sekunde moja inaweza kuwa kama miaka elfu moja. Dhambi za kukosa subira  ni nyingi. Kuiba ni dhambi ya kukosa subira badala ya kufanya kazi mtu anachukua njia fupi ambazo zinamfupisha kiroho. Uzinzi na uasherati ni dhambi za kukosa subira. Kipindi cha kungoja Krismasi ni kipindi cha kujifunza somo la subira.



Tambarare ya Ujasiri
Juu ya ujasiri Nelson Mandela alikuwa na haya ya kusema: “Nimejifunza maishani kwamba ujasiri maana yake si ukosefu wa woga; bali ni ushindi dhidi ya woga, na kwamba shujaa si yule ambaye hana woga; bali ni yule anayeushinda woga.” Khruschchev aliposimama na kutoa shutuma zake dhidi ya utawala wa Stalini katika ukumbi wa Congress, mtu mmoja alisema, “Ulikuwa wapi Komredi Khruschchev wakati watu wasiokuwa na hatia walipochinjwa ?”Khruschchev alinyamaza kwa muda na kutazama watu kwa makini na kusema: “Yule aliyesema hayo asimame tafadhali”. Watu ukumbini walishikwa na wasiwasi, mahangaiko na fadhaa, hakuonekana wa kujitingisha wala kujikuna. Ndipo baadaye Khruschchev aliposema: “Yeyote uwaye sasa hivi unajibu, nilikuwa katika hali uliyomo sasa”.
Tambarare ya Ukarimu
“Unaweza kutoa bila kupenda lakini hawezi kupenda bila kutoa,” alisema, Robert Louis Stevenson. Kuna mtu aliyeenda kwa tajiri kuomba elfu tatu. Tajiri akampa elfu hamsini. Yule aliyeomba elfu tatu akashangaa na kusema, “Bwana Mkubwa, Chifu, Bosi! Mimi nimeomba elfu tatu wewe mbona umenipa hamsini.” Bwana huyo akasema, “Elfu tatu zinakutosha wewe kuomba lakini hazinitoshi mimi kutoa.” Hivyo kutoa ni moyo vidole huachia. Uchoyo ni adui wa ukarimu. Mweheshimiwa Rais Mwai Kibaki alitoa maneno ya hekima juu ya uchoyo. Alisema, “Uongozi ni fursa ya kuyaboresha maisha ya wengine. Sio fursa ya kuridhisha uchoyo wa mtu.” Kusema kweli maneno kwenye kanga au leso za wanawake yanasema, yote. Kula unibakizie. Ni ukarimu kuwabakizia wengine. Uchoyo ni chanzo cha kuzika haki. Uchoyo hauna malipo.

Tambarare ya Unyenyekevu
Somo la unyenyekevu tunalipata toka mahali pengi. Nyota hazilifuniki jua. Nyota hazishindani na mwanga wa jua. Nyota zinatupa somo la unyenyekevu. “Unyenyekevu unamaanisha mambo mawili. Kwanza, ni uwezo wa kujikosoa…Sifa ya pili ni kuwaruhusu wengine wang’ae, kuwakubali wengine, kuwawezesha na kuwafanya wawe na uwezo,” alisema Cornel West mwanafalsafa wa Amerika aliyezaliwa 1953. Kama ambavyo huwezi kuzuia nyota sizing’ae hauwezi kuzuiwa using’ae ingawa unawezwa kucheleweshwa.
Kunyenyekea ni kumfanyia mtu kitendo kinachoonyesha heshima kubwa. Ni kutii.Kadiri ya Kamusi ya Karne ya 21 nyenyekea maana yake  ni kuwa mtiifu sana kwa matarajio ya kupata kitu fulani. Unyenyekevu ni kukubali nafasi Mungu aliyokupa iwe ya kiti cha mbele au ya kiti cha nyuma. Unyenyekevu una faida nyingi. “Hakuna kitu kinachomweka mtu mbali na mkono wa shetani kama unyenyekevu,” alisema Jonathan Edwards. Pia unyenyekevu huzaa fadhila nyingine. “Unyenyekevu ni mzizi, mama, nesi, msingi, na kiungo cha fadhila zote,” alisema Mtakatifu Yohane Chrysostom (347 – 407). Unyenyekevu unatambulika katika mambo ya kila siku. Kufanya kazi ndogo ndogo kwa mtu mkubwa ni unyenyekevu. Balozi toka nchi ya kigeni alimtembelea zamani Rais wa Amerika Abraham Lincoln akamkuta anang’arisha viatu vyake. “Nini hii, Rais unapaka dawa viatu vyako wewe mwenyewe?” Rais alimjibu, “Ndiyo, wewe huwa unapaka vya nani?” Zaidi ya hayo kuwa tayari kushukuru ni ishara ya unyenyekevu. “Maneno nakushukuru ni sala nzuri sana ambayo mtu yeyote anaweza kusali. Naisali sala hiyo mara nyingi. Maneno nakushukuru yanabainisha shukrani isiyo na kifani, unyenyekevu na kuelewa,” alisema Alice Walker mshairi wa Amerika aliyezaliwa mwaka 1944. Yote yakishasemwa, nakubaliana na Mignon McLaughlin (1913 -1983) mwandishi wa Amerika, aliyesema, “Mtu mwenye majivuno anaweza kujifunza unyenyekevu, lakini atajivunia unyenyekevu huo.” La msingi nyenyekea ule vya Mungu. Upate neema ya Mungu. Ili Mungu akuinue lazima kunyenyekea.

Counter

You are visitor since April'08